UCHAMBUZI WA TAMTHILIYA-MORANI


UHAKIKI  WA TAMTHILIYA
TAMTHILIYA: MORANI
MWANDISHI : E. MBOGO
WACHAPISHAJI : DUP
MWAKA : 1993
UTANGULIZI
Morani ni tamthiliya inayoelezea  juu ya matatizo yaliyoikumba nchi yetu mwaka 1980 na kusababisha hali ngumu ya uchumi kwa tabaka la chini.Matatizo haya ni kama uhujumu uchumi, wizi wa mali ya umma, ulanguzi, rushwa na kukosekana kwa haki, unafiki wa viongozi wetu, matabaka,n.k.Mwandishi wa tamthiliya hii, E.Mbogo anaonesha kuwa, kukithiri huko kunakwamisha maendeleo hapa nchini.
MAUDHUI
Dhamira Kuu: Ujenzi wa jamii mpya
Ujenzi wa jamii mpya ndiyo dhamira kuu ya tamthiliya hii ya Morani. Katika kujadili dhamira hii mwandishi anapendekeza kuwa jamii mpya itakayojengwa iwe jamii inayopinga aina yoyote ya unyonyaji,ukoloni mamboleo pamoja na wahujumu uchumi wa nchi, msanii anasema,
‘’ Tuandike risala itakayoamsha chuki dhidi ya ubeberu, ukoloni mamboleo, risala yenye mishale ya sumu.Sumu itakayounguza maini na mapafu ya wahujumu uchumi,mabepari uchwara na vibaraka popote walipo’’ (uk 41)
Msanii anaonesha wazi nia yake ya kupinga unyonyaji na uhujumu katika jamii itakayojengwa ili kuleta haki na usawa kwa kila mtu.Vile vile msanii anapendekeza kuwa, katika jamii hiyo mpya,lazima njia kuu za kuzalisha mali zimilikiwe na umma.Msanii anasema,
’ Tena risala hii iwakumbushe wananchi sherehe za harusi – matanga : sherehe za kutaifisha viwanda,mabenki,majumba,mashamba,hospitali na maduka kila kitu mali ya umma’’ (uk 4)
Hapa msanii anakumbusha kuwa ili umma umiliki njia hizi ni lazima zitaifishwe toka kwa watu binafsi na ziwekwe mikononi mwa umma ambapo zitatumika kwa faida ya umma.Katika kujadili dhamira hii, mwandishi anaona kuwa ili tujenge jamii mpya ni lazima jamii iungane kuwa kitu kimoja, kwani umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu, msanii anasema,
’Risala itoe mwito kwa Morani wote,Morani waungane ili kuendeleza safari ya kuitafutanguzo ya uswezi’’ (uk 41)
Pili,msanii anaonesha kuwa, ili tujenge jamii lazima tujitoe mhanga,Tuwe na ujasiri na ushujaa ili tusiogope upinzani wa watu wanaonyonya.Vile vile msanii anawahimiza wanajamii kushika silaha ili kuweza kujenga jamii mpya. Hivyo anasema,
‘’Enyi Morani nyakueni sime na ngao ili kulitetea dongo’’ (uk 44)
Dongo na Jalia ni mfano mzuri wa watu waliojitoa mhanga kupigania ujenzi wa jamii mpya. Hawa hawajali upinzani wa aina yoyote wakisaidiwa na Mapoto,Malongo na Hadikwa. Hawa wapo mstari wa mbele katika ujenzi wa jamii mpya ambayo itafutilia mbali ukoloni mamboleo na aina zote za unyonyaji (uk 40-42)
Vile vile msanii anatahadharisha kuwa katika ujenzi wa jamii mpya kuna wasiliti wasiopenda mafanikio ya umma. Yusufu na Mlemeta ni mfano wa waliopewa jukumu la kuliongoza gurudumu la ujenzi wa jamii mpya, lakini kutokana na ubinafsi pamoja na kushirikiana na wahujumu,wanakwamisha zoezi zima la ujenzi wa jamii mpya (sehemu ya pili, tatu na nne).

