KUCHUNGUZA DHAMIRA ZA KIJAMII

KUCHUNGUZA DHAMIRA ZA KIJAMII NA KIUTAMADUNI KATIKA
RIWAYA YA KISWAHILI: MIFANO KUTOKA KULI NA VUTA N’KUVUTE
OMAR ABDALLA ADAM
TASINIFU ILIYOWASILISHWA KWA AJILI YA KUTIMIZA SHARTI
PEKEE LA KUTUNUKIWA DIGRII YA UZAMIVU (PH.D KISWAHILI) YA
CHUO KIKUU HURIA CHA TANZANIA
2014
UTHIBITISHI
Mimi Profesa T.S.Y.M. Sengo, ninathibitisha kuwa nimesoma tasinifu hii iitwayo
Kuchunguza Dhamira za Kijamii na Kiutamaduni katika Riwaya ya Kiswahili:
Mifano Kutoka Kuli na Vuta N’kuvute, na ninapendekeza ikubaliwe na Chuo Kikuu
Huria Cha Tanzania kwa ajili ya kutimiza sharti pekee la kutunukiwa Digrii ya
Uzamivu (PhD) ya Kiswahili ya Chuo Kikuu Huria Cha Tanzania.
………………………………………………………………….
Sheikh, Profesa, Daktari, T.S.Y.M. SENGO
(Msimamizi)
…………………………………………..
Tarehe
ii
HAKIMILIKI
Hairuhusiwi kuiga au kunakili kwa namna yoyote sehemu yoyote ile ya tasinifu hii
kwa njia yoyote kama vile, kielektroniki, kurudufu nakala, kurekodi au njia yoyote
nyingine bila ya idhini ya mwandishi au Chuo Kikuu Huria cha Tanzania kwa niaba.
iii
TAMKO
Mimi, Omar Abdalla Adam, nathibitisha kuwa tasinifu hii ni kazi yangu halisi na
haijawahi kuwasilishwa katika Chuo Kikuu kingine chochote kwa ajili ya
kutunukiwa shahada kama hii au nyingine yoyote.
……………………………………………..
Saini
……………………………………………..
Tarehe
iv
TABARUKU
Ninapenda Kuitabaruku kazi hii kwa Wazazi wangu, Mke wangu na Mtoto wetu.
v
SHUKURANI
Kazi hii ya utafiti ni matokeo ya mchango na ushirikiano mkubwa baina yangu na
watu wengine, wakiwemo walimu wangu. Kwa kuwa sio rahisi kuandika kwa kina
mchango wa kila aliyenisaidia kuikamilisha kazi hii, wafuatao wanastahiki shukrani
za kipekee. Kwanza napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia uhai,
uzima, nguvu na fahamu katika kipindi chote cha masomo yangu.
Pili, napenda kutoa shukurani zangu za dhati kwa msimamizi wangu wa tasinifu hii,
Sheikh, Profesa, Daktari, T.S.Y.M Sengo kwa kuniongoza vyema katika kila hatua
ya utafiti huu. Hakusita wala kuchoka kunishauri na kuirekebisha kazi hii katika
hatua zote mpaka ilipokamilika. Msaada wake hauwezi kukisiwa wala kulipwa.
Ninachoweza kusema ni kutoa asante sana Profesa Sengo, Mwenyezi Mungu
Akubariki na Akujalie afya njema na maisha marefu. Aaamini, Aaamini, Aaamini.
Tatu, napenda kutoa shukurani zangu za dhati kwa walimu wengine wa Chuo Kikuu
Huria Cha Tanzania kwa msaada mkubwa walionipatia katika kipindi chote cha
masomo yangu. Walimu hao ni Profesa, Emmanuel Mbogo, Profesa H. Rwegoshora,
Dkt. Peter Lipembe. Dkt. Anna Kishe, Dkt. Hanna Simpasa, Dkt. Zelda Elisifa na
Mohamed Omary.
vi
IKISIRI
Riwaya za Kuli na Vuta N’kuvute zimepata umaarufu na kuwa riwaya nzuri na imara
za mtunzi Shafi Adam Shafi. Utafiti huu ulifanywa kwa nia kuu ya kuchunguza
dhamira za kijamii na kiutamaduni zinazojitokeza katika riwaya hizo mbili (Kuli na
Vuta N’kuvute). Katika kutimiza nia hii, tulikusanya data kwa kutumia mbinu za
maktabani, mahojiano ya ana kwa ana kufanya na uchambuzi wa kimaudhui. Data
zilizokusanywa zilichambuliwa kwa kutumia mbinu za mkabala wa kimaelezo na ule
wa kidhamira. Nadharia za Simiotiki, Saikolojia Changanuzi na dhima na kazi, ndizo
zilizotumika katika kuhakiki riwaya hizo mbili. Matokeo ya utafiti yanaonesha
kwamba, dhamira zinazojitokeza zaidi katika riwaya hizo mbili ni matabaka katika
jamii, ndoa za kulazimishwa, mapenzi na ukarimu katika riwaya ya Vuta N’kuvute.
Katika Kuli, dhamira zinazojitokeza zaidi ni busara na hekima, umuhimu wa elimu,
umasikini, utamaduni na mabadiliko yake, ukombozi katika jamii na masuala ya
uzazi. Dhamira hizo zimesheheni uhalisia katika maisha ya sasa ya jamii ya leo. Pia
matokeo ya utafiti yanaonesha kwamba, mbinu za kisanaa zinazotumiwa na mtunzi
katika uwasilishaji wake wa dhamira ni upambaji wa wahusika, usimulizi,
kuingiliana kwa tanzu, tashibiha, misemo, takriri, taswira, motifu na matumizi ya
barua.
vii
YALIYOMO
UTHIBITISHI ......................................................................................................... i
HAKIMILIKI ........................................................................................................ ii
TAMKO ................................................................................................................. iii
TABARUKU .......................................................................................................... iv
SHUKURANI ......................................................................................................... v
IKISIRI ................................................................................................................. vi
VIAMBATANISHO ............................................................................................. xii
SURA YA KWANZA ............................................................................................. 1
1.0 UTANGULIZI ............................................................................................... 1
1.1 Utangulizi ....................................................................................................... 1
1.2 Usuli wa Tatizo la Utafiti ................................................................................ 1
1.3 Tatizo la Utafiti ............................................................................................... 6
1.4 Lengo la Jumla................................................................................................ 7
1.4.1 Malengo Mahususi .......................................................................................... 7
1.4.2 Maswali ya Utafiti .......................................................................................... 8
1.5 Umuhimu wa Utafiti ....................................................................................... 8
1.6 Mipaka ya Utafiti ............................................................................................ 9
1.7 Changamoto za Utafiti .................................................................................... 9
1.7.1 Utatuzi wa Changamoto .................................................................................10
1.8 Mpangilo wa Tasinifu ....................................................................................10
1.9 Hitimisho .......................................................................................................11
SURA YA PILI .....................................................................................................12
2.0 MAPITIO YA KAZI TANGULIZI NA MKABALA
viii
WA KINADHARIA .....................................................................................12
2.1 Utangulizi ......................................................................................................12
2.2 Maana ya Riwaya ..........................................................................................12
2.3 Historia na Chimbuko la Riwaya ya Kiswahili ...............................................17
2.4 Dhamira katika Riwaya ya au kwa Kiswahili .................................................19
2.5 Muhtasari .......................................................................................................35
2.6 Fani katika Riwaya ya Kiswahili ....................................................................36
2.6.1 Utangulizi ......................................................................................................36
2.6.2 Vipengele vya Kifani .....................................................................................36
2.7 Muhtasari .......................................................................................................48
2.8 Kazi Tangulizi Juu ya Riwaya za Shafi Adam Shafi .......................................48
2.9 Mkabala wa Kinadhari ...................................................................................55
2.9.1 Nadharia ya Simiotiki ....................................................................................55
2.9.2 Nadharia ya Dhima na Kazi ...........................................................................57
2.9.3 Nadharia ya Saikolojia Changanuzi ................................................................58
2.10 Muhtasari .......................................................................................................60
SURA YA TATU ...................................................................................................61
3.0 MBINU NA ZANA ZA UTAFITI .............................................................61
3.1 Utangulizi ....................................................................................................61
3.2 Mpango wa Utafiti .......................................................................................61
3.3 Eneo la Utafiti .............................................................................................62
3.4 Aina ya Data Zilizokusanywa ......................................................................62
3.4.1 Data za Msingi ............................................................................................62
3.4.2 Data za Upili ...............................................................................................63
ix
3.5 Watafitiwa ...................................................................................................63
3.6 Ukusanyaji wa Data .....................................................................................64
3.6.1 Uchambuzi wa Nyaraka ...............................................................................64
3.6.2 Mahojiano ya Ana kwa Ana.........................................................................65
3.6.3 Usomaji na Uhakiki wa Riwaya Teule .........................................................66
3.7 Uchambuzi wa Data.....................................................................................66
3.7.1 Mkabala wa Kidhamira ................................................................................67
3.8 Usahihi, Kuaminika na Maadili ya Utafiti ....................................................68
3.8.1 Usahihi wa Data ..........................................................................................68
3.8.2 Kuaminika kwa Data ...................................................................................68
3.9 Maadili ya Utafiti ........................................................................................68
3.10 Hitimisho.....................................................................................................69
SURA YA NNE .....................................................................................................70
4.0 UWASILISHAJI, UCHAMBUZI WA DATA NA MJADALA WA
MATOKEO YA UTAFITI ........................................................................70
4.1 Utangulizi .....................................................................................................70
4.2 Muhtasari wa Riwaya ya Vuta N’kuvute .......................................................71
4.3 Uchambuzi wa Dhamira katika Riwaya ya Vuta N’kuvute.............................71
4.3.1 Matabaka Katika Jamii ................................................................................72
4.3.2 Ndoa ya Kulazimishwa ................................................................................81
4.2.3 Mapenzi ......................................................................................................91
4.3.3.1 Mapenzi ya Bwana Raza kwa Yasmini ........................................................96
4.3.3.2 Mapenzi ya Yasmini kwa Waswahili ......................................................... 102
4.3.3.3 Upendo wa Yasmini kwa Mama Yake ....................................................... 104
x
4.3.4 Ukarimu .................................................................................................... 107
4.2.5 Muhtasari .................................................................................................. 111
4.4 Uchambuzi wa Dhamira katika Kuli .......................................................... 111
4.4.1 Utangulizi .................................................................................................. 111
4.4.2 Muhtasari wa Riwaya ya Kuli .................................................................... 112
4.3.2.1 Busara na Hekima ..................................................................................... 112
4.3.2.2 Umuhimu wa Elimu Katika Jamii .............................................................. 116
4.3.2.3 Umasikini Katika Jamii ............................................................................ 122
4.3.2.4 Utamaduni na Mabadiliko Yake Katika Jamii ........................................... 126
4.3.2.5 Ukombozi Katika Jamii ............................................................................ 133
4.3.2.6 Masuala ya Uzazi ...................................................................................... 136
4.3.2.7 Muhtasari ................................................................................................. 139
4.4 Mbinu za Kisanaa katika Riwaya Teule za Shafi Adam Shafi .................... 139
4.4.1 Upambaji wa Wahusika ............................................................................. 140
4.4.2 Usimulizi katika Riwaya za Shafi Adam Shafi ........................................... 144
4.4.2.1 Usimulizi Maizi ......................................................................................... 145
4.4.2.2 Usimulizi wa Nafsi ya Kwanza .................................................................. 147
4.4.2.3 Matumizi ya Nafsi ya Kwanza Wingi ........................................................ 148
4.4.3 Kuingiliana kwa Tanzu .............................................................................. 149
4.4.4 Matumizi ya Tashibiha .............................................................................. 153
4.4.5 Matumizi ya Misemo ................................................................................. 157
4.4.6 Matumizi ya Takriri ................................................................................... 162
4.4.7 Matumizi ya Taswira ................................................................................. 164
4.4.8 Matumizi ya Motifu ................................................................................... 170
xi
4.4.8.1 Motifu ya Safari ........................................................................................ 171
4.4.8.2 Motifu ya Uzuri ......................................................................................... 174
4.4.8.3 Motifu ya Uzee wa Bwana Raza ................................................................ 175
4.4.9 Matumizi ya Barua .................................................................................... 179
4.4.10 Hitimisho................................................................................................... 183
SURA YA TANO ................................................................................................ 184
5.0 MUHTASARI, HITIMISHI NA MAPENDEKEZO ................................ 184
5.1 Utangulizi .................................................................................................... 184
5.2 Muhtasari ..................................................................................................... 184
5.3 Hitimisho ..................................................................................................... 186
5.4 Mapendekezo ............................................................................................... 188
5.4.1 Mapendekezo ya Utafiti Ujao ....................................................................... 188
5.4.2 Mapendekezo kwa Wazazi na Wanafunzi ..................................................... 188
5.4.3 Mapendekezo kwa Wasomaji ....................................................................... 189
5.4.4 Mapendekezo kwa Serikali .......................................................................... 189
MAREJELEO ..................................................................................................... 190
VIAMBATANISHO............................................................................................ 200
xii
VIAMBATANISHO
Kiambatanisho 1: Muongozo wa Usaili kwa Wasomaji wa Riwaya Teule ............ 200
Kiambatanisho 2: Muongozo wa Usaili kwa Wataalamu wa Fasihi ...................... 201
1
SURA YA KWANZA
1.0 UTANGULIZI
1.1 Utangulizi
Utafiti kuhusu riwaya ya Kiswahili umefanywa na wataalamu kadhaa lakini bado
haujafanywa kwa kiwango cha kuridhisha (Mlacha na Madumulla, 1991). Utafiti huu
unafanywa kama sehemu mojawapo ya kuchangia mjazo wa pengo lililotajwa,
kukuza na kuimarisha utafiti katika riwaya ya Kiswahili kwa nia ya kuongeza
machapisho na marejeleo katika fasihi ya Kiswahili. Ili kutimiza lengo hili, sura hii
ya kwanza itawasilisha vipengele vya kiutangulizi ambavyo vinahusu usuli wa tatizo
la utafiti, tatizo la utafiti, lengo kuu na madhumuni mahsusi ya utafiti. Pia, maswali
ya utafiti, umuhimu wa utafiti, mipaka ya utafiti, vikwazo vya utafiti, utatuzi wa
vikwazo vya utafiti na mpangilio wa tasinifu. Vipengele vyote hivi ndivyo
vinavyokamilisha utangulizi wa utafiti mzima.
1.2 Usuli wa Tatizo la Utafiti
Utanzu wa riwaya ndiyo utanzu katika fasihi ya Kiswahili ambao unaeleza masuala
mbalimbali yanayohusu maisha ya mwanadamu kwa mawanda mapana
ikilinganishwa na tanzu nyingine za fasihi ya Kiswahili (Njogu na Chimerah, 1999).
Kupitia utanzu huu, mtunzi wa riwaya, anaweza kueleza visa na matukio mbalimbali
yanayomuhusu muhusika au wahusika fulani, tangu wanapozaliwa mpaka
wanapofariki (Wamitila, 2008).
Vilevile, maelezo na matukio hayo ambayo yanamuhusu muhusika au wahusika
fulani huelezwa kwa mchangamano na mwingiliano ambao si rahisi kuupata katika
2
utanzu mwingine wowote wa kazi ya fasihi ya Kiswahili. Pamoja na sifa hizo za
riwaya kueleza maisha ya wanadamu kwa mawanda mapana, utanzu huu si wa
kwanza kupata kuwapo katika ulimwengu wa fasihi si ya Kiswahili tu, bali fasihi
duniani kote. Utanzu wa mwanzo kabisa kupata kuwapo hapa duniani ni ushairi tena
ushairi simulizi. Utanzu wa mwanzo kabisa kupata kuwapo hapa ulimwenguni ni
ushairi wa nyimbo (Mulokozi na Sengo, 1995).
Hata hivyo, maelezo tuliyoyatoa hapo juu hayana maana kwamba utanzu wa riwaya
haukuwapo katika kipindi hicho cha ushairi simulizi. Utanzu huu ulikuwapo ndani ya
ushairi. Tunapotazama tenzi za zamani, kama vile,Utenzi wa Raslgh’ul, tunakutana
na masimulizi ya wahusika wanaotenda matendo na matukio. Hii inaonesha kwamba
utanzu wa riwaya ulikuwapo tangu hapo kale lakini ulikuwa umefungamanishwa
katika tungo za kishairi simulizi, hususani ya tenzi au tendi (Madumulla, 2009).
Jambo la msingi la kufahamu hapa ni kwamba, utanzu wa riwaya uliokuwapo ndani
ya ushairi ulikuwa bado haujafahamika kwa namna ya uainishaji ambao
tunaufahamu hivi leo. Uainishaji wa riwaya ambao tunao hivi leo ni ule ulioanza
mwishoni wa karne ya 18 na mwanzoni mwa karne ya 19 uliohusishwa na
kugundulika kwa maandishi ya Kirumi (Senkoro, 1977).
Riwaya hiyo- the novel- ni ya Kizungu, tafauti na hadithi ndefu ya Kiafrika ambayo
tangu azali, haikuwa imeainishwa kwa misingi ya maandishi. Baada ya kugunduliwa
kwa maandishi haya ndipo riwaya ilipoanza kuandikwa kwa muktadha wa
Kimagharibi lakini katika nchi za Kiarabu ambako maandishi yalikuwako tangu
3
karne za nyuma, utanzu wa riwaya ulikuwako kwa sura tafauti ambazo zinakaribisha
wasomi kuzifanyia utafiti. Katika ulimwengu wa riwaya ya Kiswahili, wenyewe
ulikuwapo tangu kale, pale tu mwanadamu alipoanza kuwasiliana na wenzake na
kushirikiana katika kufanya shughuli mbalimbali (Mulokozi, 1996).
Kauli hii inakingana na hizo za hapo juu. Hata hivyo, utanzu huu ulihusishwa sana
na hadithi ambazo bibi au babu alikuwa akiwasimulia wajukuu wake wakati wa jioni
walipokuwa wakiota moto (Msokile, 1992; 1993). Hadithi hizi zilikuwa ni simulizi
kwa wakati huo ambao hakukuwa na utaalamu wa kuandika. Kupitia hadithi
simulizi, watoto na watu wa marika yote,waliweza kupata elimu kuntu zilizohusu
maisha. Baada ya kuanza kutumika kwa maandishi, masimulizi yale yale yaliyokuwa
yakitolewa na babu au bibi, sasa yalianza kuandikwa katika vitabu na kuanza kuitwa
riwaya ya Kiswahili.
Walioziandikia, wakiziita ni zao. Mfano mzuri ni Adili na Nduguze. Senkoro (1977)
anaeleza kwamba riwaya ya kwanza kabisa kuandikwa ni Uhuru wa Watumwa
iliyoandikwa na Mbotela mwaka 1934. Kwa maoni yetu yaliyomo ndani ya kazi hiyo
ni masimulizi yaliyowahusu watumwa ambayo yalifanywa na watumwa kupitia njia
ya mazungumzo na masimulizi. Kilichofanywa na Mbotela ni kuyachukua
masimulizi hayo na kuyaweka katika maandishi.
