UCHAMBUZI WA RIWAYA YA MFADHILI



UHAKIKI WA RIWAYA
KITABU:  MFADHILI
MWANDISHI: HUSSEIN TUWA
WACHAPISHAJI: MACMILLAN
MWAKA: 2007

UTANGULIZI
Mfadhili ni riwaya inayoelezea suala la mapenzi na ndoa, ikionesha matatizo mbalimbali yanayotokana na mapenzi na ndoa na athari zake kwa jamii. Ni riwaya inayoongelea juu ya penzi zito baina ya Gaddi Bullah na Dania Theobald na jinsi ambavyo penzi hilo lilivyoingiliwa na mitihani pamoja na majaribu makubwa.Riwaya hii imejadili kwa  mapana suala ya mapenzi na ndoa na athari zake kwa jamii.
MAUDHUI
Dhamira kuu: Mapenzi na ndoa
Msanii ameainisha aina mbili za mapenzi na ndoa;
v Mapenzi ya kweli
v Mapenzi ya uongo
 Mwandishi amejadili mapenzi ya kweli kama ifuatavyo;
  Mosi, mapenzi ya kweli,kati ya Gaddi Bullah na dada yake Bi Hanuna.Hawa walipendana kwelikweli na ndio maana mmoja alikua akiwa na tatizo lina kuwa ni tatizo la wote wawili,mtu akimuudhi Gaddi amemuudhi na dada yake Bi Hanuna pia  na walisaidiana katika shida zao zote.
       Pili,Mapenzi  ya kweli kati ya Gaddi Bullah na Dania, mwanzoni walipendana hasa mchana walikua wakienda kula chakula pamoja na hata walifika hatua ya kutembeleana. Gaddi katika kuonesha mapenzi ya dhati kwa Dania alimsaidia kwa kila hali wakati wa shida raha na (UK 101-106)
Hata baada ya Dania kumsaliti Gaddi bullahh, bado Gaddi bullah aliendelea  kumpenda  Dania na hata alimfadhili baada ya kusalitiwa na Jerry kwa mara ya pili.Alikubali kutoa ini lake ili Dania aendelee kuishi. (UK 137-139).
  Tatu,Mapenzi ya kweli kati ya Gaddi  Bullah na Junior mtoto wa Dania. Pamoja na kwamba Junior hakuwa mtoto wake.Gaddi alimpenda sana na ndio maana baada ya Junior kuumia mkono aliyempeleka hospital ni Gaddi Bullah na wala si baba yake Jerry (UK 146)
    Nne,Mapenzi  ya kweli kati ya Mama Mlole (Fausta) kwa wafanyakazi wa chini yake kama vile Gaddi Bullah na Dania. Pamoja na Gaddi Bullah kuharibu kazi, Mama Mlole alimtetea sana asifukuzwe kazi bali aangaliwe upya (UK 69-71). Vilevile alimtetea sana Dania asifutwe kazi kipindi anaumwa .Mama Mlole ni mfano wa viongozi wenye mapenzi ya kweli kwa wale anaowaongoza .
    Tano,Mapenzi ya dhati kati ya Nunu na Dania,Nunu alimsaidia sana Dania  kulea mtoto wake Junior wakati Dania yuko kituo cha kuponya walevi (UK 115). Pia Nunu alikua bega  kwa bega na wazazi wake Dania wakati wa magonjwa yote yake yaliyomkumba na alimsaidia kumtafuta Gaddi  Bullah na Bi Hanuna ili awaombe msamaha kwa yote aliyowatendea.
       Sita,Mapenzi ya dhati kati ya Nunu na Boazi; Hawa walipendana  kwa dhati na ndio maana shida ya Nunu ilikua shida ya Boazi pia. Nunu na Boazi walisaidana kwa hali na mali katika kumtafuta Gaddi Bullah aliyekuwa anatafutwa na Dania. Hata wakafikia hatua ya kuhatarisha maisha yao kumteka nyara Bi Hanuna kwa lengo la kumsaidia Dania (UK 36-56).