MBINU ZA UJENZI WA JAMII MPYA

1.   KUPIGA VITA UHUJUMU UCHUMI WA NCHI
Msanii anaonesha kuwa uhujumu uchumi ni kikwazo cha ujenzi wa jamii mpya.Katika tamthiliya hii,msanii anaonesha kuwa wafanyabiashara wengine pamoja na viongozi wa juu ndio wahujumu uchumi wakubwa, kwani wanavusha mazao  kwenda nchi za nje. Nungunungu ni mfano wa watu matajiri wahujumu uchumi  wanchi.Msanii anasema,
‘’ Ufahamu kuwa Nungunungu anavusha kahawa na karafuu  katika nchi ya jirani kwa magendo?Husemi? Sawa! Mlemeta unajua kuwa Nungunungu ana hoteli kubwa Marekani? Ana akaunti ya fedha Uswisi, Eee’’ (uk 12)
Msanii anaonesha kuwa  vitendo kama hivyo vinalikosesha taifa kupata fedha ambazo zingetumika kuendeleza nchi na badala yake pesa hizo zinaingia mikononi mwa watu binafsi kwa faida yao binafsi.Kana kwamba haitoshi ,Nungunungu pia anaingilia kuvusha madini nje kwa magendo kama anavyosema jalia;
’Ninyi ndio mnaotuvurugia nchi,Mbona husemi chochote kuhusu kahawa na Tanzanite mnazovusha nje kwa magendo? Mbona husemi lolote kuhusu madola yenu mnayolundika  ughaibuni? Hata ufunike mavi kwa bakuli haitakusaidia kitu’’ (uk 29)
Msanii anaonesha kuwa uhujumu uchumi  unakwamisha maendeleo  na watu wanaohujumu ni watu wa juu wala sio wa chini,msanii asema;’Katikati hakuna wahujumu, wahujumu wako juu’’ (uk 13)
Katika harakati za kutokomeza uhujumu uchumi unakwamisha maendeleo, na watu wanaohujumu ni watu wa juu wala sio wa chini, msanii asema;
‘’ Hatuwezi kuacha mapapa tukavuna pelege’’ (uk 13)
Hapa mapapa huwakilisha watu wa tabaka la juu wanaohujumu uchumi wanchi ambao huvusha mazao nchi za jirani.Wana akaunti,mahoteli nchi za nje na kulikosesha taifa pesa na Pelege ni watu wa kawaida wanaohujumu uchumi wanchi. Hivyo msanii anapendekeza kuwa vita dhidi ya wahujumu uchumi lazima vianze kwa mapapa na sio pelege.
 Uhujumu uchumi,magendo na ulanguzi vinapokithiri katika nchi husababisha  uadimu wa bidhaa muhimu.Bidhaa zinapoadimika zile chache zinazopatikana huwa ghali sana kiasi kwamba,watu wa tabaka la chini hushindwa kuzinunua na kubaki kuwa za watu wa juu tu.Msanii anasema;
’Vitu vimepanda bei chumvi,mchele,sukari,unga kila kitu.Ninyi tu mnaolalia magodoro ya manoti ndio mnaozimudu hizo bei,makabwela na watoto wao wakale wapi? (uk 29)
Hapo msanii anaonesha hali halisi iliyopo kwenye jamii; wakati wengine wanalalia manoti ya fedha watu wa chini wanashindwa hata pesa ya kununulia chumvi kwa sababu ya bei yake kuwa juu.Hii inasababisha hali ngumu ya maisha kwa tabaka la chini.Hivyo kujaa vitu madukani hakusaidii lolote kutatua shida za maskini.Kwani vitu vinauzwa kwa bei ghali kiasi kwamba wanakosa hela ya kununulia.