Kwa hivi ingelikuwa vema maelezo ya Senkoro yangeeleza kwamba Mbotela
alikuwa ni mmoja kati ya watu wa mwanzo kuyaweka masimulizi ya hadithi katika
maandishi. Haya yangalikuwa na mashiko zaidi kitaaluma kuliko kusema kwamba
Mbotela ndiye mtu aliyeanzisha riwaya ya Kiswahili kwa kuandika kitabu mwaka wa
4
1934. Kimsingi, baada ya kuingizwa kwa maandishi, watunzi kadhaa walijitokeza na
kuandika riwaya ya Kiswahili, na kwa Kiswahili. Miongoni mwao ni Shaaban Robert
aliyeibukia kuwa mwandishi bora wa kazi za fasihi ya Kiswahili kupitia kazi zake za
Maisha Yangu na Baada ya Miaka Hamsini, Kusadikika, Kufikirika, Adili na
Nduguze, Utu Bora Mkulima, Siku ya Watenzi Wote na Siti Binti Saad. Kazi hizo
zimemfanya Shaaban Robert kuwa mwandishi bora wa fasihi ya Kiswahili
anayefahamika na kuheshimika katika Ukanda wa Afrika ya Mashariki na
Kwingineko barani Afrika (Chuwachuwa, 2011).
Katika sehemu hii tumetaja kazi zake za riwaya tu kwa sababu ndizo
tunazozishughulikia lakini ameandika pia kazi nyingi za ushairi na insha. Utunzi wa
Shaaban Robert ndiyo kwa hakika unaofahamika kuwa ulifungua mlango kwa
watunzi wengine wa riwaya ya Kiswahili. Miongoni mwa watunzi wa riwaya ya
Kiswahili waliovutiwa na Shaaban Robert na kuanza kutunga riwaya ni Kezilahabi
kama anavyoeleza katika tasinifu yake ya Uzamili ya mwaka wa 1976. Pia, Sengo
(2014) amemuainisha Shaaban Robert kuwa mwandishi bora wa riwaya kwa
Kiswahili na si ya Kiswahili kwa kuwa Uswahilini si kwao na hakutaka kukifanyia
utafiti wa kukipata Kiswahili cha sawasawa na kuandikia angalau kazi moja ya
riwaya ya Kiswahili.
Mlacha na Madumulla (1991) wanaeleza kuwa utunzi wa Shaaban Robert, kwa
hakika, ndiyo ulioleta athari ya kuandika riwaya ya Kiswahili. Utunzi wake wa
riwaya ulifuata kanuni za kijadi za utunzi wa riwaya ya Kiswahili. Yapo mambo
mengi ambayo yanathibitisha kwamba utunzi wa riwaya za Shaaban Robert ulikuwa
ni kijadi lakini kwa muktadha huu tutazungumzia jambo moja tu. Tunapotazama
5
matumizi ya wahusika katika riwaya za Shaaban Robert tunakuta kwamba anatumia
wahusika wa kijadi. Mlacha na Madumulla (wameshatajwa) wanamuainisha mhusika
wa aina hii kuwa ni mhusika mkwezwa na mhusika dunishwa. Mhusika mkwezwa ni
yule ambaye anapewa sifa za utu wema tangu mwanzo wa riwaya mpaka mwisho.
Mhusika dunishwa ni yule ambaye anapewa sifa za uovu tu tangu mwanzo mpaka
mwisho wa riwaya. Kezilahabi (1976) anasema kwamba, katika ulimwengu wa
kawaida hatuwezi kumpata mtu wa namna hiyo mahali popote kwani wanadamu ni
watu wenye sifa za wema na uovu. Na hili ndilo humfanya mtu akaitwa
mwanadamu, vinginevyo, angeitwa Malaika ambao wao hawana maovu kabisa. Hata
hivyo, matumizi ya wahusika wa aina hii yalifanywa kwa makusudi na Shaaban
Robert kwa nia ya kuihamasisha jamii kufanya mambo mema na kuepuka maovu
(Kalegeya, 2013). Kauli hii ya mwisho inaendana na Nadharia ya Kiislamu ya Fasihi
(Sengo, 2009) inayomtaka muumini ahimize na atende mema na asifanye kinyume
kwa kupendeza watu ili aonekane kuwa naye ni msomi.
Shafi Adam Shafi ni miongoni mwa watunzi wa riwaya ya Kiswahili aliyekuja na
kuandika riwaya kadhaa baada ya Shaaban Robert. Miongoni mwa riwaya
alizoziandika ni Kasri ya Mwinyi Fuad, Kuli, Haini, Vuta N’kuvute na Mbali na
Nyumbani (Walibora, 2013). Wamitila (2002) anamtaja Shafi Adam Shafi kuwa ni
miongoni mwa watunzi bora aliyeshinda tuzo kadhaa za uandishi bora wa riwaya ya
Kiswahili. Tafauti na utunzi wa Shaaban Robert, Shafi Adam Shafi anatumia aina ya
mhusika anayefahamika kama mhusika jumui (Mlacha na Madumula, 1991).
Wahusika wa Shafi Adam Shafi ni wale ambao wanajipambanua kwa kutumia sifa za
wema na uovu kwa wakati huo huo (Kyando, 2013). Mfano mzuri ni mhusika
6
Yasmini katika Vuta N’kuvute ambaye anasawiriwa kwa kufunya matendo mema
yenye kukubalika katika jamii na wakati mwingine kufanya mambo ambayo
hayakubaliki katika jamii. Huu ndiyo ubinadamu na kwamba kila mwanadamu
huangukia katika kundi kama hili (Wamitila, 2002).
Mulokozi (2013) anamtaja Shafi Adam Shafi kuwa ni mtunzi bora wa riwaya za
Kihistoria hususani kupitia riwaya yake ya Kuli. Pamoja na ukweli kwamba, Shafi
Adam Shafi, anatunga riwaya za kihistoria, riwaya zake zinaweza kuingia katika
mkondo wa riwaya za Kisaikolojia zinazofanana kwa karibu na Nyota ya Rehema na
Kiu, za Suleiman (1978; 1985). Hii inaonekana pale wahusika wake wakuu,
wanapokumbana na matatizo ambayo huwaletea athari za Kisaikolojia/Kiushunuzi
(Wamitila, 2008). Baada ya kulifahamu hili, tukaona ipo haja ya msingi ya kufanya
utafiti wa kina katika kuchunguza dhamira za kijamii na za kiutamaduni kama
zinavyojitokeza katika riwaya mbili za Kuli na Vuta N’kuvute.
1.3 Tatizo la Utafiti
Riwaya ya Kiswahili imekuwa ikifanya kazi ya kusawiri maisha halisi ya jamii ya
Waswahili na hata kuvuka mipaka na kuzifikia jamii nyingine duniani kwa kipindi
kirefu sasa (Madumulla, 2009). Kutokana na kuisawiri jamii vilivyo, riwaya ya
Kiswahili imekuwa ni chombo imara katika kujenga maadili kwa jamii, hususani
katika shule ambako riwaya hizo husomwa zikiwa vitabu vya kiada au ziada.
Kutokana na mchango wa riwaya ya Kiswahili katika kukuza na kujenga maadili,
watafiti kama vile Mlacha na Madumulla (1991) wamevutiwa kufanya utafiti katika
riwaya ya Kiswahili. Na leo mtafiti wa riwaya hii amejitia timuni kutimiza wajibu
wa kuichunguza riwaya ya Kiswahili.
7
Miongoni mwa riwaya zinazotoa mchango wa kukuza na kujenga maadili ya jamii ni
zile za Shafi Adam Shafi. Watafiti waliovutiwa kuzifanyia uhakiki na kuzisemea ni
Mbise (1996), Njogu na Chimerah (1999), Wamitila (2002; 2008), Walibora (2013)
na Mulokozi (2013). Katika watafiti wote hao, hakuna hata mmoja ambaye
amechunguza kwa mawanda mapana kipengele chochote cha kifasihi katika riwaya
za Kuli na Vuta N’kuvute. Wamekuwa wakitaja tu baadhi ya vipengele vya riwaya za
Shafi Adam Shafi, kama sehemu ya kukamilisha madhumuni ya kazi zao ambazo
mawanda yake hayakujumuisha kuchunguza dhamira za kijamii na kiutamaduni.
Utafiti huu utafanywa ili kuziba pengo hilo la kiutafiti kwa kuchunguza dhamira za
kijamii na za kiutamaduni ambazo zinajitokeza katika riwaya za Kuli na Vuta
N’kuvute.
1.4 Lengo la Jumla
Lengo la jumla utafiti huu ni kuchunguza usawiri wa dhamira za kijamii na
kiutamaduni katika riwaya za Kuli na Vuta N’kuvute.
1.4.1 Malengo Mahususi
1.4.1.1 Kubainisha dhamira za kijamii na kiutamaduni zinazojitokeza katika riwaya
za Kuli na Vuta N’kuvute.
1.4.1.2 Kutathimini uhalisia wa dhamira za kijamii na kiutamaduni zinazojitokeza
katika riwaya za Kuli na Vuta N’kuvute kwa jamii ya leo.
1.4.1.3 Kubainisha mbinu za kisanaa zinazotumiwa na mtunzi katika kusawiri
dhamira za kijamii na kiutamaduni katika riwaya za Kuli na Vuta N’kuvute.
8
1.4.2 Maswali ya Utafiti
Utafiti huu ulikuwa na jumla ya mswali matatu ambayo yanaendana na malengo
mahususi kukamilisha nia kuu ya utafiti huu. Maswali hayo ni haya yafuatayo:
1.4.2.1 Ni dhamira zipi za kijamii na kiutamaduni zinazojitokeza katika riwaya za
Kuli na Vuta N’kuvute?
1.4.2.2 Dhamira za kijamii na kiutamaduni zinazojitokeza katika riwaya za Kuli na
Vuta N’kuvute zina uhalisiya gani kwa jamii ya leo?
1.4.2.3 Ni mbinu zipi za kisanaa zinazotumiwa na mtunzi katika kusawiri dhamira za
kijamii na kiutamaduni katika riwaya za Kuli na Vuta N’kuvute?
1.5 Umuhimu wa Utafiti
Kitaalimu: Matokeo ya utafiti huu yatakuwa marejeleo kwa wasomi wa ngazi zote za
taalimu ya fasihi. Wanafunzi hao watakaoyatumia matokeo ya utafiti huu kuwa
sehemu ya madondoo yao ya kukamilisha madhumuni ya utafiti wao watakaokuwa
wanaufanya. Aidha, matokeo ya utafiti huu watayatumiya kama sehemu ya kujinoa,
ili kubainisha pengo la maarifa ambalo wao watalijaza katika utafiti wao.
Wanataalimu ambao ni walimu, wahadhiri na maprofesa katika taalimu ya fasihi
watauona umuhimu wa utafiti huu katika kuandika vitabu, makala na maandalio ya
masomo ya kufundishia wanafunzi wao wa ngazi mbalimbali za elimu. Kwa wale
ambao ni walimu wa shule za Sekondari, watautumia utafiti huu kuwafundishia
wanafunzi wao, mada ya uchambuzi na uhakiki katika fasihi ya Kiswahili
madarasani.
9
Kinadharia: utafifiti huu umetoa uthibitishi kwamba, nadharia za uhakiki wa fasihi
zinapotumika kuhakiki kazi za fasihi huifanya kazi hiyo kuwa imara na yenye
mashiko ambayo huaminika kitaalimu. Kupitia utafiti huu watafiti wa baadaye
wataona umuhimu wa kutumia nadharia katika kuhakiki kazi za fasihi.
Kisera: Utafiti huu unaeleza matatizo mengi ya kijamii ambayo yanaikumba jamii
kwa sasa kama vile, masuala ya elimu, matabaka na umasikini. Kwa watunga sera,
utafiti huu utawafaa katika kuainisha mambo mbalimbali ambayo yanastahili
kuingizwa katika sera na kufanyiwa utekelezaji ili kuimarisha mipango ya
utekelezaji kwa manufaa ya jamii kubwa.
1.6 Mipaka ya Utafiti
Utafiti huu unachambua dhamira za kijamii na za kiutamaduni ambazo zinajitokeza
katika riwaya za Kuli na Vuta N’kuvute tu. Uchambuzi unaofanywa katika utafiti huu
ni wa kifasihi ambao unaongozwa na nadharia teule za uhakiki wa kifasihi. Kwa
upande wa mipaka ya kimaeneo, utafiti huu umefanyika katika jiji la Dar es Salaa,
Unguja na Pemba. Uteuzi wa maeneo haya umefanywa kwa sababu ndiko
kulikopatikana data zilizohitajika katika kuikamilisha kazi hii.
1.7 Changamoto za Utafiti
Changamoto mojawapo ya utafiti huu ilikuwa ni baadhi ya watafitiwa kutokuwa
tayari kufanya mahojiano na mtafiti. Watafitiwa hao ni wale wa kundi la wasomaji
wa riwaya za Shafi Adam Shafi. Sababu kuu ya kukataa kuhojiwa ilikuwa ni madai
kwamba, watafiti kadhaa wamekuwa wakifanya tafiti kwa masilahi binafsi ya kupata
10
fedha huku watafitiwa ambao ndio waliotoa data hawapati faida yoyote. Kwa hiyo,
walihitaji kupatiwa fedha ndiyo washiriki katika mahojiano na mtafiti.
1.7.1 Utatuzi wa Changamoto
Utatuzi wa changamoto za utafiti ni jambo muhimu sana ambalo husaidia kukamilika
kwa utafiti. Katika kuhakikisha kwamba, utafiti unakamilika kwa wakati, mtafiti
alijitahidi kutoa elimu ya umuhimu wa utafiti anaoufanya kwa watafitiwa wake.
Aliwaeleza kuwa, utafiti anaoufanya ni wa kitaaluma ambao utamwezesha
kutunukiwa Shahada ya Uzamivu na hakuna faida yoyote ya kifedha anayoipata
kutokana na kufanya utafiti huu. Pia, aliwaeleza kuwa, katika utafiti wowote wa
kitaaluma ni kinyume na maadili ya utafiti kumlipa mtafitiwa kwa sababu tu
amefanyiwa usaili au mahojiano na mtafiti. Kwa kufanya hivyo, utafiti huo utakuwa
ni biashara na kuruhusu kupatikana kwa data za uongo zisizokuwa na uwezo wa
kukidhi malengo ya utafiti. Hivyo, baada ya kutolewa kwa elimu hii, baadhi ya
watafitiwa walikubali kufanya mahojiano na mtafiti na baadhi walikataa. Msimamo
wa wale waliokataa uliheshimiwa na hawakulazimishwa kufanya kile wasichokitaka.
1.8 Mpangilo wa Tasinifu
Tasinifu hii inajumla ya sura kuu tano zenye mada kuu na mada ndogondogo ndani
yake. Sura ya kwanza inaelezea vipengele mbalimbali vya kiutangulizi. Vipengele
hivyo ni usuli wa tatizo la utafiti, tatizo la utafiti, lengo la jumla la utafiti, malengo
mahususi ya utafiti na maswali ya utafiti. Vipengele vingine ni umuhimu wa utafiti,
mipaka ya utafiti, changamoto za utafiti, utatuzi wa changamoto za utafiti na
mpangilio wa tasinifu. Sura ya pili inaelezea mapitio ya kazi tangulizi huku sura ya
tatu ikiwasilisha mbinu za utafiti. Sura ya nne imehudhurisha uchambuzi wa data za
11
utafiti na sura ya tano ikitoa muhtasari, hitimisho na mapendekezo ya utafiti wa
baadaye.
1.9 Hitimisho
Katika sura hii tumeeleza vipengele mbalimbali ambavyo vinaonesha haja ya
kufanyika kwa utafiti huu. Ni katika sura hii ndipo pengo la kiutafiti lilipobainishwa
na kisha kujengwa hoja kuu ya kufanyika kwa utafiti huu. Kimsingi, hakuna utafiti
wa kina ambao umefanyika katika ngazi ya uzamili na uzamivu wa kuchunguza
dhamira mbalimbali zinazojengwa na Shafi Adam Shafi katika riwaya zake zote na
hususani Kuli na Vuta N’kuvute. Hivyo basi tukaona kwamba kunahaja ya msingi ya
kufanya utafiti katika ngazi ya uzamivu ili kuziba pengo hili la kiutafiti kwa
kuchunguza dhamira ambazo zinajitokeza katika riwaya za Kuli za Vuta N’kuvute.
12
SURA YA PILI
2.0 MAPITIO YA KAZI TANGULIZI NA MKABALA WA KINADHARIA
2.1 Utangulizi
Katika sura hii kumefanywa mapitio ya kazi tangulizi kwa nia ya kupata maarifa ya
watafiti waliotangulia. Katika kuhakikisha hili, tumeanza kwa kutazama
wanataalimu watangulizi wanaeleza nini kuhusiana na maana ya riwaya. Kisha
tukaendelea na uhakiki na uchambuzi wa riwaya kwa jumla kabla ya kumalizia na
kipengele cha uhakiki na uchambuzi wa riwaya na mtunzi ambaye, tunashughulikia
riwaya zake. Mapitio ya kazi tangulizi ymetujuza maarifa mengi kuhusu mada ya
utafiti na kutuwezesha kubaini pengo la utafiti. Pia katika sura hii tumewasilisha
nadharia kadhaa zilizotumika katika kuongoza uchambuzi wa data za utafiti huu.
2.2 Maana ya Riwaya
Maana ya riwaya imetolewa na wataalamu mbalimbali wakifanana katika baadhi ya
vipengele na kutofautiana katika mambo yanayounda riwaya ya Kiswahili. Miongoni
mwa wataalamu walioandika kuhusu dhanna ya riwaya ni Nkwera (1978) pale
aliposema: riwaya ni hadithi iliyo ndefu kuweza kutosha kufanya kitabu kimoja au
zaidi. Ni hadithi ya kubuniwa iliyojengwa juu ya tukio la kihistoria na kuandikwa
kwa mtindo wa lugha ya mfululizo na ya kinaganaga katika kuelezea maisha ya mtu
au watu na hata taifa.Riwaya huwa ina mhusika mmoja au hata wawili.
Maana ya riwaya inayotolewa na Nkwera (1978) inatufahamisha kwamba riwaya ni
hadithi ndefu, jambo ambalo tunakubaliana nalo kwa asilimia mia moja. Riwaya ni
hadithi ndefu ambapo kutokana na urefu huo huifanya kuwa tafauti na hadithi fupi,
13
ushairi na tamthilia. Urefu wa riwaya huifanya kueleza mambo kwa kina na marefu
kiasi cha kumfanya msomaji kuelewa kisa, tukio au matukio mbalimbali
yanayoelezwa katika riwaya husika. Kiasili, neno riwaya lina maana ya taarifa
iliyokamilika hasa katika masuala ya dini ya Kiislamu (Sengo, 2014).
Jambo jinguine ambalo tumejifunza juu ya maana ya riwaya hapo juu ni kuwapo kwa
lugha au mtindo wa kishairi. Hapa tunafahamishwa kwamba, riwaya huweza
kuandikwa kwa kutumia mitindo mingi na sio lazima ule wa nathari ambao ndiyo
uliyozoeleka na watunzi wengi wa riwaya ya Kiswahili. Katika utafiti wetu
tumeilewa dhana hii kwa kuzingatia tenzi ndefu za zamani ambazo zilikidhi sifa za
riwaya. Katika utafiti huu, kumechunguzwa namna Shafi Adam Shafi anavyotunga
riwaya zake na kama anaitumia mbinu hii ya mtindo wa kishairi katika riwaya zake
na sababu za kutumia mtindo huu.