Saba,Mapenzi ya kweli kati  ya daktari Virani na Gaddi Bullah; Hawa walipendana sana na ndio maana Virani alimsaidia Gaddi Bullah katika matatizo mbalimbali kwa mfano; kumtibu mpenzi wake Dania.Vilevile   daktari Virani alihangaika sana kuokoa maisha ya Gaddi  Bullah kutokana na ugonjwa aliokuwa anaumwa ingawa hakufanikiwa.  Haya yote aliyafanya kwasababu alimpenda Gaddi  Bullah kwa dhati na Gaddi Bullah vilevile alimpenda Virani.
     Nane,Mapenzi mengine ya dhati ni kati ya Nunu na Gaddi Bullah;  Nunu alimpenda sana  Gaddi Bullahkwa dhati ndio maana alimshauri sana Dania asimwache Gaddi na kurudiana na Jerry . Si kwasababu alimsaliti, bali awe na Gaddi Bullah aliyemsaidia wakati wa shida (UK 114-115). Vilevile  Gaddi alimpenda pia Nunu kama rafiki mzuri anasema (UK 146).                                                                                                                                                            “…..Nunu ….”A…..bee! Nunu alitikia kwa upole huku akitiririkwa na machozi wewe….ni rafiki…  mzuri….”Gaddi alimwambia……”
  Tisa,Mapenzi ya dhati kati ya wazazi wa Dania kwa mtoto wao Dania. Wazazi hawa walimpenda sana mtoto wao ndio maana walimsaidia kwa hali na mali hadi wakampeleka Afrika ya kusini kutibiwa ugonjwa wake wa ulevi. Pia wakati wa ugonjwa wake wa ini ,wazazi wake walimsaidia sana mpaka hatua ya kuweka matangazo radioni  ili kumsaidia mtoto wao kwa mtu ambaye angejitolea ini. Hayo ni mapenzi ya dhati ya wazazi kwa binti yao.
      Pia mwandishi amejadili kwa kina mapenzi ya uongo kama ifuatavyo;
     Mosi,Mapenzi ya uongo  kati ya Jerry na Dania. Inaonyesha Jerry hakumpenda kwa dhati Dania na ndio maana alimsaliti wakati wa harusi yao. Jerry alipenda sana masomo kuliko kufunga ndoa na Dania. Jerry alitakiwa kutolewa ini moja ili waponye maisha ya Dania, lakini siku ilipofika hakufika hospitali bali alitokomea kusikojulikana(UK 133-135).
       Pili,Mapenzi  ya uongo ni kati ya rafiki yake Gaddi na Gaddi. Huyu hakuwa rafiki wa kweli kwani alimshauri vibaya Gaddi Bullah pale ambapo Gaddi alipomuomba ushauri kuhusu uwepo wa mabadiliko mabaya ya kimahusiano kati yake na mkewe rafiki yake alimshauri atafute nyumba ndogo. Pia alimtorosha mke wa Gaddi Bullah na kumuoa na akawa mkewe (UK 64-67).
 Tatu,mapenzi ya  uongo kati ya  Gaddi na Nyambuja. Gaddi alimpenda sana mkewe alimjali kwa kila kitu  Lakini mke wake Nyambuya hakuwa na mapenzi ya dhati katika ndoa yake. Baada ya mwaka mmoja tu wa ndoa yao, Nyambuja alianza kumsaliti mume wake kwa kuchelewa kurudi nyumbani, kusafiri bila taarifa kwa mume wake na mwisho akamwacha nakwenda kuolewa na rafiki yake Gaddi Bullah (UK 60-67).