Msanii anasema;
‘’Tena risala hii ieleze jinsi maisha yalivyo magumu kwa watu wa chini,ieleze jinsi maduka yalivyojaa vitu, vitu vyenye bei ya kutisha makabwela na watoto wao wakiendelea kuandamwa na utapiamlo.’’(uk 41)
Pia msanii anasema fedha kidogo zinazopatikana badala ya kuendeleza uchumi zinatumika kununua vitu vya anasa ili kuwanufaisha wenye hela kama Nungunungu (uk 41)
Msanii anaeleza kwa masikitiko makubwa kuwa nchi yetu ni tajiri, lakini ni kutokana na kuhujumiwa na wachache ndiyo maana uchumi wetu uko chini ukilinganisha na nchi nyingine.Msanii anasema;
’Tena risala hii ieleze jinsi nchi ilivyotajiri, ardhi tele, maji, maziwa, mamilioni ya ng’ombe, mbuzi, kondoo, samaki na kwamba kusingizia hali ya hewa na opeki ni uzandiki-dhambi nyekundu pyu isiyofutika wala kusameheka’’ (uk 42)
Hivyo msanii anasema, ilikujenga jamii mpya ni lazima tupige vita wahujumu uchumi wanchi.Kwa upande mwingine vita iliyoanzishwa dhidi ya uhujumu uchumi ilionekana kama ni kuwaonea wahujumu uchumi hao. Wao walifikiri vita hii imeanzishwa na wachache wenye wivu dhidi yao. Nungunungu mmoja wa wenye mawazo hayo anasema;
‘’Hii kampeni mmeivaa kama koti la kutungua. Akina Fulani wachache wameibua hii vurugu isiyokuwa na mbele wala nyuma’’ (uk 29)
Kwa upande wa wahujumu uchumi wao wanaona hizi kampeni kama vurugu za kuwavurugia maslahi yao kama anavyosema Nungunungu;
’Ukifungua duka unaambiwa hujuma, mtu akinunua lori hujuma?,Ukijenga kajumba ka ghorofa moja hujuma, ukiweka vielfu vichache benki hujuma.Baadae mtasema mtu akioa wake wawili au watatu pia ni hujuma? Uyai huo? Mnataka kutuvurugia nchi’’ (uk 29)
Mawazo kama haya anayosema Nungunungu ni potofu, kwani haelezi waziwazi hizo pesa kapata wapi, labda kama tungekubaliana naye. Katika Morani msanii anasema ili tujenge jamii mpya lazima tupige vita wahujumu,kwani wanakwamisha zoezi hilo.
2.   KUPIGA VITA UNAFIKI NA USALITI
Unafiki ni hali ya mtu kutokuwa mkweli au hali ya kujifanya mkweli huku sivyo.Katika Morani msanii anasema wazi kuwa zoezi la kupiga vita uhujumu uchumi nchini lilikwama kutokana na wasimamizi kuwa wanafiki.Yusufu na Mlemeta ni mfano wa watu wanaowakilisha suala hili.Hii ni kwasababu walinunuliwa na Nungunungu kama asemavyo Jalia:
‘’ Mlemeta kama wewe umenunuliwa siyo mimi’’ (uk 13).
Kutokana na kununuliwa huko wanashindwa kumuweka Nungunungu kwenye orodha ya wahujumu uchumi na hivyo kukwamisha zoezi zima. Licha ya hiyo Yusufu na Mlemeta wako mstari wa mbele kutetea hujuma.Wanawazuia askari ili wasimkamate Nungunungu.Mlemeta anasema;
’Na wewe mzee umeponea chupuchupu kama tusingetumia mbinu ya kuzuia askari wa Jalia, basi sa hii tungekuwa tunazungumza hadithi nyingine’’ (uk 23).
Wakati wahujumu wengi wamekamatwa na mali zao kufilisiwa, Nungunungu analindwa na watekelezaji wa kampeni hiyo. Kana kwamba hiyo haitoshi,Mlemeta na Yusufu wamepewa jukumu la kumtafutia Nungunungu wakili pindi akamatwapo,kama msanii asemavyo;
Nungunungu: ‘’ Itabidi mwende mkamuone…..advocate mpange kila kitu tayari. Lazima ahakikishe nikiwekwa ndani, nishinde kesi’’.