Jambo ambalo hatukubaliani sana na Nkwera (ameshatajwa) ni kuhusu wahusika wa
riwaya. Yeye anataja mhusika mmoja au hata wawili kuwa wanaweza kuunda
riwaya. Kwa hakika riwaya ni utungo ambao hueleza mambo mengi kama
alivyoeleza yeye Nkwera mwenyewe. Kama hivyo ndivyo, ni wazi kwamba, riwaya
yenye mhusika mmoja haiwezi kueleza mambo kama itakavyokuwa kwa riwaya
yenye wahusika wengi. Mlacha na Madumulla (1991) wanasema kwamba, riwaya
huwa inawahusika wengi ambapo kunakuwa na mhusika mkuu na wahusika wadogo
au wasaidizi ambao kazi yao kuu ni kumpamba mhusika mkuu aweze kukamilisha
lengo la mtunzi. Maelezo ya Mlacha na Madumulla (wameshatajwa), yanaonekena
kuwa na mashiko ya kitaaluma zaidi kuhusu idadi ya wahusika katika riwaya ya au
kwa Kiswahili.
14
Wataalamu wengine ambaowameandika kuhusu maana ya riwaya, ni Muhando na
Balisidya (1976). Wao walisema kwamba riwaya ni kazi ya kubuni, ni hadithi
ambayo hutungwa kufuatana na uwezo wa fanani kuibua mambo kutokana na
mazoea au mazingira yake.Riwaya yaweza kuanzia maneno 35000 hivi na
kuendelea, lakini tukisema juu ya urefu na tukaishia hapo hapo tu, jambo hili
halitakuwa na maana. Maana mtu yeyote aweza kuweka habari yoyote ile na
kuiweka katika wingi wa maneno kama hayo. Jambo muhimu hapa ni kuwa riwaya
huwa na mchangamano wa matukio, ujenzi wa wahusika na dhamira, muundo wake
na hata mtindo maalumu.
Maelezo ya wataalamu hawa juu ya riwaya ni muafaka katika kukamilisha utafiti
wetu kwa sababu wametueleza mambo ya msingi hususani juu ya kwamba, riwaya
hutungwa kulingana na uwezo wa fanani. Hii ina maana kwamba, mtunzi wa riwaya
hutunga riwaya yake kwa hadhira maalumu na si kila mtu anaweza kuwa hadhira ya
riwaya hiyo. Mawazo hayo yanaungwa mkono na Kezilahabi (1983:235) anaposema:
“Kwa bahati, hivi sasa hatuwezi kusema kuwa kuna riwaya ya
Kiswahili ambayo haieleweki kabisa kwa watu; ingawa dalili za
kuanza kuandika riwaya na hadithi fupi zisizoeleweka kwa urahisi
zimeanza kuonekana. Jambo ambalo ningependa kuonya hapa ni
kuwa, mwandishi wa riwaya, asisukumwe kuandika riwaya kwa ajili
ya watoto wa shule. Riwaya si kitabu cha kiada na si cha ziada.
Mwandishi wa riwaya si mtu wa kufugwa, lakini si mtu anayeweza
kuruhusiwa kusema chochote kile anachotaka awe hana mipaka”.
Maelezo haya yanaonesha, mtunzi wa riwaya anayo fursa ya kuandika riwaya kwa
hadhira fulani ambayo yeye anataka kuiandika na isiwe rahisi riwaya hizo kueleweka
kwa kila hadhira. Pamoja na kuonesha kwamba, mtunzi wa riwaya anao uhuru wa
kuandika riwaya yake vile anavyotaka bado ana mipaka ya kiuandishi. Kauli
kwamba “mwandishi aandike anachotaka awe hana mipaka” ni nzito. Mwandishi
15
yeyote hutawaliwa na ujumi, ubunifu, usanii na lengo kuu la hazina ya jamii yake
ambamo yeye hupewa fursa ya kuchota kiasi cha kumtosha kwa ridhaa na kwa niaba
ya hiyo jamii kuu. Mradi mwandishi ni zao la jamii; kufungwa kwake ni katika kutii
mafunzo ya mama (jamii) ili asipate mikasa ya adhabu za ulimwengu.
Mhando na Balisidya (wameshatajwa) wamekwenda mbali zaidi na kutaja hata idadi
ya maneno ambayo inatakiwa kuiunda riwaya. Wanasema kwamba, riwaya inaweza
kuwa na maneno kuanzia 35000 na kuendelea. Bila shaka, maneno haya ni
mengi.Kwa maoni yetu, riwaya inaweza pia kuwa na maneno chini ya hayo na bado
ikaitwa riwaya. Jambo la msingi ni kwamba, riwaya hiyo sharti iwe na maudhui na
hicho kinachoelezwa, kielezwe kwa ufundi na ufanisi.
Senkoro (1977) yeye anasema riwaya ni kisa ambacho ni kirefu vya kutosha, chenye
zaidi ya tukio moja ndani yake. Ni kisa mchangamano ambacho huweza
kuchambuliwa na kupimwa kwa uzito na undani kwa mambo mbalimbali ya
kimaudhui na kiufundi. Riwaya ni kisa ambacho urefu wake unakiruhusu na
kutamba mahali pengi na kuambaa vizingiti vingi kama apendavyo mwandishi wake.
Maelezo haya yanaeleza kwamba, riwaya ni lazima iwe na urefu wa kutosha wa
kuitamba hadithi. Hivi ndivyo ilivyo katika riwaya za Shafi Adam Shafi ambazo sisi
tunazishughulikia katika utafiti wetu.
Wamitila (2003) anasema kwamba, riwaya ni kazi ya kinathari na kibunilizi, ambayo
huwa na urefu wa kutosha, msuko uliojengeka vizuri, wahusika wengi
walioendelezwa kwa kina, yenye kuchukua muda mwingi katika maandalizi yake na
kukitwa katika mandhari muafaka. Maelezo haya ya Wamitila hayatafautiani sana na
16
ya wataalamu wenzake. Yeye anatufunza jambo moja muhimu katika taaluma ya
riwaya, nalo ni lile la wahusika, matukio na dhamira kuwa ni lazima kukubalika na
mandhari. Muktadha na Mandhari husaidia kumfanya msomaji ayapate maudhui kwa
urahisi kwa vile yanavyoendana na fikra za jamii hiyo ya riwaya. Mandhari ni
miongoni mwa vipengele vya fani katika kazi ya fasihi. Ujuzi wa matumizi ya
mandhari katika kazi za fasihi hutegemea uhodari wa mwandishi. Katika utafiti wetu
tutaonesha ni namna gani Shafi Adam Shafi ameweza kuzikita kazi zake katika
muktadha na mandhari ya jamii inayohusika.
Njogu na Chimerah (1999) wanasema, riwaya ni utungo mrefu wa kubuni, na wenye
ploti, uliotumia lugha ya nathari. Lakini ploti ni nini? Ploti inahusu maingiliano na
mazuano ya vitushi. Yaani, ploti ni jinsi vitushi, katika kazi ya sanaa,
vinavyoingiliana na kuzuana. Maana hii ya riwaya haitofautiani sana na zile
zilizotolewa na wataalamu wengine ambao tumewaona hapo juu. Badala yake,
wataalamu hawa wawili wametuletea misamiati mipya lakini inarejelea mambo yale
yale yaliyokwisha kuelezwa na wataalamu watangulizi. Misamiati hiyo ni “vitushi”
ukiwa na maana ya visa na matukio na “ploti” ikiwa na maana ya muundo.
Mulokozi (1996), anahitimisha kwamba, ili kuifahamu vizuri maana ya riwaya ni
vema kuzingatia mambo kadhaa, kama vile, matumizi ya lugha ya kinathari, isawiri
maisha ya jamii, iwe na masimulizi ya kubuni na visa virefu, wahusika zaidi ya
mmoja, iwe na msuko na mpangilio wa visa matukio, maneno zaidi ya 35000 na
kuendelea, ifungamane na wakati, yaani visa na matukio vifungamane na wakati.
Hitimisho hili lililotolewa na Mulokozi juu ya maana ya riwaya ndilo tulilolichukua
na kulifanyia kazi katika utafiti huu. Riwaya za Shafi Adam Shafi ambazo
17
tunazishughulikia katika utafiti wetu zimejengwa kwa kutumia vigezo ama sifa hizi
ambazo zinatajwa na Mulokozi (ameshatajwa).
2.3 Historia na Chimbuko la Riwaya ya Kiswahili
Njogu na Chimerah (1999) wanaeleza kwamba, historia ya riwaya ya/kwa Kiswahili
inafungamana na historia ya maendeleo ya jamii za Afrika ya Mashariki. Hii ina
maana kwamba, mtu anapotaka kueleza juu ya chimbuko la riwaya ya/kwa
Kiswahili, basi anapaswa kutazama maendeleo ya jamii ya Waswaahili wa Pwani
katika vipindi mbalimbali vya maendeleo yao kiuchumi, kisiasa, kijamii na
kiutamaduni.
Mulokozi (1996) naye anaeleza kuwa chimbuko la riwaya/kwa Kiswahili lipo katika
mambo makuu mawili ambayo ni fani za kijadi za fasihi pamoja na mazingira ya
kijamii. Maelezo hayo yanaonesha kukubaliana na yale ya akina Njogu na Chimerah
(tumeshawataja) ambao nao wanasema kuwa, “chimbuko la riwaya ya Kiswahili ni
ngano za kisimulizi.” Mawazo hayo yanakubalika kutokana na ukweli kwamba
masimulizi ya ngano ndiyo yaliyochukuliwa na kutiwa katika maandishi na kuipata
riwaya ya/kwa Kiswahili (Mulokozi, tumeshamtaja).
Madumulla (2009) ana mawazo zaidi juu ya chimbuko la riwaya ya/kwa Kiswahili
kwamba, riwaya ilitokana na nathari bunilifu kama vile hadithi, hekeya na ngano
zilizosimuliwa tangu kale. Riwaya ilitokana na maandiko ya fani ya ushairi, hususani
tendi za Kiswahili katika hati za Kiarabu- Kiswahili kwa sababu ndiyo maandishi
yaliyokuwako katika Pwani ya Afrika ya Mashariki. Riwaya ya/kwa Kiswahili
inatokana na fasihi simulizi si kauli yenye mashaka. Historia ya/kwa riwaya ya
18
Kiswahili, inafungamana na historia ya Waswahili wa Pwani. Ngano zinazotajwa na
Madumula (tumeshamtaja) ni hadithi ambazo watoto walisimuliwa wakiwa na bibi
na babu wakati wanaota moto usiku na kwa sasa wakiwa darasani au mahala popote
panapofaa.
Hata hivyo, Senkoro (1977) anaeleza kuwa, chimbuko la riwaya bila shaka ni The
Novel, ni ubepari uliosababishwa na mapinduzi ya viwanda huko Ulaya. Mapinduzi
ya viwanda yalileta mabadiliko makubwa katika mienendo ya jamii na hivyo kuleta
aina mpya ya maisha iliyojulikana kama “mchafu koge” au kama anavyoita
Kezilahabi “Dunia uwanja wa fujo”. Ni katika kipindi hiki ndipo masuala ya wizi,
ubakaji, uuaji, njaa, ufedhuli, ukata, kukua kwa matabaka, unyonyaji na kadhalika
yalikuwa kwa kasi kubwa katika jamii za Ulaya na athari zake kuzifikia jamii za
makoloni, Afrika. Ni kutokana na kuwapo kwa mambo yote hayo ndipo ikalazimika
kuwapo na aina ya utanzu wa fasihi ambao ungeweza kuyasawiri masuala hayo.
Utanzu huo si mwingine, bali ni riwaya ambayo ndiyo ina sifa ya kueleza visa na
matukio kwa ufundi zaidi kuliko aina nyingine yoyote katika tanzu za fasihi.
Maelezo haya ya Senkoro (1977) yanaonesha kuwa na ukweli juu ya riwaya-andishi
(The Europian Novel). Hata hivyo, asili ya riwaya ya/kwa Kiswahili haifungamani
na ubepari kwa sababu hata kabla ya ujio wa Wakoloni, Waafrika wote, Waswahili
wakiwemo, walikuwa na masimulizi ya hadithi na ngano ambazo hasa ndivyo
vyanzo au visimbuzi vya masimulizi vya riwaya ya/kwa Kiswahili. Mazungumzo
ndiyo yaliyoanza na kisha kufuata maandishi. Maandishi hadi leo bila ya kusomwa,
kujadidiliwa, kuzungumzwa, fasihi andishi haiwezi kuwapo. Kwa mantiki hiyo,
kusema kwamba, riwaya ya/kwa Kiswahili ilitokana na mwanzo wa ubepari huko
19
Ulaya ni ukweli lakini unaowatosha watu wa Ulaya na huko Marekani juu ya
chimbuko na historia ya riwaya ya au kwa Kiswahili, ndani ya Afrika, chanzo ni
hisiya tu za kawaida zilizohusu maisha kwa jumla yake (Sengo na Kiango, 2012).
Njogu na Chimerah (1999) wanasema kwamba, riwaya ya kwanza ya Kiswahili
kuandikwa ni Uhuru wa Watumwa iliyoandikwa na Mbotela. Wanasema:
“Polepole pakaanza kuibuka maandishi ya nathari yaliyotokana na
Waafrika wenyewe. Kwa mfano, kitabu cha Uhuru wa Watumwa
(1934) kilichoandikwa na James Mbotela, ni usimulizi wa kinathari
unaoshughulikia uhusiano baina ya mataifa ya kimagharibi na ya
Kiafrika. Katika usimulizi huu Mwarabu na/au Mwislamu
wanalaumiwa kwa utumwa uliokuwemo Afrika Mashariki ilhali
mkoloni anasifiwa kwa kuleta uhuru, hata ijapokuwa utumwa ulitiwa
nguvu na ukoloni. Baada ya 1940 na kuendelea hadi miaka ya sitini,
riwaya nyingizilifuata mkondo wa ngano za fasihi simulizi kama
“Paukwa pakawa… Hapo zamani zakale paliondokea…”
Kimaudhui, nyingi zilikuwa na mambo ya mila na tabia kama njia ya
kufunza maadili” (1999:37).
Kimsingi, nukuu hii inawasilisha na kuthibitisha kuwa riwaya ya kwanza ya
Kiswahili iliandikwa katika mwaka wa 1934 lakini hata jina la riwaya yenyewe
inaonesha kwamba, ilianza kama masimulizi ya watumwa na baadaye kuwekwa
katika maandishi ambayo leo ndiyo yaliyotamalaki kuliko masimulizi. Ufafanuzi huu
wa historia ya riwaya umetufungua zaidi katika uelewa wetu na kwamba,
tunapochambua riwaya za Shafi Adam Shafi tunazingatia pia suala la historia ya
utunzi wake ili kupata vilivyo dhamira mbalimbali.
2.4 Dhamira katika Riwaya ya au kwa Kiswahili
Uchunguzi na uhakiki wa dhamira katika riwaya za/kwa Kiswahili, umefanywa na
watafiti wengi kwa makusudio mbalimbali. Mmoja, kati ya waliohakiki dhamira,
katika riwaya za/kwa Kiswahili ni Sengo (1973a) katika Hisi Zetu amehakiki riwaya
ya Mtu ni Utu. Dhamira kuu aliyoiona katika kazi hiyo ni ile inayohusu misingi na
20
umuhimu wa kila mwanadamu kuwa na utu kwa manufaa ya wanadamu wenzake.
Anaeleza kwamba, mwanadamu ni tofauti na mnyama kwa sababu yeye ana uwezo
wa kiakili ambao akiutumia vizuri utamfanya awe na utu bora zaidi. Katika riwaya
ya Mtu ni Utu, kunaelezwa bayana kwamba, ipo tofauti ya msingi kati ya maneno
binadamu na utu na kwamba si kila binadamu ana utu. Wapo baadhi, wana utu
tafauti na ule unaotarajiwa na wengi. Shaaban Robert (1968) analisisitiza suala la utu
katika riwaya yake ya Maisha Yangu na Baada ya Miaka Hamsini kuwa:
“Utu ulikuwa jambo la aushi lililohusu wanadamu wote, na kanuni
ilikuwa tabia ya milele, haikufa; haifi wala haitakufa” (uk.100).
Njogu na Chimerah (1999:50) wanashadidia hoja hii kwa maelezo kwamba, Shaaban
Robert alikuwa anasisitiza kwamba, utu ndicho kiini cha ubinadamu na yeyote
ambaye amekiukana nao, hawi mtu wa kisawasawa. Wanadondoa katika Maisha
Yangu na Baada ya Miaka Hamsini kuwa:
“Mwanadamu alikuwa si mnyama, mchache wa wajibu na daraka;
alikuwa kiumbe wa heshima na dhima ambaye alistahiki ushirika wa
adili katika ndoa. Ilikuwa nini kama si ujinga mtupu kutupilia mbali
madaraka na wajibu wetu? Ilikuwa nini kama si ukosefu wa
matumizi bora ya akili kujisawazisha sisi wenyewe na wanyama?
Ilikuwa nini kama si aibu kubwa kuacha heshima iliyopambanua
ubora wetu katika viumbe?” (uk.98).
Dondoo hili kwa hakika linaonesha kwamba, utu wa mwanadamu ni kitu muhimu
sana katika maisha na ndicho kitu pekee ambacho kinamtofautisha mwanadamu na
wanyama wengine. Mwanadamu anapoacha kutenda kiutu, basi hugeuka kuwa na
hadhi ya chini ya mnyama.
Maelezo ya Njogu na Chimerah (tumeshawataja) yana umuhimu mkubwa katika
utafiti wetu kutokana na kule kutufafanulia kwamba katika riwaya ya Kiswahili
21
kunaelezwa dhamira mbalimbali zinazohusu masuala ya utu wa mwanadamu. Baada
ya ufafanuzi huu juu ya utu wa mwanadamu ufahamu wetu umefunguka zaidi na
kuweza kuielewa dhamira hii kwa kiwango cha juu na kuihusianisha na riwaya
ambazo tunazishughulikia katika utafiti huu. Kwa mfano, katika Kuli tunaoneshwa
namna Wazungu walivyokuwa wamekosa utu kutokana na kuwatesa watumishi wa
bandarini kwa malipo kidogo na kutowapatia matibabu na fidia pale walipopata
matatizo kazini.
Sengo (1973a) katika mwendelezo wa uhakiki tuliouona hapo juu, alihakiki pia
riwaya ya Utu Bora Mkulima na kuainisha moja ya dhamira hizo kuwa ni ile ya
umuhimu wa kila mtu kufanya kazi kwa bidii kama njia pekee ya kujiletea
maendeleo. Dhamira ya utu wa mwanadamu kama alivyoianisha hapo juu, haiwezi
kupatikana kama mwanadamu hatajishughulisha katika kufanya kazi kwa bidii.
Mwanadamu anapokuwa hafanyi kazi kwa bidii hushindwa kupata kipato cha
kukidhi mahitaji yake na hivyo anaweza kuukosa utu. Hii ina maana kwamba, katika
harakati za kutaka kukidhi mahitaji, mwanadamu asiye na kipato, anaweza kufanya
uhalifu ili apate kukidhi mahitaji yake. Kwa msingi huo, utu wa mwanadamu
unakwenda sambamba na kufanya kazi kwa bidii. Moja kati ya falsafa za Sengo ni
kushikilia kuwa, “kazi ni uhai,” na kazi ni Ibada” (Sengo, 2014).