DHAMIRA NDOGO NDOGO
1.     USALITI
Ni hali ya kufanya jmbo kinyume na makubaliano.Mwandishi ameonyesha namna wahusika walivyosalitiana pamoja na athari zake kama ifuatavyo;
 Mosi,Mwandishi ameonesha jinsi Nyambuja alivyomsaliti mumewe Gaddi Bullah kwa kufanya mapenzi nje ya ndoa na  aliamua kumwacha Gaddi Bullah  na kwenda kuolewa na rafiki yake Gaddi Bullah.
Pili,Mwandishi ameonesha jinsi Rafiki yake Gaddi  Bullah alivyomsaliti Gaddi Bullah  kwa kumnyang’anya mkewe Nyambuja. Matokeo ya usaliti huo yalimpelekea Gaddi bullah kushindwa kufanya  kwa ufanisi pamoja kasi ya itendaji wake kupungua. Hatimye akaandaliwa barua ya kumuonya na kutokana na mawazo mengi aliyokuwa nayo akasaini cheki feki za wizi (UK 62-63)
Tatu,Mwandishi ameonesha namna  Afisa usafirishaji  alivyomsaliti Gaddi Bullah kazini. Huyu aliandaa vocha ya malipo hewa ili  Gaddi Bullah aisaini . Matokeo yake Gaddi Bullah alishushwa cheo na kuhamishwa kituo chake cha Arusha  na kuja kufanya kazi Dar-es-salaam kwa uangalizi wa makao makubwa (UK 71-72).
Nne,Mwandishi  ameonesha namna Dania alivyomsaliti Gaddi Bullah.Kwanza Dania alimsaliti Gaddi kwa kutoandaa ripoti aliyotakiwa kuandaa kwa ajili ya kwenda kusoma kwenye kikao cha wakuu wa vitengo. Dania hakuandaa ripoti hiyo na siku ya kikao hakuonekana kazini hadi muda wa kikao ulipoanza saa mbili na nusu asubuhi (UK 77-79) na matokeo yake Gaddi Bullah alimwandikia barua ya onyo na kumtaka ajieleze ,lakini kwa busara ya mama Mlole alisuluhisha mgogoro huo.
Tano,Mwandishi ameonesha namna Dania alivyomsaliti Gaddi Bullah kwa kumwacha wakiwa katika mapenzi mazito na wakati huo huo wajindaa kufunga ndoa. Dania alimwacha Gaddi na kurudiana na Jerry ambaye alimsaliti siku ya harusi yake. Matokeo yake Gaddi  Bullah alipata shinikizo la moyo, kupigana na Jerry na dada yake Bi Hanuna kuwekwa ndani (Lupango).
Sita,Mwandishi ameonesha namna Jerry alivyomsaliti Dania,kwanza alimsaliti wakati wa harusi yao kwani Jerry kwani alikuwa Marekani na wakati huo  aliahidi angerudi ili wafunge ndoa. Na kutokana na usaliti huo harusi ilivunjwa na Dania alikonda sana hali  chakula  na akawa mlevi wa kupindukia wa pombe kali  na ikapelekea kupata ugonjwa wa ini (uk 83-87).
Saba,Mwandishi ameonesha namna Jerry alivyomsaliti Dania akiwa mgonjwa mahututi hospitalini kwa kuahidi kutoa ini lake moja ili amuokoe mpenzi wake Dania lakini hakufanya hivyo bali alimtoroka akiwa kitandani hospitalini (UK 133-134)
2.     NAFASI YA MWANAMKE KATIKA JAMII
 Mwandishi wa riwaya hii amemchora mwanamke katika nafasi au sura mbali mbali kama ifuatavyo;
v Mosi,Mwandishi amemchora mwanamke  kama kiumbe asiyekuwa na msimamo katika kufanya maamuzi. Mfano, Dania anaonekana kuwa  na maamuzi yasiyofaa kwa kutokuwa na msimamo na kuamua tena kumrudia Jerry ambaye alimuumiza mwanzoni.
v Pili,Mwandishi amemchora mwanamke  kama mtu mwenye huruma na mshauri mzuri. Mfano Nunu alimhurumia rafiki yake Dania na kumhangaikia kwa hali na mali wakati anaumwa.Pia alikuwa mshauri mzuri wa Dania.
v Tatu,Mwandishi amemchora Mwanamke kama mtu  jasiri. Mfano Nunu ambaye alifanya kazi kubwa sana ya kumpatanisha Dania na Gaddi Bullah hata akafikia hatua ya kumteka kwa nguvu dada yake Gaddi Bullah  Bi Hanuna ili aweze kuwasaidia kumpata Gaddi Bullah.
v Nne,Mwandishi amemchora mwanamke kama mtu katili na msaliti. Mwandishi amewaonesha  Nunu,Nyambuja na Dania walivyomsaliti Gaddi Bullah na hatimaye  kwenda kuolewa kwa wanaume wengine.
v Tano,Mwandishi amemchora kama mtu mwenye upedo,moyo wa huruma na moyo wa kusaidia.Mwandishi amemuonesha  mhusika Mama Mlole alivyokuwa na upendo na wafanyakazi wa chini yake.