Mlemeta: Sawa mzee’’ (uk 24).
Kutokana na Yusufu na Mlemeta kutetea hujuma, wanakwamisha zoezi la ujenzi kwa jamii mpya na ili tujenge jamii mpya lazima tuwaondoe watu kama hao. Msanii hakuishia hapo tu, anasema pia utaona wanaopinga maendeleao ya nchi ndio kwanza wanapandishwa vyeo na kuwa mabalozi Uchina, na kuwa mkuu wa jimbo. Hapo msanii anakejeli tabia za nchi yetu ya kuwapandisha madarakani watenda maovu na kuacha wale watimizao vema  wajibu wao. (uk 37).



3.   KUPIGA VITA MATABAKA
 Ni hali kuishi kutokana na kipato,cheo n.k. Msanii ameonesha matabaka ya aina mbili. Kwanza,kuna tabaka la juu yaani la wenye pesa.Tabaka hili humiliki njia kuu za uzalishaji mali, vyombo vya dola, ili kulinda maslahi yao  kama vile; pesa na vitega uchumi nchi za nje (uk 12). Pia tabaka hili hupata hudumu muhimu kama matibabu bila matatizo yoyote (uk 38). Msanii anaonesha kuwa tabaka hili pia hupendelewa kwenye sheria pindi wapelekwapo.Kwa kuelezea kesi ya Nungunungu msanii anadhihirisha hayo;
’Basi unajua yule Jaji alifungua mbuku wake mweusi wa sheria akasoma ….kamati na mahakama imechunguza na kuona kuwa hakuna ushahidi wowote kuwa ndugu Nungunungu amejihusisha na biashara haramu. Mahakama inaridhika na bila mashaka kuwa ushahidi uliotolewa dhidi ya Nungunungu ni majungu matupu yenye nia ya kumpaka matope. Hivyo mahakama inamwachilia Nungunungu huru’’ (uk 34)
Kwa upande mwingine tabaka hili wapo mstari wa mbele kufanya biashara haramu inayohujumu uchumi wetu.Tabaka la pili ni la chini, kwanza maisha yao ni duni ukilinganisha na tabaka la juu (uk 41).Hufanyishwa kazi ngumu na tabaka la juu yaani mizuke (uk 2) na pia hunyanyaswa na vyombo vya sharia kama vile mahakama ukilinganisha na tabaka la juu.Msanii anasema;
‘’Juzi juzi kasimama msulupwete,yule mbele ya mahakama.Hakimu wala hakujisumbua kufungua ule mbuku wake wa sharia.Hakupoteza muda.Hakupoteza muda. Aliegesha miwani yake katika ncha ya pua jicho kali la hakimu lilimtambaa kabwela toka vidoleni hadi utosini.Mvua saba, kazi ngumu!....Mvua saba!! Muhujumu uchumi mkubwa!Eti kakutwa nyumbani kwake na tenga mbili za kisamvu na dawa tatu za kolgeti.Dawa tu za mswaki.Maskini haokoti,akiokota – mwizi’’ (uk 35)
Msanii anaonesha jinsi vyombo vya sheria vinavyowatendea watu wa tabaka la chini kutokana na kutokuwa na sauti yoyote katika jamii. Tabaka hili linanyonywa, kunyanyaswa,kuonewa na kugandamizwa.Ili tujenge jamii mpya lazima tuondoe
matabaka haya katika jamii zetu.

4.   KUJITOA MHANGA
Msanii anaonesha kuwa,ili tujenge jamii mpya ni lazima tujitoe mhanga katika kuondoa unyonyaji na uonevu wa kila aina.Dongo,Jalia,Mapoto,Malongo na Hadikwa ni mfano mzuri wa wahusika waliopo mbele katika kupiga vita hujuma.Mzee,Malongo na Mapoto walijitoa mhanga kwa safari ya mbali kufuata nguzo ya uswezi,ingawa safari yao ilikuwa ya shida sana lakini hawakukata tamaa (uk 7-8).