Katika riwaya za Shafi Adam Shafi, tulizoziteua, tumeona kuwa, wahusika wake
walifanya kazi kwa bidii, na maarifa ili kujipatia maendeleo.Makuli walikuwa
wakifanya kila kazi kwa bidii kila uchao, kwa malipo ya mkia wa mbuzi. Ufanyaji
kazi huo umewafanya kuwa ni watu ambao wanapenda taratibu za utu wao ambao
ungewawezesha kuishi maisha mazuri katika jamii zao. Mawazo hayo ya Sengo
22
(1973a) yametuongeza nguvu za kuendeleza utafiti wetu. Sengo (1973b) aliandika
makala ya, “Dhima ya Fasihi kwa Maendeleo ya Jamii,” ambamo alieleza dhima
mbalimbali za fasihi katika jamii; kuwa ni kuadilisha, kuonya, kufichua maovu,
kutetea haki za watu, kuburudisha, kukosoa sera za maendeleo na kupendekeza sera
mbadala za kuliletea taifa maendeleo endelevu.
Fasihi ni kuwa kioo cha jamii ambacho kila mwanajamii hujitazamia na baada ya
hapo hujifunza mengi kutokana na yale aliyoyaona katika kioo hicho. Mawazo hayo
ya Sengo (1973b), yanamchango muhimu katika kusukuma mbele utafiti wetu. Hii
imekuwa ni ukumbusho kwetu kwamba, tunapotafiti riwaya za Shafi Adamu Shafi,
tunatakiwa tufahamu kwamba, hii ni kazi ya fasihi na ina dhima zake kwa jamii
husika. Ufahamu huu umeturahisishia kazi ya utafiti wetu kwa sababu kila mara
tulipokuwa tunasoma riwaya teule mawazo haya ya Sengo (tumeshamtaja) yalikuwa
yakipita kichwani mwetu kwa msisitizo mkubwa.
Mwanataaluma mwingine aliyetafiti dhamira katika riwaya za Kiswahili ni
Kezilahabi (1976). Aliandika tasinifu ya Uzamili yenye anuani isemayo “Shaaban
Robert: Mwandishi wa Riwaya.” Katika kazi hiyo, Kezilahabi alitia mkazo kwamba,
dhamira ya utu na heshima kwa mwanadamu ndiyo dhamira kuu inayojitokeza katika
riwaya za Shaaban Robert. Hili linajitokeza pale Shaaban Robert anapozungumzia
masuala ya upendo, amani, hekima, busara na wema kuwa ni mambo muhimu
ambayo kila mwanadamu anapaswa kupambika nayo. Vilevile, anaonya juu ya
chuki, choyo, ubahili, ukatili, wivu mbaya, unafiki, uchochezi, uchonganishi na fitina
kuwa ni mambo mabaya ambayo mwanadamu hapaswi kupambika nayo na
anapaswa kukaa mbali nayo. Ndani ya tasinifu yake, Kezilahabi anamsifu Shaaban
23
Robert kuwa ni mlimwengu kwa sababu anasawiri masuala yanayohusu sehemu
mbalimbali za jamii duniani na si jamii ya Waswahili peke yake. Kwa upande
mwingine, ana mawazo tofauti kuhusu matumizi ya wahusika ambao Shaaban Robert
anawatumia katika riwaya zake kama vile Karama, Majivuno na Utu Busara kuwa si
wahusika halisia katika jamii.
Dhamira zilizowasilishwa na riwaya za Shaaban Robert, zimetoa athari za namna
fulani uandishi wa Shafi Adam Shafi.Dhamira ya upendo na mapenzi ya dhati
inavyojitokeza katika kazi teule, kitaaluma inaonekana imetokana na hayo
aliyoyashughulikia Shaaban Robert. Shaaban Robert aliwatumia wahusika wake kwa
nia ya kuweka msisitizo kwamba, ipo haja ya kila mwanajamii kuwa mtu mwema
kwa kuiga mema yanayofanywa na baadhi ya wahusika wa kazi zake. Hili kalifanya
kwa kuzingatia Nadharia ya Kiislamu ya fasihi inayomtaka muumini kutenda na
kuhimiza mema (Sengo, 2009). Pia, kila mwanajamii aepuke mambo mabaya na
maovu. Kwa maoni yetu, wahusika wa aina hii wanao uhalisia katika jamii
aliyokuwa akilelewa Shaaban Robert. Hata hivyo, katika jamii ya leo ni nadra sana
kukutana na wahusika wa aina hii katika kazi za fasihi bali wapo wahusika wenye
sifa mchanganyiko kama wale wanaotumiwa na Shafi Adam Shafi.
Senkoro (1982) alihakiki riwaya ya Dunia Uwanja wa Fujo na kueleza kwamba,
riwaya hii inawasilisha dhamira mbalimbali ikiwapo ile ya matabaka katika jamii,
hususani katika kipindi cha Azimio la Arusha. Anasema kwamba, mtunzi anaonesha
kuwa lengo la kuanzishwa kwa Azimio la Arusha halikufikiwa kama ilivyokuwa
imekusudiwa kwa sababu baadhi ya viongozi walikuwa ni wabinafsi na kufanya
mambo mbalimbali ya kuhujumu uchumi ambayo yaliwanufaisha wao binafsi huku
24
wananchi wa kawaida wakiishi maisha ya dhiki na duni. Maelezo haya ya Senkoro
(1982) tunakubaliana nayo kwa sababu hata sisi tulipopata fursa ya kusoma riwaya
hiyo tulikutana na dhamira hii. Uwepo wa dhamira hii katika riwaya za Kiswahili
unafafanuliwa na kuthibitishwa pia na Chuachua (2011). Mawazo ya mhakiki
Senkoro (ameshatajwa) yamekuwa na umuhimu mkubwa katika kupeleka mbele
utafiti wetu kwa msingi kwamba, umetufahamisha namna ya kuipata dhamira ya
utabaka katika jamii, nasi tukafanya hivyo hivyo katika riwaya za Vuta N’kuvute na
Kuli kisha tukaiainisha dhamira hii ya utabaka kama inavyoonekana katika sura ya
tano ya tasinifu hii.
Mlacha na Madumulla (1991) wanasema kuwa, riwaya ya/kwa Kiswahili, imepiga
hatua kubwa ya maendeleo katika kusawiri dhamira mbalimbali kabla na baada ya
kupatikana kwa uhuru. Katika kipindi cha kabla ya kupatikana kwa uhuru, riwaya za
Shaaban Robert, kama vile Kusadikika na Kufikirika, ndizo riwaya zilizosheheni
dhamira ya ukombozi hasa wa kisiasa. Dhamira zinazowasilishwa katika riwaya hizo
ni masuala ya haki na usawa katika jamii, kuheshimiana, utawala bora wa sheria,
kukomesha dhuluma na rushwa na kujenga misingi ya ubinadamu katika jamii.
Katika kipindi cha ukoloni, Waafrika walinyanyaswa sana na wakoloni. Shaaban
Robert katika kuziandika kazi hizi mbili, aliwasilisha dhamira muafaka kwa jamii
yake ya wakati ule na hata jamii ya sasa. Mawazo hayo yanajitokeza katika kazi za
Shafi Adam Shafi tulizoziteua ingawa tunakiri kwamba, kazi hizi zimeandikwa
katika muktadha tofauti.
Vilevile, Mlacha na Madumulla (tumeshawataja) wanaendelea kueleza kwamba,
dhamira ya ujenzi wa jamii mpya ndiyo iliyotawala katika riwaya zilizoandikwa
25
mara tu baada ya kupatikana kwa uhuru na kuendelea. Miongoni mwa kazi za riwaya
wanazozitaja kuwa ziliisawiri dhamira hii vilivyo ni zile za Kezilahabi, hususani
Rosa Mistika, Gamba la Nyoka, Kichwa Maji na Dunia Uwanja wa Fujo. Pamoja na
mambo mengine, wanaeleza kwamba, riwaya hizi zinaitathimini kwa makini jamii
mpya ambayo inajengwa baada ya kupatikana kwa uhuru kwa kubainisha upungufu
wa mbinu zinazotumika kujenga jamii mpya na hata kupendekeza mbinu muafaka za
kuchukuliwa. Kwa mfano, katika Gamba la Nyoka tunaoneshwa kwamba, Ujamaa na
Kujitegemea ilikuwa ni mbinu nzuri ya kujenga jamii mpya iliyo chini ya misingi ya
usawa na haki. Hata hivyo, ubinafsi na tamaa za viongozi ndio uliosababisha
kushindwa kwa mbinu hii ya ujenzi wa jamii mpya.
Maelezo kuhusu dhamira ya ujenzi wa jamii mpya yanayotolewa na Mlacha na
Madumulla (tumeshawataja) ni muhimu katika kupeleka mbele utafiti wetu. Hii
inatokana na msingi kwamba mambo yaliyomo katika riwaya za Shafi Adam Shafi ni
pamoja na ujenzi wa jamii mpya. Hata hivyo, maelezo ya Mlacha na Madumulla
(tumeshawataja), juu ya ujenzi wa jamii mpya, na hata yale ya dhamira ya ukombozi,
hayakuwa ya kina kirefu. Utafiti wetu umejaribu kuingia ndani zaidi na kuchambua
dhamira mbalimbali zinazojitokeza katika riwaya za Vuta N’kuvute na Kuli.
Nao Njogu na Chimerah (1999) wamechambua dhamira kadhaa ambazo zinapatikana
katika riwaya za Kiswahili hususani zile za Shaaban Robert na watunzi wengine.
Miongoni mwa dhamira waliyoiona ikijitokeza katika riwaya ya Kusadikika ni ile ya
unyonyaji wa rasilimali za Watanganyika uliofanywa na wakoloni. Wanasema,
katika Kusadikika kwa mfano, tunaelezwa kwamba, akina mama walikuwa wakizaa
watoto mapacha. Hii inatoa ishara kwamba, nchi hii ya Tanganyika ina rasilimali
26
nyingi ambazo ni muhimu kwa maendeleo ya taifa lakini rasilimali hizo zinatumiwa
kwa maslahi ya Wazungu na mataifa yao.
Maelezo haya yametupatia mwanga wa kuweza kuelewa zaidi dhamira
zinazojitokeza katika riwaya tulizoziteua. Hii inatokana na ukweli kwamba, katika
riwaya teule, tumeona mapambano ya kitabaka kati ya wazawa na wageni na bila
shaka mapambano hayo yalilenga kuleta haki na usawa katika matumizi ya rasilimali
za taifa kwa maendeleo ya taifa na si ya mtu mmojammoja na wala si kwa
maendeleo ya mataifa ya kigeni. Hata hivyo, uchambuzi wa Njogu na Chimerah
(tumeshawataja) ulikuwa ni wa kudokeza dokeza tu kwa kuwa halikuwa lengo lao
kufanya uchambuzi wa riwaya husika kwa kina bali walifanya hivyo kama sehemu
ya kukamilisha madhumuni yao waliyokuwa nayo. Katika utafiti wetu tumezama
katika kina kirefu cha uchambuzi wa masuala hayo katika riwaya za Vuta N’kuvute
na Kuli.
Mhakiki na mtafiti mwingine aliyeandika juu ya dhamira katika riwaya ya/kwa
Kiswahili ni Mbatiah (1998) katika makala yake “Mienendo mipya katika uandishi
wa Kezilahabi: Nagona na Mzingile. Katika makala haya amenadika masuala mengi
lakini kubwa lililotuvutia sisi ni dhamira ya malezi kwa watoto kutoka kwa wazazi
wao. Anaeleza kuwa, dhamira hii inaelezwa katika riwaya ya Rosa Mistika
iliyoandikwa na Kezilahabi (1971) akiwa mwanafunzi wa Shahada ya kwanza katika
Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam. Kwa muhtasari anaeleza kuwa wazazi
wanaomchango mkubwa katika kuwafanya watoto wao kuwa na tabia nzuri au
mbaya kutokana na malezi watakayowapatia. Kwa mfano, Zakaria ambaye ni baba
yake Rosa, aliwabana watoto wake wa kike bila kuwapa uhuru hata wa kuongea tu
27
na mwanamme yeyote yule; hilo lilikuwa ni kosa la jinai kwake na mtoto aliadhibiwa
vikali kwa kufanya hivyo. Madhara ya malezi haya yanaonekana pale Rosa
alipokwenda kusoma katika chuo cha ualimu na kuupata uhuru wa kufanya mambo
mengi aliyonyimwa kuyafanya akiwa nyumbani kwao. Uhuru alioupata Rosa
ulimfanya apate matatizo mengi na mwishowe alifikia uamuzi wa kujiua.
Maelezo ya Mbatiah (1998) ni muhimu katika kusukuma mbele utafiti wetu kwa
kuwa umetudokezea dhamira ya malezi ya watoto katika jamii. Katika riwaya teule
za Shafi Adam Shafi wapo watoto kama vile Yasmini na Rashidi ambao nao
wanapewa malezi mbalimbali kutoka kwa wazazi wao na jamii yao. Katika utafiti
wetu tumeonesha ni kwa vipi malezi waliyoyapata yamewasaidia kuwa na maadili
mazuri au yasiyo mazuri katika jamii wanayoishi.
Shivji (2002) aliandika makala kuhusu riwaya ya Makuadi wa Soko Huria na
kuainisha masuala mbalimbali yanayozungumzwa na mwandishi wa riwaya hiyo.
Anasema kwamba, yeye si mhakiki wa kazi za fasihi lakini mambo yanayoelezwa na
Chachage katika riwaya hiyo yamemvutia sana na akaona kuna haja ya kuandika
makala yaliyochambua dhamira ya migogoro ya kitabaka kati ya wavuja jasho au
walala hoi na walala heri/vizuri. Wavuja jasho ni watu masikini ambao wapo katika
tabaka la chini huku walala heri/vizuri ni wale wa tabaka la juu. Tabaka la juu katika
jamii ni lile la viongozi ambao ndio wahusika wakuu katika kutiliana saini mikataba
ya uwekezaji katika rasilimali za taifa. Kutokana na hali hiyo, rasilimali nyingi za
taifa, hasa madini, ardhi, gesi, wanyama pori na rasilimali watu hupatiwa wawekezaji
ambao hunufaika kwa kiasi kikubwa zaidi kuliko kunufaika kwa wananchi wa
kawaida.
28
Mawazo haya ya Shivji (ameshatajwa) ni ya kweli na yanasawiriwa katika riwaya za
Shafi Adam Shafi ambazo tumezishughulikia katika utafiti wetu. Shafi Adam Shafi
naye, anasawiri dhamira ya unyonyaji wa rasilimali za taifa unaofanywa na viongozi
wakishirikiana na wawekezaji huku wananchi wa kawaida wakishindwa kupata hata
mahitaji yao ya kila siku.
Naye Mohamed (2006) anaeleza dhamira mbalimbali ambazo zinajitokeza katika
riwaya ya Siku ya Watenzi Wote (1968) ya Shaaban Robert. Dhamira kuu anayoiona
yeye ni ile ya Muungano wa dini za Kiislamu na Kikiristo kuwa dini moja. Anaeleza
kuwa; Shaaban Robert ni mmoja kati ya waandishi mashuhuri aliyeona mbali na
kuzitaka dini hizi mbili ambazo ni kubwa katika jamii kuungana na kuwa kitu kimoja
ili kuepusha migogoro na machafuko ya kidini yanayotokea katika sehemu
mbalimbali duniani. Katika kushadidia hoja hii Mohamed (tumeshamtaja) anadondoa
sehemu katika Siku ya Watenzi Wote; isemayo,
“Sioni kuwa shida. Jumuiya imekwisha jithibitisha yenyewe kuwa
bora kwa kufuata mwenendo wa ulimwengu na tabia ya watu wake.
Pana umoja wa mataifa, pana umoja wa dola, pana umoja wa rangi,
pana umoja wa udugu kwa ajili ya manufaa ya maisha ya kitambo.
Si ajabu kukosekana umoja wa dini kama ulimwengu wataka kweli
kuendesha na kutimiza wajibu wake?” ... (uk. 83).
Katika dondoo hili tunaoneshwa namna Shaaban Robert anavyosisitiza juu ya
dhamira yake ya kutaka kuona kwamba, dini zote zinaungana na kuwa kitu kimoja
kama ilivyokuwa kwa jumuiya mbalimbali ambazo zimeungana kama alivyozitaja.
Hata hivyo, uelewa wetu juu ya dhamira hii unatofautiana kidogo na uelewa wa
Mohamed (tumeshamtaja). Kwa ufahamu wetu, alichokitaka Shaaban Robert hapa ni
kuona kwamba, dini zote zinakuwa kitu kimoja kwa kila moja kuheshimu misingi ya
dini nyingine bila kuingilia wala kukosoana. Ni kutokana na kutoheshimu misingi ya
29
dini nyingine ndio maana kunatokea machafuko ya hapa na pale yakihusisha masuala
ya dini. Shaaban Robert anafahamu fika kwamba, dini ni suala la imani na kwamba,
kuchukua imani mbili ambazo ni tofauti na kujenga imani mpya itakayokubaliwa na
pande zote ni suala gumu sana. Lakini anaamini kwamba, dini hizi zitakuwa kitu
kimoja kwa kuheshimiana na kuthaminiana. Mawazo haya yanatupatia uelewa
kwamba, tunapohakiki au kuchambua kazi ya kifasihi tunatakiwa tuwe makini kwa
kuisoma kazi fulani kwa kina na kurudiarudia ili tuweze kupata dhamira stahiki.
Tumefanya hivyo katika utafiti wetu na kufanikiwa kuwasilisha dhamira mbalimbali
kama zinavyojitokeza katika sura ya nne ya tasinifu hii.
Mtaalamu mwingine ni Mwaifuge (2006) ambaye alifanya uhakiki wa dhamira ya
rushwa katika riwaya ya Kitu Kidogo tu iliyoandikwa na Thomas Kamugisha. Katika
makala yake aliyoiita “Fasihi ya Kiswahili na Rushwa Tanzania: Thomas A.
Kamugisha na Kitu Kidogo tu anaisawiri vilivyo dhamira ya rushwa katika jamii.
Anaeleza kwamba, rushwa katika jamii imeenea kila mahali na kila ambaye
anajaribu namna ya kupambana na rushwa anashindwa kwa sababu anakosa watu wa
kumsaidia katika mapambano hayo Anasema:
“Mwandishi anamchora Musa kama mtu mwenye msimamo, msomi
na mkombozi anayekuja toka masomoni nje ya nchi kuikomboa nchi
yake iliyopoteza dira na mwelekeo. Tatizo linalomkabili musa ni
kwamba, yuko peke yake. Hakuna anayemuunga mkono katika
kuikataa rushwa. Jamii ya Tanzania inaonekana kuukubali
utamaduni huu mpya” (2006: 41).