3.     CHUKI
Mwandishi ameonesha namna baadhi ya wahusika walivyona chukiana au kuwa na chuki kwa wenzao kma ifuatavyo;
     Mosi,Bi Hanuna alikuwa na chuki na Nunu kwasababu ya Dania. Dania alimuacha kaka yake Gaddi  Bullah wakati wako katika mapenzi ya raha na furaha,kitendo hichi kilimuudhi sana Bi Hanuna. Hata Nunu alipokwenda kwake mkuranga kuomba msaada wa kusaidiwa  kuonana na Gaddi Bullah Bi Hanuna alikataa kumsikiliza kutokana na chuki aliyokuwa nayo (UK 25).
       Pili,Bi Hanuna alikuwa na  chuki kwa Dania .Hii ilitokea baada ya kumuacha kaka yake Gaddi Bullah na kumuweka ndani (Gerezani) Bi Hanuna.Mwandishi anaendelea kuonesha kuwa jinsi Bi Hanuna alivyokuwa anamuona mdogo wake akiteseka ndivyo alivyozidi kumchukia Dania (UK 125-126).
      Na kutokana na chuki aliyokuwa nayo Bi Hanuna kwa Dania ndiyo maana alikataa kuwaeleza Nunu na Boazi ailikokuwa Gaddi Bullah. Vile vile alikataa hata kuwapelekea barua kwa Gaddi Bullah iliyotoka kwa Dania kwaajili ya kuomba msamaha (UK 24-56). Pia Dania alionesha  chuki za waziwazi kwa Gaddi Bullah kwa kumuacha na kumuona kama mtu aliyemnyang’anya cheo chake.
  Tatu,Dania alikuwa na chuki kwa Gaddi Bullah, Hii ilipelekea Dania kuharibu kazi ili Gaddi Bullah aonekani hafai. Matokeo yake Dania akaandikiwa barua kali na Gaddi na kumuonya na kutaka ajielezee kwanini asifukuzwe kazi (UK 75-79).
Nne,Dania naye alikua na chuki na Jerry hasa baada ya kumuacha au kumtelekeza  wakati wa maandalizi yote ya harusi yao yamekamilika. Hata Jerry aliporudi kutoka Marekani alimfukuza kama mbwa nyumbani kwake (UK 107).
    Tano,Nunu alikuwa na chuki kwa Jerry kwasababu ya Jerry kumuacha rafiki yake Dania, hata Jerry alipokwenda kuomba msaada wa kumsaidia kumshawishi Dania alimfukuza na kumtaka asirudi tena nyumbani kwake (UK 109).
   Sita,Wazazi wake Dania nao walikua na chuki na Jerry kwasababu ya kumsaliti motto wao (UK 109-110).
 Mwandishi anaonesha kuwa wenye chuki ipo siku watasameheana na anaonyesha  Bi Hanuna anamsamehe Nunu, halafu Dania anamsamehe Jerry ingawa msamaha huo ulileta matatizo kwa Gaddi Bullah na Bi Hanuna. Hivyo msanii anaonesha kuwa ni muhimu kumsamehe mtu aliyekufanyia makosa.