Pia Jalia alionesha ujasiri bila woga kwenda kwa Nungunungu kumpiga (uk 28-30) na kuongoza harakati za kupiga vita hujuma (uk 40-45).Pia aliwakemea Yusufu na Mlemeta kuwa wamenunuliwa na Nungunungu bila woga,hata walipotaka kumpiga,alimpiga Yusufu na wala hakujali lolote (uk 12-14)
Kwa upande mwingine, tunamwona Dongo akipambana na wahujumu uchumi  ili kuwaendeleza na kuwasaidia wanyonywaji bila kuogopa kitu chochote.Na ni kutokana na msimamo wake wa kutoteteleka anauwawa na wahujumu (uk 43-45).
Ili tujenge jamii mpya ni lazima tuwe na ujasiri na ushujaa kwani bila ya vitu hivi hatuwezi kujenga jamii mpya.
5.   KUWA NA UMOJA NA MSHIKAMANO
Msanii anaonesha kuwa, ili tujenge jamii mpya lazima tuwe na umoja kwani umoja ninguvu na utengano ni udhaifu.Msanii anawahimiza wana Morani waungane ili waweze kupiga vita hujuma nchini. Msanii anasema;
‘’ Morani waungane na umma.Waungane kuiendeleza kutafuta nguzo za uswezi’’ (uk 41)
Pia katika kauli mbalimbali za Dongo naye anawahimiza wana Morani ili kupiga vita hujuma.Ni kutokana na utengano uliokuwepo katika jamii ndio maana zoezi la kupiga vita wahujumu lilishindwa na matokeo yake kushindwa kujenga jamii mpya.
Mfano mzuri tunauona kupitia Yusufu na Mlemeta waliokuwa viongozi wa kusimamia zoezi hili walitofautiana na wenzao kwa ajilia ya ubinafsi,hivyo zoezi zima likakosa mshikamano miongoni mwa watekelezaji (uk 8-25).Msanii anapendekeza kuwa ili tujenge jamii mpya lazima umoja na mshikamano viwepo,kwani bila hivyo hatuwezi kufanikisha zoezi hilo.


6.   NAFASI YA MWANAMKE KATIKA JAMII
Msanii  amemchora mwanamke katika sura mbalimbali  kama ifutavyo:,
 kwanza kama mwanamapinduzi aliyeko mstari wa mbele katika kupiga vita hujumu. Jalia ni mfano wa mwanamke mwanamapinduzi katika kutokomeza hujuma akishirikiana na Dongo, Mapoto, Malongo na Hadikwa (uk 39-42).
Pili  kama jasiri,jalia aliwambia waziwazi kina Mlemeta na Yusufu kuwa, wamenunuliwa na Nungunungu ndio maana wakawa wanakwamisha zoezi zima la kuwakamata wahujumu (uk 13-18).
Pia Jalia ndiye aliongoza kikosi cha kwenda kumkamata Nungunungualiyeogopwa na watu wote kwa ajili ya umaarufu wake.Licha ya kumkamata alimwambia wazi madhambi yake aliyoyafanya (uk 28-30). Kama hiyo haitoshi Jalia alimpiga Nungunungu bila kuogopa vitisho vyake atoavyo kwa wengine tena bila wasiwasi (uk 38). Katika kuandaa mipango ya kupinga hujuma,Jalia alifanya kazi bega kwa bega na akina Mapoto bila kujali vitisho alivyopewa na Nungunungu (uk 40). Kwa upande mwingine mwanamke amechorwa kama chombo cha kustarehesha wanaume. Rejea Aisha alivyomstarehesha Nungunungu (uk 26-27).