Kupitia nukuu hii tunaona kwamba, rushwa katika jamii imekuwa ni sehemu ya
utamaduni ambapo kila mtu anaiona kuwa ni kitu cha kawaida. Hali hii inasababisha
wale wachache ambao wanakataa kutoa na kupokea rushwa kuonekana kama
wasaliti na hivyo kutopatiwa ushirikiano husika. Mrikaria (2010) anaunga mkono
30
maelezo haya pale anaposema kwamba, katika Miradi Bubu ya Wazalendo (1995)
iliyoandika na Ruhumbika, mtunzi anasawiri kuenea kwa rushwa katika jamii.
Anadondoa sehemu ya riwaya hiyo isemayo kuwa:
Kila mtu mwenye fursa kwenye ofisi za serikali, kwenye mashirika ya
umma, ugawaji na usagishaji, kwenye maduka ya kaya, akakazana
kuhakikisha hiyo kazi yake au madaraka yanamtajirisha
iwezekanavyo. Matokeo yake wizi, magendo na ulanguzi vikatia fora
na ikawa kila kitu hakinunuliki tena….
Mawazo haya tumeyachukua na kuyafanyia kazi katika utafiti wetu yapo matukio ya
wahusika kupewa au kupeana rushwa kwa nia fulani.Maelezo ya kina kuhusiana na
hili yamefafanuliwa katika sura ya tano ya utafiti wetu. Khamis (2007) ameandika
kwa kiwango kikubwa juu ya fasihi ya/kwa Kiswahili hususani riwaya kwa upande
wa utunzi na uhakiki au uchambuzi. Katika makala yake aliyoandika kuhusu
“Utandawazi au Utandawizi, Jinsi lugha ya Riwaya Mpya ya Kiswahili Inavyodai,”
anaeleza kwa muhtasari kuhusu dhamira za riwaya mpya. Anaeleza kwamba, riwaya
mpya zimevuka mipaka ya kitaifa na kimaeneo katika kusawiri mambo mbalimbali
yanayotokea duniani kote katika kipindi hiki cha utandawazi. Riwaya mpya
anazozirejelea hapa ni zile za E. Kezilahabi za Nagona (1990) na Mzingile (1991),
riwaya ya Walenisi (1995) ya Katama Mkangi, riwaya ya W.E. Mkufya ya Ziraili na
Zirani (1999), riwaya ya Said A. M. Khamis ya Babu Alipofufuka (2001) na ya K.
W. Wamitila ya Bina - Adamu (2002).
Mawazo kwamba riwaya mpya ya Kiswahili imevuka mipaka ya kiuchambuzi na
kiusawiri, kwa kusawiri mambo ambayo yanahusu jamii pana zaidi duniani ni ya
ukweli. Ingawa bado inasawiri masuala ya ndani ya jamii fulani lakini pia tunaona
kuwa yanasawiri maisha ya sehemu kubwa ulimwengu.Mawazo haya tutayachukua
31
na kuyafanyia kazi katika utafiti wetu.Dhamira za riwaya za Shafi Adam Shafi
tumezibaini kuwa nazo zinasawiri sehemu kubwa ya jamii za duniani ingawa riwaya
hizo hazipo katika kundi la riwaya mpya.
Chuachua (2011) alifanya utafiti juu ya Itikadi katika riwaya za Shaaban Robert na
kuainisha dhamira mbalimbali ambazo zinajenga itikadi ya Shaaban Robert juu ya
mambo mbalimbali katika jamii. Anasema kwamba, itikadi ya Shaaban Robert
kuhusu maisha imejengwa na misingi ya dini ya Kiislamu ambayo Shaaban Robert
alikuwa muumini mzuri. Kutokana na itikadi hiyo akawa ni mtu ambaye aliamini
sana katika upendo, mapenzi bora, ukweli, uadilifu, uaminifu, heshima na utu wa
mwanadamu kama mambo muhimu kuwa nayo kila mtu ili kuifanya jamii iishi
maisha mepesi, kila siku. Itikadi hii haijitokezi katika riwaya zake tu bali pia katika
mashairi na insha alizopata kuandika.
Mawazo haya ni muhimu katika kufanikisha utafiti wetu kwa namna moja au
nyingine. Kutokana na utafiti huu tunaelewa kwamba, kumbe kuifahamu itikadi ya
mwandishi ni kitu muhimu sana katika kuwezesha kuyapata maudhui au dhamira
anazozizungumzia kwa ufasaha. Kwa kiasi fulani, nasi tumejitahidi kuifahamu
itikadi ya Shafi Adam Shafi na hivyo kutusaidia kueleza ni dhamira zipi
zinazojitokeza katika riwaya zake tulizoziteua.
Mhakiki na mtafiti mwingine ambaye ameandikia kipengele cha dhamira katika
riwaya ya Kiswahili ni Taib (2008) katika makala, “Mkabala wa Kiisilamu katika
Uchanganuzi na Uhakiki wa Fasihi ya Kiswahili”. Katika makala yake hii anaeleza
kwamba, mkabala huu ni muhimu sana katika kuhakiki kazi zinaonekana kuwa ni za
32
mtazamo wa Kiislamu kwa kuwa kufanya hivyo, kutazitendea haki kazi hizo. Laa
sivyo, kazi hizo zinapohakikiwa kwa mikabala mingine, inakuwa hazitendewi haki
yake. Kwa mfano, wengi wa wahakiki ambao wanahakiki nafasi ya mwanamke
katika kazi za Shaaban Robert wanaonesha kwamba, mwanamke anasawiriwa kama
chombo cha kumstarehesha mwanamme. Iwapo wahakiki hao wangetumia mkabala
wa Kiislamu katika kufanya uhakiki wao basi wasingemsawiri mwanamke kwa
namna hiyo kwa sababu kumstarehesha mwanamme ni wajibu wa mke kama
alivyoagizwa na Muumba wake kupitia mafundisho ya Dini. Mwanamke kuumbiwa
mume na mwanamme kuumbiwa mke, starehe ni wajibu wa watu hao wawili ili
kipatikane kizazi cha kuindesha hii dunia.
Maelezo haya tunakubaliana nayo kwa kiasi kikubwa sana.Mhakiki anapotumia
mkabala au nadharia kama hii na kama zile za Sengo (2009), “Fasihi ina Kwao”,
“Ndani Nje” na “Uhalisiya wa Kiafrika”, majibu atakayopata mtafiti katika utafiti au
uhakiki wake yatakidhi uhalisia wa nadharia aliyoitumia. Ndio maana wahakiki
wanaohakiki kazi, kwa mfano, riwaya au mashairi ya Shaaban Robert, kwa kutumia
mkabala wa Kifeministi wa Kimagharibi, hupata majibu kwamba, mwanamke
anasawiriwa kama chombo cha starehe katika kazi hizo.
Kwa mshangao, mwanamme hatajwi kuwa ni mwenza wa hicho kitendo cha starehe
bali huoneshwa kuwa ni mnyonyaji! Mhakiki au mtafiti mwingine, akihakiki kazi
hiyohiyo kwa kutumia nadharia nyingine kama hii ya mkabala wa Kiislamu,
inayopendekezwa na Taib (ameshatajwa) na Sengo (ameshatajwa) atatoa matokeo
ambayo ni tafauti kabisa, akaweza kutoa hitimishi kwamba, Shaaban Robert
anamsawiri mwanamke kama vile anavyotakiwa kuwa kwa mujibu wa mafundisho
33
na misingi ya Dini ya Kiislamu. Kwa msingi huu, mawazo kwamba, kuhakiki kazi
zenye mtazamo wa Kiislamu kama zilivyo kazi za Shaaban Robert ni kutozitendea
haki si kauli sahihi sana katika ulimwengu wa taaaluma. Tunasema hivi kwa sababu
kazi ya fasihi huwa haina jibu moja na kila mhakiki anao uhuru wa kuhakiki kazi
yoyote ile ya fasihi kwa kutumia mkabala anaoutaka kulingana na lengo lake.
Hata hivyo, nadharia za “kila fasihi ina kwao”, “Mkabala wa Kiislamu” na “Ndani
Nje”, zinambana mhakiki ili asipotoshe mambo ya watu kwa vile lengo la kazi ya
fasihi duniani ni kujenga “furaha ya wote.” Hivyo basi, haja ya kutumia nadharia
fulani katika kufanya uhakiki na uchambuzi wa kazi ya fasihi ni kitu muhimu sana
nasi tumeliona hilo na kisha tukateua nadharia kadhaa ambazo tumezitumia katika
uhakiki wa kazi yetu hii.
Naye Mwangoka (2011) aliandika tasinifu ya Uzamili akichunguza motifu ya safari
na msako katika riwaya za Kezilahabi. Matokeo ya utafiti wake yanaonesha kwamba,
motifu ya safari na msako inayojitokeza katika riwaya za Kezilahabi zinasaidia
kujenga dhamira mbalimbali kwa wasomaji wake. Kwa mfano, kupitia maotifu ya
safari tunapata dhamira inayozungumzia maana ya maisha katika jamii. Maisha ni
kitu ambacho wanadamu wanapambana nacho kila siku na kila siku kuna vikwazo,
furaha, huzuni, mashaka, wasiwasi, mafanikio, matatizo na mambo mengine mengi.
Katika safari hii, msafiri anatakiwa kuwa mvumilivu na mstahamilivu ndio afanikiwe
kufika salama mwisho wa safari yake. Fikira na tafakuri kuhusu maisha
zinazoelezwa katika tasinifu ya Mwangoka (tumeshamtaja) ni muhimu sana katika
kupeleka mbele utafiti wetu. Tumezichukua fikira hizi na kuzihusianisha na
34
uchambuzi wetu wa dhamira katika Vuta N’kuvute na Kuli.Henry (2011) pia ni
mtaalamu mwingine ambaye alifanya utafiti katika Kiswahili juu ya Simulizi za
watumwa katika riwaya ya Uhuru wa Watumwa iliyoandikwa na Mbotela (1934).
Matokeo ya utafiti wake, pamoja na mambo mengine, yanaonesha kwamba,
watumwa walinyanyaswa na kuteswa kwa kazi na adhabu mbalimbali ambazo
hakustahili kufanyiwa mwanadamu. Haya yalifanyika kwa nia ya kuwaleta utajiri
mkubwa wale ambao walikuwa wanawamiliki watumwa. Mtumwa aliyechoka baada
ya kufanya kazi kwa muda mrefu na kushindwa kufanya kazi na kuamua kulala au
kupumzika aliadhibiwa vikali, lengo likiwa arejee kazini.
Mawazo haya tumeyachukua na kuyafanyia kazi katika utafiti wetu kwa maana ya
kuhaulisha mawazo. Katika riwaya za Shafi Adam Shafi tulizoziteua hazizungumzii
masuala ya watumwa kwa sababu zimeandikwa katika kipindi ambacho utumwa
ulikwishakomeshwa. Hata hivyo, malipo kiduchu na manyanyaso wanayopatiwa
makuli katika bandari ni muendelezo tu wa utumwa ingawa ni kwa namna tafauti.
Ufahamu huu wa mambo umetuwezesha kueleza kwa kina dhamira mbalimbali
zinazojitokeza katika riwaya za Shafi Adam Shafi kama zinavyojibainisha katika
sura ya tano ya tasinifu hii.
Kalegeya (2013) alifanya utafiti kuhusu utandawazi katika riwaya za Makuadi wa
Soko Huria (2002) na Almasi za Bandia (1991) zilizotungwa na Chachage S.L.
Chachage. Katika tasinifu yake amebainisha dhamira mbalimbali zinazohusu
masuala ya utandawazi na athari zake kwa jamii. Kwa mfano, anaeleza kwamba,
Chachage anausawiri utandawazi kama chombo cha kunyonyea rasilimali za mataifa
machanga, Tanzania ikiwemo na kutajirisha mataifa ya Ulaya na Marekani huku nchi
35
kama Tanzania zikiendelea kukabiliwa na umasikini mkubwa. Haya yanaonekana
kupitia njia za soko huria na uwekezaji unaofanywa na wageni katika nchi
zinazoendelea. Anasema kuwa, wageni wanakuja kuchuma rasilimali za mataifa
masikini kwa kisingizio cha kuwekeza na kwenda kunufaisha mataifa yao kwa faida
kubwa wanazozipata kutokana na uwekezaji wanaoufanya hapa nchini.
Mawazo haya tunakubaliana nayo kwa kiasi kikubwa kwa sababu yanatoa taswira na
picha kamili ya unyonyaji unaofanywa na mataifa tajiri dhidi ya mataifa masikini.
Wawekezaji wa kigeni hupewa msamaha wa kodi kwa kipindi cha miaka mitano ili
watazame kama biashara wanayoifanya au uwekezaji waliouanzisha unaleta faida au
hauleti. Kama unaleta basi baada ya miaka mitano ndio wanaanza kulipa kodi. Hata
hivyo, uzoefu unaonesha kwamba, kipindi cha miaka mitano kinapofika mwekezaji
hudai kwamba, hapati faida na hivyo kuuza uwekezaji wake kwa mtu mwingine ili
naye apewe msamaha wa kodi na hali huendelea kuwa hivyo kila mara.
Hali hii, kwa hakika, husababisha rasilimali za taifa kama vile, ardhi, madini,
rasilimali watu, mali asili na kadhalika kunyonywa na watu wachache tena wageni
huku wazawa wakikabiliwa na ukata mkubwa. Mawazo haya tumeyachukua na
kuyafanyia kazi katika utafiti wetu kwani hata Shafi Adam Shafi anasawiri masuala
ya kiutandawazi hususani uwekezaji katika bandari uliofanywa na kampuni ya
kikoloni.
2.5 Muhtasari
Katika sehemu hii tumeleza kwa kirefu kuhusu kazi tangulizi ambazo zimechambua
maudhui na hasa dhamira katika riwaya za/kwa Kiswahili na kisha kuhusianisha
36
madhumuni mahususi ya utafiti wetu. Mawazo ya watafiti watangulizi juu ya
dhamira katika riwaya yamekuza ufahamu wetu juu ya nafasi ya riwaya katika
kusawiri hali halisi ya maisha nasi tukapata fursa na kuhusianisha na utafiti wetu.
2.6 Fani katika Riwaya ya Kiswahili
2.6.1 Utangulizi
Fani ni ufundi wa kisanaa unaotumiwa na mtunzi wa kazi ya kifasihi katika kuisana
kazi yake (Omary, 2011). Ufundi huo wa kisanaa unapatikana katika vipengele vya
matumizi ya lugha, wahusika, mtindo, muundo na mandhari katika kazi ya fasihi
(Senkoro, 2011; Msokile, 1992). Ni kutokana na ufundi huo ndio wasomaji husema
wanavutiwa au kutovutiwa na kazi fulani wakati wanaposoma au kusikiliza kazi
husika ya fasihi kama riwaya, ushairi, hadithi fupi, tamthiliya, vichekesho na
maigizo. Watafiti ambao wamehakiki na kuchambua fani katika riwaya ni wengi kwa
kiasi cha kuridhisha huku kila mmoja akichambua au kuhakiki kwa nia tafauti.
2.6.2 Vipengele vya Kifani
Kezilahabi (1983) ametaja vipengele vingi miongoni mwa vipengele hivyo ni
mandhari. Anaeleza kwamba, zipo mandhari za aina mbili katika utunzi wa riwaya
ambazo ni madhari halisi na ile isiyokuwa halisia yaani mandhari bunilifu au
dhahania. Anaendelea kueleza kwamba, mandhari ina mchango mkubwa sana katika
kujenga dhamira mbalimbali ambazo mtunzi anataka ziifikie hadhira yake na
kwamba kukosea katika kipengele cha mandhari huifanya kazi ya fasihi kutotoa
dhamira ambazo zitaeleweka kwa urahisi kwa wasomaji wake. Anataja riwaya ya
Ubeberu Utashindwa iliyoandikwa na Kimbila (1971) kuwa ni miongoni mwa
riwaya ambazo mandhari zake hazijajengwa vizuri, na hivyo kumpa taabu msomaji
37
kuzipata vizuri dhamira za riwaya hiyo. Mawazo haya ya Kezilahabi (tumeshamtaja)
ni muhimu sana katika kusukuma mbele utafiti wetu huu kwa namna mbalimbali.
Kwanza umetufahamisha kwamba, mandhari ni mbinu ya kisanaa ambayo inatumiwa
na mwandishi katika kujenga dhamira mbalimbali za riwaya au kazi nyingine yoyote
ya fasihi. Katika utafiti wetu tumeonesha ni kwa vipi mandhari iliyotumiwa na Shafi
Adam Shafi imesaidia kujenga dhamira mbalimbali tulizoziainisha. Pili, maelezo ya
Kezilahabi yanatufahamisha kwamba, ujuzi wa matumizi ya mandhari katika kazi ya
fasihi hutofautiana kati ya mwandishi mmoja na mwingine. Wapo waandishi ambao
huweza kubuni mandhari ya kazi zao vizuri na wengine hukosea. Baada ya
kulifahamu hili tumeweza kupima ni kwa vipi Shafi Adamu Shafi anaweza kutumia
mandhari katika kujenga dhamira mbalimbali katika riwaya zake za Vuta N’kuvute
na Kuli.
Mlacha (1989) amechunguza matumizi ya lugha ya sitiari katika riwaya ya Rosa
Mistika ya Kezilahabi (1971). Anaeleza kwamba, katika riwaya hii Kezilahabi
amejenga dhamira mbalimbali kupitia matumizi ya lugha ya sitiari kurejelea mambo
kadhaa yenye kujenga dhamira. Kwa mfano, katika sehemu moja ya riwaya ya Rosa
Mistika anasema, “mwezi mkubwa ukimwangalia mlangoni.” Anafafanua sitiari hii
kuwa ina maana ya kwamba, wakati Rosa akifanya mambo yake ambayo ni kinyume
na maadili alidhani kwamba, hakuna mtu anayemuona lakini kumbe mambo yake
yalifahamika katika ulimwengu kwa sababu daima huwa hakuna siri. Hii ina maana
kwamba, mtu asije akafanya jambo baya akidhani kwamba halitafahamika katika
jamii kwa kuwa alipokuwa analifanya alikuwa peke yake. Mawazo ya Mlacha
(tumeshamtaja) tumeyachukua na tutayafanyia kazi katika utafiti wetu, hususani
38
tunapoangalia lengo mahususi la pili la utafiti wetu ili kuweza kuainisha sitiari
kadhaa zilizotumiwa na Shafi Adam Shafi katika riwaya zake za Kuli na Vuta
N’kuvute.
Mjema (1990) alihakiki riwaya ya Kusadikika na kuainisha vipengele mbalimbali
vya kifani vilivyotumiwa na mtunzi katika kuwasilisha dhamira kwa hadhira
iliyokusudiwa. Miongoni mwa vipengele vya matumizi ya lugha alivyoviainisha
katika makala yake ni kejeli, kebehi na mafumbo. Pia ameainisha vipengele vya
muundo, wahusika na mandhari iliyotumiwa na mwandishi katika Kusadikika.
Makala ya Mjema (ameshatajwa) kwa hakika imekuwa na mchango mkubwa katika
kusukuma mbele dhamira mbalimbali ambazo zinawasilishwa na mtunzi, vipengele
ambavyo sisi pia tumevichukuwa na kuvifanyia kazi katika utafiti wetu.