4.     UMUHIMU WA UONGOZI BORA
Msanii amemtumia mhusika mama Mlole ambaye alikua kiongozi mzuri ambaye aliwajali wale aliowasimamia.
Gaddi Bullah alipata matatizo kazin yaliyotokana na athari za kuacwa na mkewe , mama Mlole aimtetea sana asifukuzwe kazi baada ya kumwelezea matatizo yake (UK 70). Pia alipendekeza Gaddi ahamishiwe DSM  ili aangaliwe zaidi badala ya kufukuzwa kazi.
Pia mama Mlole alimtetea Dania asifukuzwe kazi baada yakuachwa na Jerry. Baada ya ndoa kuvunjika, utendaji wake wa kazi uliathirika sana. Alifikia hatua anakwenda ofisini amelewa (UK 88) na hatua aliyofikia ilikua aachishwe kazi lakini mama Mlole kama Afisautumishi wakapuni alimtetea sana na akapendekeza apewe likizo bila malipo kwa muda wote akaokua kwenye matibabu ya ulevi wake (UK 88)
Msanii anataka kuifundisha jamii kuwa cheo ni dhamana lazima kukitumia kwa faida ya watu wote na sio kuwanyanyasa.

                            DHARAU
Msanii amemtumia Nyambuya kama mtu mtu mwenye dharau kwa mume wake,hata akiulizwa swali na mume wake majibu aliyokua akiyatoa yalikua yamejaa dharautupu (UK 60). Pia kitendo cha Nyambuya kusafiri safari za gafla na kumtaarifu mume wake kwa simu ni sehemu ya dharau. (UK 61)
Kitendo cha Nyambuja kufanya mapenzi na rafiki wa Gaddi na kumwacha Gaddi na kwenda kuolewa na rafiki yake Gaddi hiyo nayo ni dharau kwa mume wake. Hata barua aliyoiandika kwa Gaddi (UK 65) ilijaa dharau ya Nyambuja kwa Gaddi.
Dania pia alimdharau Gaddi siku ya kwanza tu alipomkuta ofsini kwake. Kitendo cha Dania kumuita Gddi kwamba wewe ni “Gaddi Bullah” (UK 73) ni sehemu ya dharau alioionyesha kwa Gaddi. Pia kitendo cha Dania kumfukuza Gaddi kwenye meza aliyokuwa amekaa na motto wake Junior kwenye bar ni sehemu ya dharau. Dania alimfukuza Gaddi kwenye meza kama mbwa mwizi.
Pia Dania alionesha dharau ya hali ya juu baada ya kumwacha Gaddi na kurudi kwa Jerry, majibu aliyokua anamjibu Gaddi yalikua majibu ya kijeuri na dharau tupu (UK 120-123).
 Lakini msanii anaitaadharisha jamii kuwa mtu anayemdharau baadae anaweza kukufaa. Dania alimwacha Gaddi , alimdharau  lakini baadae akawa mfadhiliwake baada ya kutelekezwa na Jerry kwa mara ya pili akiwa mgonjwa mahututi hospitalini,hivyo tuepuke dharau.
                      BIDII KATIKA KAZI
Msanii amemtumia Gaddi Bullah ambaye alionesha kuwa kijana mdogo lakini mchapa kazi mzur,alipendwa na wafanyakazi wote waliokuwa chini yake na hata wakuu wake wa kazi huko makao makuu (UK 59).
Pia Dania ambaye alikua mmoja kati ya wafanyakazi wenye nidhamu, bidii na ushirikianao. Pia aliwaheshimu wafanyakazi wote na wala hakuruhusu utajiri wa wazazi wake umpe kichwa.
Pia msanii anaonesha matatizo ya mtu binafsi au ya kifamilia yanaweza kupunguza bidii na ufanisi wa mtu katika kazi yake. (UK 63)
Kwa ufupi msanii anaonyesha kuwa bidii katika kazi ni kichocheo cha maendeleo ya jamii. Pia matatizo yanaweza kumfanya mtu achanganyikiwe, aache kazi na pia yanaweza kupunguza ufanisi katika kazi , kufukuzwa kazi au kushushwa cheo.