7.   UZURUFU
Katika tamthiliya hii msanii  ameonesha jinsi wazee wanavyofanya mapenzi na watoto wadogo.Mfano mmoja wapo ni Nungunungu ambaye anafanya mapenzi na Aisha ambaye ni mwanafunzi.Kutokana na hali hiyo,Aisha anasahau hata kwenda shule na matokeo yake anafukuzwa shule.Msanii anasema (uk 26);
Nungu: Nini Aisha!!!
Aisha: Wamenifukuza shule
Nungu: (Anagutuka) Ee! Umefanya nini?
Aisha: Nakueleza mie!
Kitendo cha watu wazima kufanya mapenzi na watoto wa shule kina madhara yake kwa jamii kama tulivyooneshwa hapo juu, mtoto anaweza kufukuzwa shule au anaweza kupata mimba au magonjwa ya zinaa.
Aisha alifukuzwa shule kwa sababu hakwenda siku nyingi; na hakwenda shule kwa sababu ya starehe alizokuwa anapewa na Nungunungu usiku kucha. Msanii anasema (uk 26);
Aisha: Siku nyingi sijaenda shule mie mwezi.Walimu wamemletea barua mzee. Wamenifuta….utanisamehe mpenzi Nungu.
Nungu: (Anamsukuma) mpumbavu mkubwa. Hutaki shule halafu unakuja kunililia mimi? Mpumbavu mkubwa?
Aisha:Mpumbavu! Mpumbavu mimi? Mimi mpumbavu?Siku zote narudi saa nne usiku nyumbani baada ya hekaheka za night-club mimi na wewe. Ulitegemea nini?Ee?
Matukio kama haya yapo katika jamii yetu. Akina Nungunungu wako wengi na akina Aisha nao wapo wengi. Jambo la muhimu ni kupiga vita vitendo kama hivyo.Vitendo vya kurubuni watoto wa shule kwa hela zao nyingi halafu wanawaharibia maisha yao ya baadaye,ni kinyume na maadili ya jamii.Nungunungu alimfundisha Aisha umalaya, ulevi na kuvuta sigara kitu ambacho ni kinyume na maadili ya jamii.Waswahilii husema mshika mawili mmoja humponyoka,na ukweli Aisha alifukuzwa shule,kwani aliendekeza starehe.Starehe hizo zikamfanya asahau shule na matokeo yake alifukuzwa shule.
MIGOGORO
v Mgogoro wa wahujumu uchumi na wale wapiga vita wahujumuuchumi.
v Mgogoro kati ya Jalia na Mlemeta pamoja na Yusufu.
v Mgogoro kati ya Malongo na Yusufu kwenye baa.
v Mgogoro kati ya Jalia na Nungunungu.
v Mgogoro kati ya Aisha na Nungunungu.
UJUMBE
Ø Hujuma,unafiki na kuwepo kwa matabaka katika jamii ni kikwazo cha ujenzi wa jamii mpya.
Ø Umoja na mshikamano, ujasiri na ushujaa  na kujitolea mhanga ni mbinu za kujenga jamii mpya.
Ø Kikulacho ki-nguoni mwako, yule anayekwamisha maendeleo ya nchi ni mwananchi mwenyewe – Nungunungu, Mlemeta na Yusufu.
Ø Kupiga vita ukoloni,ukoloni mamboleo na aina yoyote ile ya unyonyaji ni mbinu muhimu za ujenzi wa jamii mpya.
FALSAFA
Msanii anaamini kuwa wahujumu uchumi wetu ndio wanaokwamisha ujenzi wa jamii mpya.Msanii anasema lazima tuwaondoe wahujumu hao,tupige vita aina zote za unyonyaji.
MSIMAMO
Msimamo wa msanii ni wa kimapinduzi,kwani ameonesha waziwazi matatizo yanayoikabili jamii yetu na kuonesha kuwa matatizo haya ni pamoja na hujuma,unafiki, rushwa,matabaka na kupeana kazi kwa kujuana (uk 27).