Hata hivyo, uhakiki uliofanywa na Mjema (ameshatajwa) umekuwa ni wa kudokeza
tu vipengele hivi pasipo kuvifanyia uchambuzi wa kina na kueleza ni kwa vipi
vinatumika katika kujenga dhamira mbalimbali zinazowasilishwa katika Kusadikika
na kuzihusisha na hali halisi ya maisha katika jamii. Katika utafiti wetu tumezama
kwa kina zaidi na kueleza vipengele vya kisanaa vinavyojitokeza katika riwaya
tulizoziteua kwamba vinawasilisha dhamira gani kwa jamii ambayo imekusudiwa.
Mulokozi (1990) katika makala yake “Utunzi wa Riwaya ya Kihistoria” katika
Mulika Namba 22, ameainisha mambo mbalimbali kuhusu riwaya. Miongoni mwa
mambo hayo ni wahusika wa riwaya ya kihistoria. Anaeleza kuwa, wahusika wa
riwaya ya Kihistoria wanaweza kugawanywa katika makundi mawili ambayo ni
wahusika ambao ni watu halisi waliopata kuishi na wahusika wa kubuni ambao
39
hawajapata kuishi katika ulimwengu huu ambao tunaufahamu. Mulokozi
(ameshatajwa) hakuishia kutaja aina za wahusika wa riwaya ya Kihistoria peke yake,
bali pia ametaja vipengele vingine kama vile usimulizi, mazungumzo ya wahusika,
na mtindo wa wahusika wa riwaya ya Kihistoria.
Hata hivyo, bado kuna vipengele kama vile mandhari ya riwaya ya Kihistoria
havikutajwa na Mulokozi (ameshatajwa). Kwa maoni yetu vipo vipengele vingine
vingi vya kifani na kimaudhui ambavyo havikutajwa na Mulokozi (ameshatajwa)
pengine kwa sababu haikuwa sehemu ya lengo lake kufanya hivyo na kwa hiyo
kuwaachia watafiti na wahakiki wanaokuja katika siku za usoni kama sisi. Kwa
ujumla maelezo haya tunakubaliana nayo kwa kiasi kikubwa na kwamba yanatoa
mchango muhimu katika kupeleka mbele utafiti wetu. Tunasema unapeleka mbele
utafiti wetu kwa sababu hata riwaya za Shafi Adam Shafi zinaingia katika kundi la
riwaya za kihistoria kwa sababu zinaeleza matukio mbalimbali ambayo kihistoria
yamepata kutokea na wahusika wake ni wa kihistoria kwa maana kwamba ni
wahusika wa kubuni ambao wanasifa zote za watu ambao wamepata kuishi katika
ulimwengu huu.
Khatibu (1986) aliandika makala yake kuhusu, “tamathali za semi za Kiswahili”
katika Mulika namba 18. Katika makala yake hiyo anaeleza tamathali mbalimbali za
usemi ambazo zinatumiwa katika fasihi ya Kiswahili huku akitolea mifano
mbalimbali kutoka katika riwaya ya Kiswahili hususani Nyota ya Rehema na
Utengano. Miongoni mwa riwaya tamathali za semi anazotaja ni tashibiha, sitiari,
tashihisi, chuku, tabaini, takriri, simango, kejeli, misemo, taashira, nasiha, tanakali
sauti na ritifaa.
40
Kwa hakika, tunakubaliana na uainishaji wa tamathali za semi unaofanywa na
Khatibu (ameshatajwa) kwamba alizotaja ni sehemu tu ya tamathali za usemi.
Kimsingi, tamathali za usemi ni nyingi mno na pengine ili kuweza kuzianisha zote
inatakiwa kufanyika utafiti wa kina ili kuzibaini katika kazi mbalimbali za fasihi
hususani zile zilizopo katika fasihi simulizi. Hata hivyo, baadhi ya tamathali za semi
zilizotajwa na Khatibu (ameshatajwa) tumezianisha katika utafiti wetu, hususani pale
tulipokuwa tunajibu swali la tatu la utafiti wetu.
Mohochi (2000) naye alichunguza usimulizi katika riwaya ya Nyongo Mkalia Ini
iliyoandikwa na Chimerah (1995) na kuainisha aina mbalimbali ya mbinu za
usimulizi zinazojitokeza katika riwaya hiyo. Anasema kwamba, mtunzi wa riwaya
hii ametumia aina tatu za usimuilizi ambazo ni usimulizi maizi, usimulizi wa nafsi ya
kwanza na usimulizi wa nafsi ya tatu. Uchanganyaji huu wa mbinu za usimulizi
katika riwaya hii unaifanya kuwa riwaya ambayo ni hai na yenye kuvuta usikivu wa
msomaji wake na kutoiweka chini pale tu atakapo anza kuisoma.
Maelezo haya yanafanana na yale ya Mohamed (1995) pale anaposema kwamba,
msomaji wa kazi ya fasihi atavutwa na usimulizi unaofanywa na mtunzi pale tu
mtunzi huyo anapokuwa mtaalamu wa kutumia mbinu za usimulizi kwa utaalamu wa
hali ya juu. Hii ina maana kuwa mtunzi asiyekuwa mtaalamu wa kutumia mbinu za
usimulizi anaweza kuuharibu usimulizi wake na wasomaji wakachukizwa badala ya
kufurahia usimulizi wa kazi husika.
Kuhusu mbinu za usimulizi zinazotajwa na Mohochi (ameshatajwa) ni muhimu sana
katika kuupeleka mbele utafiti huu kwa mantiki kwamba, hata Shafi Adam Shafi
41
naye anatumia mbinu hii katika uwasilishaji wake wa dhamira kwa hadhira
aliyoikusudia. Tumeyachukua mawazo haya na kuyafanyia kazi katika kulijibu swali
la tatu la utafiti wetu.
Hart (2003), kama anavyonukuliwa na Khamis (2007), alifanya uchambuzi juu ya
riwaya mpya ya Kiswahili kuhusu namna riwaya hiyo inavyosawiri hali halisi ya
maisha katika jamii. Anaeleza kwamba, riwaya mpya ya Kiswahili inasawiri maisha
kwa uhalisia wake kama yalivyo ila kwa kutumia vipengele vya kimazingaombwe.
Hii ina maana kwamba, riwaya ya Kiswahili imepiga hatua muhimu katika
maendeleo yake kwa kupata umbo jipya ambalo ni tofauti na umbo la riwaya za
awali ambazo hufuata umbo la kijadi katika utunzi wake. Riwaya mpya ya Kiswahili
imekuwa na muundo ambao unakiuka muundo wa kijadi kwa kuwa na wahusika
ambao ni wa ajabuajabu, mandhari tata isiyoeleweka kwa urahisi, muundo
usiojulikana mwanzo wala mwisho wake na kadhalika.
Maelezo haya yanatupatia mwanga wa kuielewa vizuri riwaya ya Kiswahili na
maendeleo yake na hivyo kuweza kuifahamu vizuri riwaya ya Shafi Adam Shafi
ambayo inafuata kanuni za kijadi katika utunzi wake. Riwaya ya kijadi ni ile ambayo
inakuwa na muundo ambayo si tata na ni rahisi kufuatiliwa na msomaji tangu
mwanzo mpaka mwisho wake. Pia, riwaya ya kijadi huwa na wahusika ambao ni wa
kawaida wasiokuwa wa ajabu ajabu, madhari yake ni halisia na wakati mwingine ni
dhahania lakini si tata kama ilivyo katika riwaya mpya. Shafi Adam Shafi ni
miongoni mwa watunzi ambao anaandika riwaya zake kwa kufuata muundo wa
kijadi. Hili tumelifahamu baada ya kupata ufafanuzi unaotofautisha riwaya mpya na
ile ya kijadi uliotolewa na Hart (ameshatajwa).
42
Mtaalamu mwingine anayezungumzia masuala ya fani katika riwaya ya Kiswahili ni
Khamis (2007) ambaye anasema kwamba, riwaya mpya ya Kiswahili imekuwa na
matumizi ya lugha ambayo inakiuka misingi ya kijadi ya matumizi ya lugha. Hii ina
maana kwamba, lugha inayotumika katika riwaya hizi ni ile ambayo inakiuka
misingi ya uhalisia unaosababishwa na mbinu ya utunzi wa kazi za fasihi
unaojulikana kama usasabaadaye. Katika kushadidia hoja yake juu yake anadondoa
katika Bina-Adamu riwaya ya Wamitila (2002:40) kuwa:
“Sikujua kama nilikuwa nikitembea kuelekea jana au kwenda kesho
au labda nilikuwa leo. Labda nilikuwa kote wakati mmoja…”
Kimsingi, tunapotazama matumizi ya lugha ya namna hii tunaona kwamba
yanakiuka kaida za matumizi ya lugha ya kijadi kwa kule kuonekana kuwa tata na
yenye kuleta ukinzani. Haiwezekani mtu akawa anatembea leo kuelekea jana kwa
sababu jana ni siku ambayo tayari imekwishapita. Haya ndiyo mambo ya
usasabaadaye ambayo ndiyo yanayozungumzwa na Khamis (ameshatajwa).
Mawazo haya ya Khamis (ameshatajwa) yanafanana na yale ya Gromova (2004)
kama anavyonukuliwa na Wamitila (2007) pale anapokariri kuwa riwaya hii mpya
inamatumizi ya lugha ya usasabaadaye na hivyo kuifanya kuwa tofauti kabisa na
riwaya za hapo awali ambazo matumizi yake ya lugha ni ya kijadi. Anashadidia hoja
yake kwa kudondoa katika Bina-Adamu ya Wamitila (2002:21) kuwa:
“Wakati wa safari yake ndefu, Mbabe, akisaidiwa na sauti ya ajabu
ya mwanamke mwenye sifa zisizo za kibinadamu anayeitwa Hanna,
anazuru Ulaya ambayo ‘inaishi jana’, Asia ya viwanda ambayo
‘inaishi kwa matumaini’ na Afrika, ambayo inaishi mwishoni mwa
kijiji cha utandawazi na imeharibiwa na njaa na vita.Anapokuwa
njiani kila pahala anakutana na mambo yanayoonekana hayana
mantiki, mambo ambayo hayaelezeki yanayofanywa na P.P mwenye
miujiza- Ulaya P.P ameushinda ufashisti, lakini bado unaishi imara
43
miongoni mwa wafuasi wake. Huko Asia ametupa bomu la Atomiki
Hiroshima. Afrika akitumia jiwe, amevigonga vichwa vya wanasiasa
kuvitoa akili…”
Maelezo haya ya Gromova (2004) na Khamis (2007) yanamsingi mkubwa katika
kutufahamisha namna ya kutazama au kuchambua matumizi ya lugha katika kazi ya
fasihi. Mara nyingi tumezoea kutazama matumizi ya lugha kwa kuangalia tamathali
za usemi zilizotumika katika kazi ya fasihi pamoja na mambo mengine lakini
hatuitazami lugha kwa namna ambayo wataalamu hawa wawili wanaitazama.
Kumbe, inawezekana kuchukua aya ya maneno katika riwaya na kuchunguza lugha
iliyotumika katika kifungu hicho kwa ujumla wake bila kurejelea kipengele
kimojakimoja kama vile, picha, ishara, taswira, sitiari na kadhalika. Tumeyachukuwa
mawazo haya na kuyatumia katika utafiti wetu ingawa kazi za riwaya za Shafi Adam
Shafi tunazozishughulikia hazipo katika kundi la riwaya zitumiazo lugha ya
kiusasabaadaye.
Wamitila (2007) aliandika juu ya muundo wa usimulizi na sitiari katika riwaya za
Nagona na Mzingile kama mbinu inayotumiwa sana katika kujenga dhamira na
maudhui ya riwaya mpya ya Kiswahili. Anaeleza kuwa, matumizi ya sitiari za
miujiza katika riwaya kama vile Nagona na Mzingile ni jambo la kawaida mno. Kwa
mfano, utaona sitiari mbalimbali kama vile mtoto anamwelekeza mama yake namna
ya kumzaa au mtoto anazaliwa na kuanza kuzungumza na kuelekeza mambo
mbalimbali yanayofanyika.
Katika ulimwengu wa uhalisia, matukio kama haya hayawezi kutokea lakini mtunzi
anayatumia kwa nia ya kuwasilisha dhamira mbalimbali katika jamii. Kwa mfano,
44
moja ya dhamira inayoweza kuwa inawasilishwa kupitia sitiari za namna hii ni
ugumu wa maisha ambao unaikumba jamii ya leo kiasi kwamba, hata mtoto mdogo
anapozaliwa tu, tayari ameshaanza kuufahamu ugumu huo na ameanza kupambana
na maisha hayo.
Maelezo ya Wamitila (2007) yametufahamisha jambo moja muhimu sana katika
tasinia ya fasihi, na hususani matumizi ya lugha. Jambo hilo si jingine bali ni uwepo
wa sitiari za kimiujiza katika kazi za fasihi hali ya kuwa sisi tulikwishazoea kuona
sitiari halisia peke yake na tukafahamu kwamba, hizo ndizo pekee zinazounda sitiari
katika kazi za fasihi. Mawazo haya yamekuza maarifa yetu ya uhakiki wa mbinu za
kisanaa katika kazi za fasihi na popote tutakapokutana na matumizi ya mbinu hizi,
basi itakuwa kazi rahisi kabisa kuzifafanua na kuainisha dhamira mbalimbali
zinazojengwa kutokana na sitiari hizo.
Pia, Wamitila (2008) anataja vipengele mbalimbali ambavyo mhakiki anaweza
kuvitumia katika uhakiki wa kazi ya riwaya ambayo atakuwa anaihakiki. Vipengele
vya kifani anavyovitaja kuwa ni sehemu muhimu katika uhakiki wa kazi za riwaya ni
wahusika, mandhari, muundo, mtindo, usimulizi na matumizi ya lugha. Uainishaji
huu wa vipengele vya kifani hautofautiani sana na ule unaofanywa na watunzi
wengine kama Njogu na Chimerah (1999). Uainishaji huu wa vipengele vya kifani
tunakubaliana nao na kwamba baadhi ya vipengele hivi ndivyo tulivyovitumia katika
kutimiza malengo mahususi ya utafiti wetu.
Hata hivyo, Wamitila (ameshatajwa) hakufanya uchambuzi wa kina kwa kila
kipengele na namna kinavyojitokeza katika kazi za riwaya pengine kwa sababu
45
haikuwa sehemu ya madhumuni yake mahususi. Katika utafiti wetu tumefanya
uchambuzi wa kina juu ya vipengele vya kifani ambavyo tumevianisha katika utafiti
wetu kwa nia ya kutimiza madhumuni mahususi ya utafiti wetu.
Vilevile, Walibora (2010) aliandika juu ya istilahi ya “Uhalisiamazingaombwe”
kama inavyojitokeza katika riwaya mpya za Nagona (1990), Mzingile (1991), Bina
Adamu (2002) na Babu Alipofufuka (2001) na Duniya Yao (2006). Anasema
kwamba, miongoni mwa watunzi wa riwaya ya Kiswahili ambao wanaandika riwaya
zao kwa mtindo huu ni Said Ahmed Mohamed pale alipoandika riwaya yake ya
Dunia Yao (2006). Anasema:
“Hata hivyo, hapana shaka kwamba Dunia Yao (2006) ambayo ni
riwaya ya kiuhalisiamazingaombwe ni sehemu ya mabadiliko
makubwa katika mkabala wa mkondo wa kisanii wa mwandishi huyu
unaojidhihirisha vilevile katika kazi zake nyingi za mwongo huu wa
kuanzia mwaka 2000, hasa katia Babu Alipofufuka (2001), na pia
kwenye baadhi ya hadithi zake kwenye Arusi ya Buldoza”.
Riwaya hizi mpya huandikwa kwa kutumia mtindo wa kiuhalisia mazingaombwe
kama njia pekee ya kuwafanya wasomaji wajifunze kufikiri ili waweze kupata
dhamira mbalimbali zinazoelezwa katika riwaya hizo. Mawazo haya yanatoa
mchango mkubwa sana katika kupeleka mbele utafiti wetu kwa kule kutufahamisha
kwamba, msomaji wa riwaya mpya anatakiwa asome kwa kutafakari sana
yanayosemwa katika riwaya husika ili aweze kupata dhamira iliyokusudiwa na
mwandishi.
Jambo hili tunaliona kuwa linawapasa hata wasomaji wa riwaya za kijadi kama vile
Vuta N’kuvute na Kuli za Shafi Adam Shafi ambazo tunazishughulikia katika utafiti
wetu. Mtaalamu mwingine ambaye ameshughulikia kipengele cha fani katika ngazi
46
ya uhakiki ni Mrikaria (2010) aliposhughulikia kipengele cha kejeli katika fasihi ya
Kiswahili. Katika kazi yake ametazama kazi mbalimbali za fasihi, riwaya ikiwemo,
akitazama kejeli mbalimbali zinazojengwa na waandishi wa fasihi ya Kiswahili juu
ya mambo mbalimbali.
Kwa mfano, anasema kwamba, jina la kitabu Miradi Bubu ya Wazalendo ni kejeli
tosha kwa watunga sera ambao ndio waletao miradi mbalimbali ya maendeleo kwa
jamii pamoja na kuitekeleza miradi hiyo. “Bubu” katika hali ya kawaida ni neno
linalotumika kumrejelea mtu mwenye ulemavu wa kuzungumza, kusoma na pengine
kusikia. Hivyo basi, kuiita miradi ya maendeleo kuwa ni bubu maana yake ni kuwa
miradi hiyo haitekelezeki na wala haiwezi kuleta tija na maendeleo kwa jamii. Hii ni
kejeli kubwa dhidi ya viongozi ambao wanaanzisha miradi mbalimbali ya maendeleo
na kisha wanahujumu miradi hiyo kwa kufanya wizi, rushwa na kujilimbikizia mali
kutokana na miradi hiyohiyo ambayo ilipaswa kuwafaa wananchi.
Mawazo haya ni muhimu katika kusukuma mbele utafiti wetu kwa kuwa umetutajia
moja kati ya kipengele cha kisanaa kinachotumiwa na watunzi wa kazi za fasihi
katika ujengaji wa dhamira za kazi zao. Nasi pia tumetumia kipengele hiki katika
kujibu swali la tatu la utafiti wetu. Hata hivyo, utafiti wa Mrikaria (tumeshamtaja)
umeshughulikia kejeli katika tanzu mbalimbali za fasihi andishi pasipo kuzamia
katika utanzu mmoja na kuchunguza kipengele hicho kwa kina.
Katika utafiti wetu tumetumia riwaya mbili za Shafi Adam Shafi za Vuta N’kuvute na
Kuli kuchunguza matumizi ya kejeli kama kipengele kimojawapo katika vipengele
vya lugha ya kitamathali. Naye Hawthorn (1985) anaeleza aina tatu za usimulizi
47
ambazo hutumiwa na watunzi wa kazi za riwaya kama mbinu ya kujenga dhamira
mbalimbali katika kazi zao. Anasema kwamba, watunzi wa riwaya hutumia usimulizi
maizi, usimulizi wa nafsi ya kwanza na usimulizi wa nafsi ya tatu katika uwasilishaji
wa dhamira mbalimbali katika kazi zao. Anaendelea kueleza kwamba, usimulizi
maizi ndio mbinu ambayo inatumiwa kwa kiasi kikubwa na watunzi wengi wa
riwaya kuliko usimulizi wa nafsi ya kwanza na usimulizi wa nafsi ya tatu.