                      UJUMBE
Ø  Rafiki wa kweli ni Yule anayekusaidia au kukujali wakati wa shida.
Ø  Si kila king’aacho nidhahabu
Ø  Bidii na ufanisi katika kazi ni chanzo cha maendeleo katika jamii
Ø  Ni vigumu kumpata mtu mwenye mapenzi ya kweli au atakayekupenda kama unavyopenda wewe
Ø  Matatizo, majaribu, chuki na dharau ni vitu visivyoepukika katika mapenzi na ndoa
Ø  Mtu anapotenda kosa, lazima akubali kutubu kosa

                             FALSAFA
Msanii anaamini kuwa katika suala la mapenzi kuna kupenda na kutokupendwa, kunakuoa na kuachwa, hivyo ni vigumu kupata mtu mwenye mapenzi ya dhati.

                           MSIMAMO
Mwandishi ana msimamo wa kimapinduzi kwani anaonesha wazi kuwa katika suala la mapenzi na ndoa kuna matatizo yake. Watu lazima tukubali kusameheana kwani hujui ni yupi atakayekusaidia wakati wa shida.

                          MIGOGORO
 Mgogoro kati ya Gaddi na Nyambuja
 Mogoro kati ya Gaddi na Dania
 Mgogoro kati ya Gaddi na Jerry
 Mgogoro kati ya Nunu, Boaz na Bi Hanuna
 Mgogoro kati ya Dania na Jerry
 Mgogoro kati ya Jerry na wazazi wa Dania
 Mgogoro kati ya Nunu na Jerry
 Mgogoro wa nafsi
                      
                FANI
    Muundo
Msanii ametumia miundo mitatu ambayo ni muundo changamano,muundo rejea na Muundo wa moja kwa moja. Sura ya kwanza ametumia muundo Rejea  na kuanzia sura ya pili na kuendelea ametumia muundo wa moja kwa moja mpaka mwisho wa riwaya.
    MTINDO
Ø  Msanii ametumia kwa kiasi kikubwa mtindo wa masimulizi na kiasi kidogo mtindo wa dayalojia, nafsi zote tatu zimetumika. Vilevile kuna matumizi ya barua. (UK 65)
MATUMIZI YA LUGHA
Ø  Ametumia lugha rahisi yenye misemo, methali, tamathali za semi na mbinu nyingiezo za kisanaa.
Misemo/ Nahau
Jibu lile lilimkata maini (UK 36)
Methali
Ø  Ukistaajabu ya Musa utayaona ya firauni (UK 27)
Ø  Hakuna marefu yasiyo na ncha (UK 17)
Ø  Ni bora nusu shari kuliko shari kamili (UK 127)
Ø  Mkaidi hafaidi mpaka siku ya Iddi ( UK 135)
TAMATHALI ZA SEMI
Tashbiha
Ø  Paa lake lililokuwa limeengwa kwa mithili yam domo kwa lile dege aina ya concord. (UK 11)
Ø  Gari iliruka mbele kama jiwe na kutimua vumbi. (UK 41)
Ø  Kamfukuza  kama mbwa kutoka kwenye nyumba ya marehemu mumewe.
Onomatopea
Ø  Vilitilia mkazo uharaka kwa binti yule kwa kutoa sauti za ko! Ko! Ko! (UK 1)
Ø  Aaaaah! Ni  -niche! Uuuuuuuuwiiii! Yallaaaaah! (UK 37)
Takriri
Ø  Toka hapa! Ondoka! Na usirudi tena! (UK 32)
Ø  Nimesema sitaki! Sitaki! Sitaki! (UK 35)
Ø  Sikubali! Sikubali!nawaambia nitawashitaki kwa hili! (UK 43)
Mdokezo
Ø  Oh, Mungu wangu, sasa itakuwaje jamani………(UK 12)
Ø  Ah! Ni kweli anti……lakin………..(UK 12)