FANI
MUUNDO
Mwandishi ametumia muundo wa moja kwa moja.Mchezo unaanza kuonesha kifo cha Dongo na utata uliojitokeza kwa wananchi juu ya kifo chake,Mchezo unaendelea kwa kueleza vita dhidi ya wahujumu uchumi na matokeo yake.Mchezo umegawanyika katika sehemu nne.

MTINDO
Msanii ametumia dayolojia ilivyo kawaida kwa tamthiliya – maelezo ya majibizano baina ya wahusika. Pia msanii ametumia nafsi zote tatu (yaani I, II, III)
Pia msanii ametumia nyimbo katika mchezo huu (uk 42).
MATUMIZI YA LUGHA
Lugha aliyotumia msanii ni ya kawaida inaeleweka na imejaa misemo,methali, tamathali za semi na mbinu nyingine za kisanaa.
MISEMO / NAHAU
v Ndumi la kuwili (uk 13)
v Anatuchomea utambi ( uk 15).
v Paka shume (uk 17).
v Kuwapaka watu matope (uk 29).
v Umeota meno jana (uk 8).
METHALI
v Penye nia pana njia na subira yavuta heri (uk 4)
v Siri ya kaburi aijua maiti na siri ya maiti aijua kaburi
v Fimbo ya mbali haiuwi nyoka (uk  23)
v Mfuga punda fadhila hukujambia  mashuzi (uk 23)
v Mwosha huoshwa (uk 24)
v Bandu bandu unataka kumaliza gogo? (uk 31)
v Usimsifu sana lasivyo tembo atalitia maji (uk 23)
v Mwenzako akinyolewa wewe tia maji (uk 23)
TAMATHALI ZA SEMI
TASHIBIHA
v Kesho tutawasambaza kama punje za mtama.
v Nungunungu na Mlemeta ni kama kupe na mkia wa ng’ombe.
v Watu wengi kama sisimizi (uk 39).
v Hii kampeni mmevaa tu kama koti la kutungua (uk 29).
TASHIHISI
v Jicho kali la hakimu lilimtambaa Kabwela Yule toka vidoleni hadi utosini.
v Jua lilipo tabasamu na kutandaza mbawa zake.
TAFSIDA
v Nikakumbatie blanketi mwenyewe? (uk 27)
v Tutaenda umana au wasiwasi? (uk 27).
MBINU NYINGINE ZA KISANAA
TANAKALI SAUTI
v Uuuuu!Uuuuuu!Dongo! Dongo jamaa.............(uk 1)
v  
TAKRIRI
v Mpumbavu mimi? Mimi  mpumbavu? (UK 26).
v Nimekosa nimekosa niseme hivi niseme (uk 22).
v Mnachuja, mnachuja mnachuja hadi lini? Mlemeta.
MDOKEZO
v Hallo bado tunaendelea na kazi .......mambo magumu mzee.....lakini nadhani tutayamudu......yaa saa ngapi.....sawa (uk 15)
v Lakini mzee.........(uk 18).
PICHA /TASWIRA
Msanii pia katumia lugha ya picha (uk 2), kuna picha ya mizuka inayolima shamba la tajiri – hiyo huwakilisha tabaka la wanyonge,watu wanaofanya kazi kubwa kwa kuwatajirisha matajiri wakati wao wenyewe wananyonywa.
Pili,kuna nguzo ya uswezi hii inaashiria mali za azimio la Arusha.Dongo anaashiria wanamapinduzi wanaotaka kuleta mabadiliko ya kisiasa, kiuchumi na utamaduni.Mti uliokuwa karibu na ofisi pamoja na wachawi hizi zote mbili huashiria wahujumu uchumi wetu.
Morani inaashiria vijana wanaotakiwa kuungana ili kuleta mabadiliko katika jamii.