Maelezo ya Hawthorn (ameshatajwa), yametufahamisha aina tatu kuu za usimulizi
ambazo hutumiwa na watunzi wa kazi za riwaya katika kujenga dhamira ambazo
kwazo zimekuwa muhimili muhimu katika kusaidia kukamilisha lengo mahususi la
tatu katika utafiti wetu. Katika harakati za kukamilisha malengo mahususi ya utafiti
wetu, tumeeleza aina mbalimbali za usimulizi zinazotumiwa na mwandishi huku
tukirejelea dhima ya kila aina katika ujengaji wa dhamira mbalimbali ndani ya kazi
husika.
Wanyonyi (2011) alifanya uhakiki wa riwaya ya Nyunso za Mwanamke iliyoandikwa
na Said Ahmed Mohamed kwa kutumia mtazamo wa Saikolojia Changanuzi. Katika
uhakiki wake, ameeleza mambo mengi miongoni mwa hayo ni kwamba, mtunzi
amesawiri vizuri wahusika wake kwa kutumia Saikolojia Changanuzi ambapo
anatuonesha kuwa mwanamke ni kiumbe anayekutana na matatizo mbalimbali katika
jamii kiasi kwamba, matatizo haya yanaweza kuhatarisha maisha yake.
Hata hivyo, mwanamke anaonekana kupambana na matatizo haya ambayo
yanamkabili na kufanikiwa. Mawazo haya yametufungua katika kufahamu namna ya
kuwachunguza wahusika katika kazi za fasihi kwa namna ya Saikolojia Changanuzi.
48
Mhusika Yasmini ni miongoni mwa wahusika ambao wanaweza kuchanganuliwa
vizuri kwa kutumia nadharia ya Saikolojia Changanuzi ili kumfahamu vizuri na kisha
kuzifahamu pia dhamira anazoziwasilisha katika jamii. Tumelichukua wazo na ujuzi
huu na kuutumia katika kukamilisha utafiti wetu hususani katika kujibu swali la
kwanza na tatu la utafi wetu.
2.7 Muhtasari
Katika sehemu hii tumepitia kazi tangulizi ambazo zimehakiki na kutafiti vipengele
vya kifani katika riwaya ya Kiswahili.Vipengele vya kifani ambavyo
vimeshughulikiwa na watafiti watangulizi ni vile vya matumizi ya lugha, mandhari,
muundo, mtindo, na wahusika. Tafiti tangulizi hizi zimekuwa muhimili mkubwa
katika kukuza maarifa na uelewa wetu juu ya vipengele vya kifani kama
vinavyotumiwa na kujitokeza katika riwaya za Kiswahili. Maarifa tuliyoyapata
kutoka katika kupitia kazi tangulizi tumeyachukua na kuyafanyia kazi katika uhakiki
na kuchambua riwaya za Kuli na Vuta N’kuvute za Shafi Adam Shafi.
2.8 Kazi Tangulizi Juu ya Riwaya za Shafi Adam Shafi
Katika sehemu hii tunapitia kazi tangulizi juu ya riwaya za Shafi Adam Shafi ili
kubaini watafiti na wahakiki watangulizi wamezungumza nini kuhusu kazi hizo na
kisha kubainisha pengo la kiutafiti ambalo linahitaji kujazwa na utafiti huu
tulioufanya. Kimsingi, wapo watafiti na wahakiki kadhaa ambao wamechunguza na
kueleza juu ya kazi za Shafi Adam Shafi kwa namna mbalimbali kulingana na
madhumuni ya kazi zao. Khatibu (1983) alifanya uhakiki wa riwaya ya Kuli na
kueleza kuwa dhamira kuu katika riwaya hiyo ni ukombozi wa kitabaka. Ukombozi
huu ulikuwa unafanywa na watu wa tabaka la chini dhidi ya tabaka la juu kuhusu
49
mgawanyo sawa na sahihi wa rasilimali za taifa. Mhakiki anaeleza kwamba, serikali
ya kikoloni iliwatesa na kuwatumikisha wananchi wa Zanzibar kwa masilahi mapana
ya Wakoloni huku wananchi wakiishia kuwa katika maisha duni kabisa.
Khatibu (ameshatajwa) hakuchambua kwa kina juu ya dhamira za riwaya hii na
badala yake ameishia kutaja tu na kueleza kwa ufupi. Hata hivyo, maelezo yake
kuwa, “ukombozi ulikuwa unafanywa na watu wa tabaka la chini kuwashusha watu
wa tabaka la juu”, yamekuwa na umuhimu mkubwa katika kutufahamisha ni ipi
dhamira kuu katika riwaya ya Kuli na kutuwia rahisi sisi kufanya uchambuzi wa kina
kuhusu dhamira hii katika riwaya husika.
Mulokozi (1990) aliandika makala juu ya utunzi wa riwaya ya Kihistoria ya
Kiswahili na kueleza mambo mbalimbali ya kifani na kimaudhui yanayoipamba
riwaya hiyo. Katika harakati zake za kukamilisha lengo hili alimtaja Shafi Adam
Shafi kuwa ni miongoni mwa waandishi ambao anatunga riwaya ya Kihistoria.
Amelisema hili kwa kutolea mfano kuwa ujenzi wa wahusika katika riwaya za
mtunzi huyu zinaashiria kwamba, yeye ni mtunzi wa riwaya za Kihistoria.
Kimsingi, mfano unaotolewa na Mulokozi (ameshatajwa) tunakubaliana nao kwani
hauna shaka kuwa riwaya karibu zote za mtunzi huyu zimendikwa katika muktadha
wa Kihistoria. Kwa mantiki hiyo, mafunzo tuliyoyapata katika makala ya Mulokozi
yametufungua macho ya kuzielewa vizuri riwaya za Shafi Adam Shafi kuwa ni za
Kihistoria na pale tunapozichambua tunalizingatia hili. Hata hivyo, maelezo ya
Mulokozi ni ya kiudokezi tu na hajazama katika kina kirefu cha uhakiki wa riwaya
hizo. Utafiti huu umefanywa kwa kuzama ndani zaidi na kuchambua mambo
50
mbalimbali katika riwaya za Vuta N’kuvute na Kuli za Shafi Adam Shafi. Njogu na
Chimerah (1999) waliandika kitabu ambacho walikiita Ufundishaji wa Fasihi
Nadharia na Mbinu ambacho kimesheheni hazina kubwa ya masuala ya fasihi ya
Kiswahili na ile ya makabila mengine ya Kiafrika.
Katika kitabu hiki wametoa darasa la kutosha kwa walimu, wahadhiri na wote
wanaohusika na ufundishaji wa fasihi juu ya namna bora ya kufundisha kazi za fasihi
katika ngazi hizo wanazofundisha. Kwa mfano, kila kipengele kiwe ni cha kifani au
kimaudhui kimeelezwa vile kinavyopaswa kufundishwa darasani ili wanafunzi
waweze kuelewa. Katika kutoa mifano mbalimbali ya kukamilisha hoja zao,
wamekuwa wakitolea mifano riwaya za Shafi Adam Shafi hususani Kasiri ya Mwinyi
Fuadi na Kuli. Mifano hiyo imekuwa ikihusu vipengele vya kifani na kimaudhui.
Kimsingi, maelekezo ya ufundishaji wa fasihi darasani yanayotolewa na wawili hawa
yamekuwa na umuhimu mkubwa katika kupeleka mbele utafiti wetu. Mawazo yao
yametusaidia sana katika kufanikisha uchambuzi na uhakiki tulioufanya katika sura
ya tano ya tasinifu hii. Mtaalamu mwingine aliyeandika kuhusu riwaya za Shafi
Adam Shafi ni Wamitila (2002) ambapo alieleza kuwa Shafi Adam Shafi ni
mtaalamu sana katika matumizi ya mbinu ya kueleza sifa za wahusika wake pamoja
na wasifu wao. Anaeleza kwamba, mbinu hii ni nzuri sana kwa sababu humfanya
msomaji kuwaelewa vizuri wahusika wa riwaya hizo na kisha kuweza kuhusisha
vyema matendo yao na wasifu wao. Hili linapotokea inakuwa ni rahisi sana kwa
msomaji kuipata dhamira iliyokusudiwa na mwandishi. Katika kusisitiza hoja yake,
Wamitila (ameshatajwa) anatolea mfano namna Shafi Adam Shafi anavyompamba
Yasmini kwa sifa mbalimbali za uzuri kwa kutaja wasifu wake ambao unapatikana
51
katika ukurasa wa kwanza wa riwaya ya Vuta N’kuvute. Kwa hakika maelezo ya
Wamitila (2002) yamekuwa na mchango thabiti wa kupeleka mbele utafiti wetu kwa
kule kutufahamisha kwamba, kumbe kumtaja mhusika na kumpamba kwa sifa zake
ni mbinu ya kisanaa ya mtunzi kuwasilisha dhamira mbalimbali kwa hadhira yake.
Mbinu hii tumeona kwamba ni muhimu nasi tukaieleza na kuifafanua kwa kina kama
inavyojitokeza katika riwaya husika kama sehemu ya kukamilisha dhumuni
mahususi la tatu la utafiti wetu. Tofauti na alivyoeleza Wamitila (ameshatajwa) kwa
kugusia tu mbinu hii, sisi tumeitafiti na kuitolea maelezo ya kutosha kabisa kiasi cha
kumfanya msomaji kuielewa kwa undani zaidi.
Pia, Wamitila (2008) aliandika kitabu adhimu katika taaluma ya fasihi na kukipa jina
la Kazi ya Fasihi. Katika kitabu hiki amehudhurisha vipengele mbalimbali ambavyo
vinajenga kazi mbalimbali za fasihi na namna ya kuvichambua au kuvihakiki
vipengele hivyo kitaaluma. Vilevele, ametaja na kutoa ufafanuzi kuhusu mbinu
mbalimbali za usomaji wa kazi za fasihi ili kuwawezesha wasomaji kupata yale
wanayoyahitaji kama wanavyoyahitaji kutoka katika kazi mbalimbali za fasihi
ambazo watazisoma kwa makusudio mbalimbali. Kazi hii ya Wamitila
(ameshatajwa) ni muhimu sana katika kupeleka mbele utafiti huu wetu ambao
umechunguza dhamira na vipengele vya kifani katika riwaya za Kuli na Vuta
N’kuvute.
Maelezo ya mtaalamu huyu yametusaidia kufahamu namna ya kuzipata dhamira
katika kazi za riwaya pamoja na namna ya kutambua vipengele mbalimbali vya
kisanaa vinavyotumiwa na watunzi wa kazi za fasihi katika kuwasilisha ujumbe
52
uliokusudiwa kwa hadhira iliyokusudiwa. Tunasema hivi kwa sababu katika kutoa
mifano ya kuthibitisha mawazo yake Wamitila (2008) amekuwa akirejelea hapa na
pale riwaya za Shafi Adam Shafi hususani Kasiri ya Mwinyi Fuad, Kuli, Vuta
N’kuvute na Haini. Kutokana na kuzitaja riwaya hizi na kuonesha namna mbinu
mbalimbali za kisanaa zinavyojitokeza imekuwa ni rahisi kwetu kuzipata mbinu hizo
na kisha kufanyia uchambuzi wa kina tofauti na yeye alivyofanya katika kitabu
chake.
Diegner (2011) alifanya mazungumzo na Shafi Adam Shafi kuhusu uandishi wake
wa riwaya tangu alipoanza mpaka hapa alipofikia. Katika mazungumzo yao
alimuuliza maswali mengi kuhusu mambo yaliyomsukuma mpaka akaandika riwaya
alizoziandika. Bila choyo Shafi Adam Shafi amejibu maswali aliyoulizwa kwa ustadi
mkubwa kiasi cha kumwezesha msomaji au mtafiti kupata mambo mengi kuhusu
utunzi wa riwaya uliofanywa na Shafi Adam Shafi.
Kwa mfano, aliulizwa swali kwamba, anauelezeaje utunzi wa Kuli na ule wa Vuta
N’kuvute? Jibu alilolitoa ni kwamba, Kuli ndiyo riwaya yake ya kwanza kupata
kuitunga kwa hivyo hakuwa ameiva katika sanaa ya utunzi wa riwaya hali ya kuwa
alipotunga Vuta N’kuvute alikuwa ameiva kiasi na hivyo kutoa riwaya imara
iliyopata tuzo ya uandishi bora nchini Tanzania.
Kimsingi, mazungumzo baina ya Diegner (ameshatajwa) na Shafi Adam Shafi ni
muhimu sana katika kupeleka mbele utafiti wetu kwa namna mbalimbali. Kwanza,
kupitia mazungumzo haya tumepata data za kutosha kumuhusu mwandishi na hivyo
kutokuwa na haja ya kufanya mahojiano na mtunzi wa riwaya tulizoshughulikia kwa
53
sababu kila tulichokihitaji tumekipata. Hivyo basi, muda ambao tulikuwa tuutumie
kufanya mahojiano na mtunzi tuliutumia kufanya jambo jingine na hivyo kuweza
kukamilisha lengo letu kuu la utafiti huu kwa muda muafaka.
Pili, mazungumzo ya Shafi Adam Shafi na Diegner (ameshatajwa) yamesaidia sana
kupata data na kukazia au kukamilisha zile ambazo tumezipata kwa kudondoa katika
riwaya husika na hivyo kujibu maswali yetu ya utafiti kwa uhakika na ufasaha zaidi.
Jambo hili pia linaufanya utafiti wetu kuonekana kuwa ni hai kutokana na kuwepo
kwa maelezo dhahiri ya mtunzi wa riwaya tulizozishughulikia na hivyo kumfanya
msomaji kuamini uchambuzi wa data tulioufanya katika tasinifu hii.
Upatanisho wa kile kinachosemwa na mwandishi katika riwaya yake na kauli zake
halisi kuhusiana na riwaya zake ni kitu muhimu sana katika kuuchambulisha utafiti
husika na kuufanya utafiti wowote ule wa kitaaluma kuaminiwa na wanataaluma
pamoja na wasomaji wengine wote kwa ujumla wao. Kwa hakika, mazungumzo
baina ya watu hawa wawili yamekuwa na umuhimu mkubwa sana katika
kukamilisha utafiti huu kama unavyoonekana hivi sasa.
Si hivyo tu bali pia Walibora (2013) ameandika makala kuhusu riwaya mpya ya
tawasifu iliyoandikwa na Shafi Adam Shafi juu ya maisha yake. Pamoja na mambo
mengi aliyoyaeleza, kubwa ni kumsifu Shafi Adam Shafi kuwa ni miongoni mwa
watunzi wajasiri ambao ameweza kueleza mambo mbalimbali, waziwazi yanayohusu
maisha yake bila kificho. Anasema kwamba, si jambo la kawaida kwa mwandishi wa
kazi ya fasihi inayomuhusu yeye mwenyewe na kisha akataja mambo ambayo kwa
mtazamo wa wengi yanaweza kuwa yanamuaibisha mbele za wasomaji wake. Shafi
54
Adam Shafi, ametaja mambo hayo bila woga wowote na hivyo kumfananisha na
Shaaban Robert alipoandika Wasifu wa Siti Binti Saad na tawasifu ya maisha yake
iliyoitwa Maisha Yangu na Baada ya Miaka Hamsini.
Mawazo haya yanamchango mkubwa katika kupeleka mbele utafiti wetu hususani
katika kujibu maswali matatu ya utafiti wetu. Kwanza, suala la mwandishi kutunga
riwaya ya tawasifu na kisha kueleza kila kitu hadharani limetufundisha jambo.
Kumbe katika kipindi hiki cha utandawazi ambapo mambo huelezwa waziwazi
kimefika mpaka katika riwaya ya Kiswahili, jambo linalodhihirisha kwamba, riwaya
inasawiri hali halisi ya maisha katika jamii.
Hata hivyo, kwa maoni yetu tunaona kwamba, si sahihi kwa kazi ya fasihi kueleza
kila jambo kwa uwazi kwa sababu si kila jambo linapaswa kuanikwa mbele za watu.
Kwa mfano, suala la Shafi Kueleza kwamba, alikuwa na mahusiano ya kimapenzi na
wanawake kadhaa huko Sudan wakati wa ujana wake halikupaswa kutokea katika
riwaya yake hiyo ya Tawasifu inayoitwa Mbali na Nyumbani. Hakuna asiyefahamu
kwamba, kijana anapobaleghe huwa anakuwa katika hali gani na kwa vyovyote vile
atatafuta njia ya kujihifadhi.
Kama hivyo ndivyo, haikuwa na haja yeye kusema waziwazi mambo hayo kwa
sababu inakuwa ni kama vile anahamasisha watu kufanya uasherati kwa kule
kuonesha kwamba, hicho ni kitu cha kawaida tu. Kwa mantiki hiyo, katika utafiti
wetu tumekuwa makini katika matumizi ya lugha ya uhakiki tuliofanya ili isije
ikatokea tumetumia lugha ambayo si stahiki katika muktadha huu wa kitaaluma.
55
2.9 Mkabala wa Kinadhari
Katika sehemu hii tumewasilisha nadharia tatu ambazo tumezitumia katika
uchambuzi na uwasilishaji wa data za utafiti. Nadharia tulizotumia ni Simiotiki,
Dhima na Kazi na Saikolojia Changanuzi.
2.9.1 Nadharia ya Simiotiki
Nazarova (1996) anaeleza kuwa Simiotiki ni natharia inayohusu taaluma ya mfumo
wa alama katika mawasiliano ya kutumia lugha. Ni mfumo kwa sababu ili kitu kiwe
ni alama ni lazima kitu hicho kisimame badala ya kitu maalumu au halisia
kinachorejelewa na alama hiyo. Pili, ni lazima alama hiyo iwe imekubaliwa na
wanajamii wote isimame kama kiwakilishi cha kitu au jambo fulani (Eco, 1976).
Hivyo, tunakubaliana na maelezo haya kuwa, Simiotiki ni taaluma ya mfumo wa
matumizi ya alama au ishara kwa nia ya kuwasiliana kati ya wanajamii na kuelewana
baina yao (Cobley, 2001).
Wamitila (2002) anafafanua kuwa, Simiotiki ni neno la Kiyunani lenye maana ya
ishara na ambalo linatumiwa kuelezea mielekeo na makundi fulani ya kihakiki.
Makundi hayo na mielekeo hiyo imezuka na mtindo wa kuhakiki kazi za kifasihi
ambao unaangaza ishara za kifasihi katika kazi hizo. Nadharia hii kwa ujumla
inajishughulisha na ishara na uashiriaji katika kazi za fasihi. Ishara zinazojitokeza
katika kazi za fasihi huundwa na mtunzi kwa kuzingatia muktadha wa jamii wa
kiuchumi, kisiasa, kijamii na kiutamaduni.
Chandler (1992) anaeleza kwamba, binadamu ni mtengenezaji na mnyambulishaji
wa alama hizo. Wasomaji na watazamaji wa kazi za fasihi hutengeneza maana
56
mbalimbali kupitia ubunifu na tafsiri zao juu ya alama hizo. Mawazo haya
yanafanana na yale ya Chandler (1992) aliposema kuwa, wanadamu hufikiri kwa
kutumia alama. Alama hizo zinakuwa katika mfumo wa maneno, picha, sauti, harufu,
ladha, matendo na mtenda. Anaendelea kueleza kwamba, kitu chochote kitakuwa
alama, kama watu watakifasiri kama kirejelee, yaani kinasimama kwa niaba ya kitu
kingine badala ya chenyewe.