                           WAHUSIKA
  1. Gaddi Bullah
·         Mhusika mkuu, alikuwa meneja wa kampuni
·         Mchangamfu na mwenye huruma
·         Mkarimu na mchapakazi mzuri
·         Alikuwa na upendo wa dhati
·         Mume wa kwanza wa Nyambuja na mpenzi wa Dania
·         Alikuwa msamehefu na alizitawala vyema hisia zake
·         Anafaa kuigwa na jamii
  2. Dania
·         Mwanamke aliyezaliwa katika familia ya kitajiri
·         Mtu mwenye hasira anapokuwa amechukizwa na mwenye chuki
·         Mtu asiye na msimamo na anadanganyika kirahisi
·         Mfanyakazi mwenye nidhamu , bidii na ushirikiano
·         Alikuwa mlevi wa kutupwa baada ya kuachwa na Jerry
·         Anafaa kuigwa kwa baadhi ya mambo na hafai kuigwa kwa baadhi ya mambo
  3. Bi Hanuna
·         Dada yake Gaddi Bullah,
·         Alimpenda mdogo wake kiasi cha kukataa kumsaliti
·         Alikua na chuki na mtu yeyote aliyemuudhi mdogo wake Gaddi, Dana na Nunu
·         Bi Hanuna anafaa kuigwa na jamii kutokana na mapenzi aliyokuwa nayo kwa mdogo wake Gaddi Bullah
  4.  Jerry
·         Alikuwa mpenzi wake Dania na mtaalamu wa kompyuta
·         Mcheshi, mtanashati na mwenye mvuto mkubwa kwa kina dada
·         Katili na msaliti mkubwa
·         Hakua na mapenzi ya kweli
·         Hafai kuigwa na jamii
     5.Nunu
·         Rafiki yake Dania
·         Alikua na mapenzi ya kweli kwa watu, aliwasaidia sana wakati wa shida.
·         Anafaa kuigwa na jamii

Ø  Wahusika wengine ni Boazi, mama Mlole, Marry, Aisha, Agness, Junior na wengineo kama daktari Virani.

MANDHARI
v  Mandhari ya riwaya hii ni ya Arusha, Dar-es-salaam na Pemba katika sehemu hizo zote kuna mandhari ya ofisini, nyumbani, baa, barabarani, hospitalini.

JINA LA KITABU
Mfadhili ni mtu anayemdhamini mtu katika kugharamia kitu fulani. Katika riwaya hiimwandishi ameonesha ufadhili wa aina mbalimbali kama ifuatavyo;
Mosi,Mama Mlole anamfadhili Gaddi Bullah baada ya kukumbwa na kashfa ofisini kwake asifukuzwe kazi. Mama Mlole ndiye aliyemtetea Gaddi Bullah  hata kumhamishia Dar es salaam kwa uangalizi zaidi.
Pili, Mama Mlole alimfadhili Dania asifukuzwe kazi kutokana na kuwa mlevi sugu baada ya kuachwa na mpenzi wake Jerry.
Tatu,Mama Mlole alimfadhili Gaddi na Dania kwa kuwapatanisha kutokana na uhasama wao pale ofisini kwao. Bila yeye ugomvi ungeendelea.
Nne,Gaddi Bullah  alimfadhili Dania baada y kuachwa na Jerry. Dania mpenzi wake wa kwanza baada ya kuachwa na Jerry alichukuliwa na Gaddi ambaye alimpenda sana hali iliyopelekea Dania asimkumbuke Jerry. Gaddi Bullah alimfadhili Dania kwa kumpa ini lake moja wakati anaumwa baada ya kusalitiwa mara ya pili na Jerry, bila Gaddi, Dania angekufa. Vile vile Gaddi alimfadhili Junior kwa kumpeleka hospitalini baada ya kuumia mkono. Asingekua Gaddi,Junior angepata matatizo makubwa.
KUFAULU NA KUTOKUFAULU KWA MSANII
KUFAULU
v  Kimaudhui msanii amefaulu kuonesha matatizo mbalimbali yanayoikumba  jamii yetu hasa katika suala la mapenzi na ndoa na kuonesha suluhisho la matatizo hayo.
v  Kifani amefaulu kutumia lugha rahisi na inayoeleweka na ujengaji mzuri wa wahusika wake.
KUTOKUFAULU
v  Kutumia viswahili badala ya Kiswahili sanifu (UK 15-16)
v  Matumizi ya kiingereza kwa mtu ambaye hajui kiingereza atashindwa kupata ujumbe. 

Powered by Blogger.