WAHUSIKA
1.   DONGO
v Huyu ni mhusika mkuu wa tamthiliya hii anayepambana na hujuma ili kuwaendeleza na kuwasaidia wanyonge.
v Dongo alikuwa mstari wa mbele katika kupiga vita hujuma akisaidiwa na  Mapoto, Jalia, Malongo, Hadikwa. Dongo ni mfano wa viongozi wanamapinduzi anayefaa kuigwa na jamii.
2.   JALIA
v Ni mhusika mwanamke aliyejitoa mhanga kuongoza kampeni ya kutokomeza hujuma.
v Jalia aliongoza askari kumkamata Nungunungu bila woga.
v Pia katika maandalizi ya maandamano  Jalia alishirikiana na Mapoto, Malongo na Hadikwa katika kufanikisha maandamano hayo.
v Vilevile  alimpiga Yusufu na Nungunungu bila woga wala wasiwasi. Hivyo Jalia ni mwanamke anayefaa kuigwa na jamii kutokana na matendo yake.
3.   MAPOTO NA MALONGO
Hawa ni wahusika wadogo wa tamthiliya hii.
v Hawa wako pia mstari wa mbele kupiga vita rushwa, ukoloni, ubepari na hujuma
v Walishitikiana bega kwa bega na Jalia katika vita hiyo.
v  Ni mfano mzuri wa kuigwa na watu katika jamii yetu.
4.   NUNGUNUNGU
v Huyu anawakilisha wahujumu uchumi.
v Alikuwa anavusha kahawa na karafuu nchi za nje kwa magendo.
v  Ana hoteli Marekani na akaunti Uswisi.
v Ni mfano wa watu wanaolikosesha taifa letu fedha za kigeni kwa kufanya magendo yao, na ni mfano wa mtu mbaya asiyehitajika kuigwa na yeyote.
5.   YUSUFU NA MLEMETA
v Hawa ni viongozi wanafiki walioko mstari wa mbele katika kukwamisha shughuli zote za maendeleo.
v  Wanashirikiana na Nungunungu kuihujumu nchi yetu.
v Wakati wa kampeni za kutokomeza hujuma, walileta wahujumu mfano Nungunungu,hivyo hawafai kuigwa na jamii.
Ø Wahusika wengine ni Mzee, Aisha, Dala Bongi, Okashi n.k.
MANDHARI
Mandhari yake ni ya Kitanzania kutokana na matukio yanayoelezwa katika tamthiliya hii, yalijitokeza wazi katika jamii yetu ya Kitanzania.Matukio haya ni kama vile hali ngumu ya maisha,hujuma na vita dhidi yake.Matukio haya  ndiyo yaliyotawala  Tanzania kuanzia miaka ya 1980 na kuendelea.Vile vile  kuna mandhari ya nyumbani, ofisini, porini, baa, kumbi za tarehe, mitaani, hospitalini, n.k.
JINA LA KITABU
Kwa ujumla  jina la kitabulinasadifu yale yaliyomo ndani ya kitabu,msanii anatoa wito kwa vijana – Morani ili waweze kuungana na umma katika kupiga vita hujuma nchini.

KUFAULU KWA MWANDISHI
Mwandishi amefaulu kwa  kiasi kikubwa kwa kuionesha jamiiyetu matatizo yanayoikabili kama vile umaskini, hujuma, hali ngumu ya maisha,matabaka, na unafiki wa viongozi wetu na ametoa wito kwa vijana kushirikiana katika kupiga vita matatizo hayo.
Pia msanii amefaulu katika kuwachora wahusika wake wanamapinduzi. Kwa upande mwingine msanii amefanikiwa katika kuoanisha jina la kitabu na yaliyomo. Morani ni vijana wa Kimasai wenye jukumu la kulinda jamii yao. Katika kitabu hiki msanii anatoa wito kwa morani(vijana) wote kupiga vita hujuma hapa nchini.
KUTOFAULU
Msanii ametumia taswira nyingi mno si rahisi kwa mtu wa elimu ya chini kupata maana zake na hivyo hushindwa kupata ujumbe uliokusudiwa na mwandishi.


Powered by Blogger.