Mark (1995) anaeleza kuwa, watunzi wa kazi za fasihi hutumia lugha ya picha na
ishara kwa kutumia alama ambazo zinafahamika kwa urahisi na wanajamii
wanaoandikiwa kazi hiyo ya fasihi. Kwa mfano, watunzi wa kazi za fasihi huweza
kutumia wanyama, wadudu, miti, mizimu, mashetani, na mawe kurejelea matendo na
tabia za mwanadamu kwa nia ya kufunza jamii masuala muhimu katika maisha.
Wamitila (2002) anaeleza kwamba, katika lugha kuna vitu viwili, ambavyo ni kitaja
(a signifier), yaani; umbo ambalo alama inachukua na kirejelee (a signified), yaani
maana iwakilishwayo na alama hiyo. Kutokana na maelezo haya tunapata uelewa
kuwa, kuna kitaja na kirejelee ambapo mahusiano ya viwili hivyo ni ya kubuni tu,
hutegemea utamaduni wa jamii husika. Inawezekana kabisa ikawa hakuna uhusiano
kati ya kitaja na kirejelee, lakini kama wanajamii wamekubaliana juu ya matumizi
yake, basi hutumika na huelewana miongoni mwao.
Kwa mfano, hakuna uhusiano wa moja kwa moja kati ya neno ng’ombe na mnyama
mwenyewe. Jina hili ni la kubuni na likakubalika kutumika katika jamii. Tunasema
ni la kubuni kwa sababu kila jamii ina jina tofauti la kumuita mnyama huyo ambaye
kwa Waswahili hufahamika kwa jina la ng’ombe. Sasa, mnyama ng’ombe
57
anapotumiwa katika kazi ya fasihi hujenga ishara, picha na taswira tofautitafauti
kulingana na uelewa na uzoefu wa msomaji kumhusu mnyama huyo.
Barthes (1994) anaeleza kwamba, kuna aina tano za misimbo zinazotumika katika
kazi za fasihi ambazo kwa pamoja huunda nadharia ya Simiotiki. Aina hizo ni
msimbo wa Kimatukio, Kihemenitiki, Kiseme, Kiishara na Kiutamaduni.
Tunaposoma kazi za fasihi tunakutana na matumizi ya lugha ambayo yanajenga
misimbo ya aina hizo tano. Kwa mfano, msimbo wa kimatukio hujitokeza, kwa
mtunzi wa kazi ya fasihi kujenga tukio linalofanywa na wanyama kama vile, mbwa,
fisi, paka na ng’ombe ambapo kwa msomaji huweza kujenga taswira, ishara na picha
ambazo zitampatia dhamira stahiki.
Shafi Adam Shafi, kama ilivyo kwa baadhi ya waandishi wengine anatunga riwaya
zake kwa kutumia lugha ya picha, ishara, mafumbo, sitiari, na taswira kali. Nadharia
ya Simiotiki imetoa mwongozo muafaka katika kuzichambua aina zote hizo za
matumizi ya lugha na kisha kuwezesha kufanikisha madhumuni ya utafiti huu.
Hivyo, nadharia hii imetumika kwa kiasi kikubwa, katika kukamilisha lengo
mahususi la tatu la utafiti huu lililolenga kubainisha mbinu za kisanaa zilizotumiwa
na Shafi Adam Shafi katika kujenga dhamira za riwaya zake. Nadharia nyingine ni
ile ya Dhima na kazi inayoelezwa katika sehemu ifuatayo.
2.9.2 Nadharia ya Dhima na Kazi
Nadharia ya Dhima na Kazi imeasisiwa na Sengo (2009). Nadharia hii inazichambua
kazi za fasihi kwa kuangalia kazi na dhima kwa kila kipengele cha fasihi.
Mwanafalsafa huyu anaendelea kueleza kwamba, kila kitu katika kazi ya fasihi
58
kimetumiwa kwa dhima maalumu katika kazi husika. Kwa mfano, hata waandishi
wanapoteua majina ya vitabu vyao hufanya hivyo kwa madhumuni mahususi.
Mawazo haya tunakubaliana nayo na kwamba yanasukuma mbele utafiti wetu.
Yanasukuma mbele utafiti huu kwa sababu ili kuweza kubainisha dhamira
mbalimbali katika riwaya za Kuli na Vuta N’kuvute ni lazima tuchunguze matumizi
ya vipengele mbalimbali vya kifani katika riwaya tulizoziteua kwa sababu
vimetumiwa kwa madhumuni mahususi ya kujenga dhamira mbalimbali. Kwa
mfano, Kuli ambalo ni jina la kitabu limetumiwa kwa dhima maalumu ambayo
tukiichunguza vizuri tunaweza kuelewa mambo mengi ambayo yanahusiana na
dhamira zinazopatikana katika riwaya husika.
2.9.3 Nadharia ya Saikolojia Changanuzi
Nadharia ya Saikolojia Changanuzi iliasisiwa na mtaalamu mwenye asili ya
Australia aliyefahamika kwa jina la Sigmund Freud. Mwanataaluma huyu alitumia
neno “Psychoanalysis” kwa mara ya kwanza katika mwaka wa 1896 (Wamitila,
2002a). Freud (1896) anaeleza kuwa, binadamu huongozwa na mambo makuu
matatu, ambayo ni mahitaji, matamanio na wasiwasi katika maisha. Mahitaji
hurejelea mambo muhimu kama chakula, malazi na mavazi ambayo humwezesha
mwanadamu kuishi vizuri. Matamanio, hurejelea dhana ya starehe hususani za
kingono. Wasiwasi ni hofu na mashaka juu ya maisha, kwamba, nitafanikiwa au
sitafanikiwa katika maisha (Wamitila, 2002a).
Sigmund Freud (1896) kama anavyonukuliwa na Wamitila (2002a) anaeleza kuwa,
kati ya mambo matatu makuu ambayo huongoza maisha ya mwanadamu ni lile la
matamanio ndiyo hutawala zaidi. Matanio huchukua nafasi kubwa katika maisha ya
59
mwanadamu na hivyo kila mwanadamu hufanya jitihada kubwa kuhakikisha
anatimiza matamanio yake. Katika harakati za kuhakisha kwamba, anatimiza
matamanio yake, huumiza watu wengine wasiokuwa na hatia. Kwa mfano, Bwana
Raza, alipomuoa Yasmini, alisukumwa na matamanio na si kitu kingine. Tunasema
haya kwa sababu katika hali ya kawaida hatutegemei mzee wa miaka hamsini na
ushee kumuoa binti wa miaka kumi na mitano. Hata hivyo, kwa kumuoa Yasmini,
aliathiri Saikolojia ya binti huyu kiasi cha kutotambua nini cha kufanya, na ndipo
alipoamua kumkimbia bwana huyo.
Sigmund Freud (1896) anaeleza kwamba matanio yamekuwa ni kitu muhimu kwa
binadamu kwa sababu tangu mwanadamu huyu anapozaliwa tu, anaanza kupata raha
ya kujamiiana kwa kunyonya kwa mama yake. Anaeleza kwamba, chuchu za mama
huwa ni kama uume na mdomo wa mtoto ni uke. Kwa hiyo mtoto anaponyonya kwa
mama yake anapata raha ya kijinsia. Hivyo, basi mtoto anavyoendelea kukua hitajio
la kujamiiana nalo linakuwa kubwa zaidi na hufanya kila njia kuhakikisha kwamba,
anatimiza hitajio hilo.
Kimsingi, nadharia ya Saikolojia Changanuzi tumeitumia kwa kiasi kikubwa
kuhakiki mikasa na matatizo yaliyompata Yasmini. Kwa muono wetu, matatizo hayo
yalisababishwa na matamanio ya Bwana Raza kukidhi haja zake za kijinsia kwa
kuwa na msichana mzuri kama Yasmini. Kwa upande mwingine Yasmini, Kutoroka
kwa mumewe kwa sababu hakumpenda na hivyo alihitaji kuwa na mahusiano na
kijana mwenzake. Yote haya kwa pamoja yamechangia mno matatizo yaliyomkumba
Yasmini na kwa hivyo, tukaona ni vyema tutumie nadharia ya Saikolojia Changanuzi
kuchambua dhamira katika riwaya teule.
60
2.10 Muhtasari
Utafiti na uhakiki juu ya riwaya za Shafi Adam Shafi haujafanywa vya kutosha
katika viwango mbalimbali kama vile uandishi wa makala na tasinifu za shahada za
awali, uzamili na uzamivu. Wataalamu wote ambao tumesoma kazi zao wamekuwa
wakigusagusa tu vipengele vya kifani na kimaudhui vya riwaya hii bila kufanya
uhakiki wa kina. Hii ilitokana na malengo yao kuwa tofauti na hili la kuchambua
riwaya hizo kwa kina na kuishia kufanya mdokezo tu wa riwaya za Shafi Adam
Shafi ili kuweza kukamilisha malengo yao. Hali hii inaonesha kuwa, ipo haja ya
msingi ya kufanya utafiti wa kina kuhusu riwaya za Shafi Adam Shafi katika ngazi
hii ya Uzamivu ili kufahamu dhamira na mbinu za kisanaa zinazotumika kuwasilisha
dhamira hizo kwa jamii iliyokusudiwa. Hii kwa hakika ndiyo sababu ya msingi
iliyotuhamasisha kufanya utafiti huu.
61
SURA YA TATU
3.0 MBINU NA ZANA ZA UTAFITI
3.1 Utangulizi
Sura hii inaelezea mbinu mbalimbali za utafiti ambazo zimesaidi kupatikana kwa
data za msingi na data za upili ambazo zimechambuliwa katika sura ya nne.
Miongoni mwa mambo yanayowasilishwa katika sura hii ni pamoja na mpango wa
utafiti, eneo la utafiti, aina ya data zitakazokusanywa, mbinu za kukusanyia data
pamoja na mbinu za uchambuzi wa data bila kusahau zana za utafiti.
3.2 Mpango wa Utafiti
Mpango wa utafiti hutoa picha kamili inayoonesha namna utafiti utakavyofanyika
tangu unaanza mpaka unamalizika (Kothari, 2008). Mpango wa utafiti ndilo
linaloonesha kuwa utafiti husika utakuwa ni wa namna gani na data zitakusanywa
vipi. Zipo aina nyingi za mpango wa utafiti lakini sisi tumetumia uchunguzi kifani
katika utafiti huu. Robson (2007) anaeleza kuwa uchunguzi kifani ni mbinu ya
mpango wa utafiti ambayo hutumika kwa mtafiti kuteua eneo au jambo maalumu
ambalo yeye atalishughulikia katika utafiti wake. Katika utafiti huu tumeteua kazi
mbili za riwaya ambazo ni Kuli na Vuta N’kuvute ambazo ndizo tulizozishughulikia.
Hii ni sawa na kusema kwamba, uchunguzi kifani, wetu ni Kuli na Vuta N’kuvute za
Shafi Adam Shafi. Yin (1994) anaeleza kuwa uchunguzi kifani ni mbinu ya utafiti
ambayo humwezesha mtafiti kutumia muda mfupi na kisha kukusanya data nyingi za
kutosha kukamilisha utafiti wake. Hii inatokana na ukweli kuwa mtafiti anakuwa na
muda wa kutosha kulichunguza jambo moja na hivyo, kuwapo uwezekano wa kupata
data za kutosha kukamilishia utafiti.
62
3.3 Eneo la Utafiti
Eneo la utafiti ni mahali ambapo utafiti unafanyikia kulingana na vile mtafiti
alivyopendekeza ili kupata data za kujibu maswali yake ya utafiti (Creswell, 2009).
Eneo la utafiti huteuliwa kulingana na lengo kuu la mtafiti na kwamba hilo eneo au
maeneo ambayo yanateuliwa ni lazima yaweze kutoa data za kukamilisha malengo
mahususi ya utafiti wake. Maeneo ya utafiti huu ni Dar es Salaam, Unguja na Pemba.
Dar es Salaam ni mahali ambapo kunapatikana maktaba mbalimbali ambazo
zimetusaidia kupata data za upili. Dar es Salaam ndipo wanapopatikana wanazuoni
wengi wa taaluma ya fasihi ambao sisi tumewasaili na kutusaidia kupata data za
msingi. Unguja na Pemba ni mahali ambapo ndipo ulipo muktadha wa utunzi wa
riwaya za Kuli na Vuta N’kuvute. Hivyo, Unguja na Pemba ni pahali muafaka pa
kuwapata wasomaji wengi wa riwaya hizo ambao nao wametusaidia kupata data za
msingi za utafiti wetu.
3.4 Aina ya Data Zilizokusanywa
Kimsingi, katika utafiti huu tumekusanya data za aina mbili ambazo ni data za
msingi na data za upili.
3.4.1 Data za Msingi
Data za msingi ni zile zinazokusanywa kwa mara ya kwanza na hivyo ni data halisi
(Kothari, 2004). Data hizi za msingi hazijapata kukusanywa na mtafiti mwingine
kwa minajili ya utafiti kama huu ambao ulikusudiwa kufanywa kwa mara ya kwanza.
Data za msingi katika utafiti huu zilikusanywa katika makundi mawili. Kundi la
kwanza ni lile ambalo lilihusisha data zilizokusanywa kutoka katika riwaya ya Kuli
63
na Vuta N’kuvute. Kundi la pili ni kutoka kwa wasailiwa ambao walikuwa ni
wanataaluma wa fasihi ya Kiswahili na wasomaji wa riwaya hizo mbili za Shafi
Adam Shafi. Makundi hayo mawili yametupatia data stahiki ambazo zimetusaidia
kukamilisha malengo mahususi ya utafiti wetu.
3.4.2 Data za Upili
Data za upili ni zile ambazo zimekwishakusanywa na watafiti wengine na
kuchapishwa ama kuandikwa (Kothari, 2004). Kadhalika, katika utafiti huu mtafiti,
alikusanya data za upili kutoka katika machapisho mbalimbali ya waandishi. Data
hizi zimesaidia kuthibitisha data za msingi na hivyo kufikia lengo la utafiti huu. Data
za upili hupatikana katika maktaba kupitia vitabu, makala, tasinifu, magazeti,
majarida na vipeperushi.
Vilevile, data za upili hupatikana katika wavuti na tovuti katika mfumo wa
Teknolojia Habari na Mawasiliano. Hivyo, ili kuzipata data hizi tulilazimika kusoma
machapisho mbalimbali katika maktaba za Chuo Kikuu Huria Cha Tanzania, Chuo
Kikuu Cha Dar es Salaam, Chuo Kikuu Cha Taifa Zanzibar na maktaba kuu ya Taifa.
3.5 Watafitiwa
Watafitiwa ni sehemu ya watu au vitu vinavyotafitiwa kutoka katika kundi kubwa la
jamii. Sehemu hiyo huteuliwa na mtafiti kwa kuzingatia sifa na tabia zao ambazo
zinaweza kukidhi katika kuwakilisha kundi kubwa la watu lililobakia. Katika utafiti
huu mtafiti ametumia uteuzi shahada katika kupata riwaya mbili alizoziteua
kuzishughulikia ambazo ni Kuli na Vuta N’kuvute. Uteuzi shahada (au kwa jina
lingine uteuzi lengwa) ni ile ambayo kwa makusudi mtafiti huchagua kundi fulani la
64
watu, vitu au dhana analoamini kuwa linafaa kwa ajili ya utafiti wake. Ni uteuzi
usiokuwa na shaka kwani hutoa majawabu ya uhakika (Kombo na Tromp, 2006).
Uteuzi shahada ulitumika pia kuteua makundi maalumu ya watafitiwa ambayo
yamekidhi haja ya kutafitiwa kulingana na mada ya utafiti. Katika utafiti huu jumla
ya watafitiwa (50) walichaguliwa ili kutoa data zitakazojibu maswali ya utafiti huu.
Watafitiwa hawa ni wanataaluma wa fasihi ya Kiswahili ambao wanapatikana katika
jiji la Dar es Salaam na wengine ni wasomaji wa riwaya za Shafi Adam Shafi
wanaopatikana Unguja na Pemba.Watafitiwa wote hawa walipatikana kwa kutumia
mbinu ya uteuzi lengwa na sampuli nasibu. Sampuli lengwa ilitumika kuwateua
wanataaluma wa fasihi ya Kiswahili ambao jumla yao ni 25. Wakati kwa upande wa
watafitiwa ambao ni wasomaji wa riwaya za Shafi Adam Shafi mbinu ya uteuzi
nasibu ndiyo iliyotumika na kupata jumla ya wasomaji 25. Mtafiti aliteua idadi hii ya
wasailiwa kwa kuwa aliona kuwa ni muafaka katika kuwezesha kupatikana kwa data
za utafiti huu. Pia, sehemu kubwa ya data za utafiti huu zilikusanywa kutoka katika
riwaya teule, hivyo data kutoka maskanini zilitosha kutoka kwa wasailiwa 25.
3.6 Ukusanyaji wa Data
Data za utafiti huu zimekusanywa kwa kutumia mbinu za uchambuzi wa maandiko
maktabani, mahojiano ya ana, kwa ana usomaji wa riwaya teule.
3.6.1 Uchambuzi wa Nyaraka
Mbinu hii ilimuwezesha mtafiti kupata data za upili. Maktaba ni chanzo kizuri kwa
ajili ya tafiti za kimaelezo kwa sababu mtafiti hufanya uchunguzi wa kina katika
muktadha wa tatizo linalohusika. Merrian (1998) Anaeleza kuwa katika maktaba
65
mtafiti huweza kupata data nyingi, kwa urahisi na bila ya gharama. Hivyo, mtafiti
alitembelea sehemu mbalimbali, zinazohifadhi kumbukumbu na nyaraka mbalimbali:
Maktaba ya Chuo Kikuu Huria cha Tanzania na Makavazi iliyopo katika Taasisi ya
Taaluma za Kiswahili na maktaba ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Chuo Kikuu
Cha Taifa Zanzibar na maktaba kuu ya Taifa. Mtafiti alisoma machapisho na
maandiko mbalimbali, kama vile vitabu, makala, magazeti, tasnifu na tahakiki kwa
ajili ya kupata taarifa kuhusu mada ya utafiti. Kwa kutumia mbinu hii, mtafiti
aliweza kupata data za ziada, kwa urahisi.
3.6.2 Mahojiano ya Ana kwa Ana
Mahojiano ni chanzo cha msingi cha utafiti unaotumia mkabala wa kimaelezo
(Kombo na Tromp, 2006). Kothari (2004) anaeleza kuwa mahojiano ni njia ya
ukusanyaji data ambayo inahusisha maswali na majibu yanayoendesha mazungumzo
ya ana kwa ana au simu baina ya mtafiti na mtafitiwa. Kwa mujibu wa Cohen na
wenzake (2000), mahojiano ni mbinu ya ukusanyaji data kwa njia ya mazungumzo
ya moja kwa moja baina ya mtafiti na mtafitiwa.
Faida kuu ya mahojiano ni kwamba mtafiti huchukua maelezo ya moja kwa moja na
ya kuaminika kutoka kwa mtafitiwa, pia yanamsaidia katika kuthibitisha taarifa
zilizo na mashaka. Zaidi ya hayo, taarifa hizo hupatikana kutoka kwa watu wote,
waliosoma na
Powered by Blogger.