UHAKIKI WA KAZI ZA FASIHI ANDISHI UTANZU: USHAIRI KITABU: WASAKATONGE MSHAIRI: MOHAMED S. KHATIB WAHAKIKI: KIDATO CHA NNE – 2013

UHAKIKI WA KAZI ZA FASIHI ANDISHI
UTANZU:    USHAIRI
KITABU:      WASAKATONGE
MSHAIRI:    MOHAMED  S.  KHATIB
WAHAKIKI: KIDATO CHA NNE – 2013
UTANGULIZI:
WASAKATONGE ni moja wapo ya vitabu vinavyotumika kuwatahini watahiniwa wa kidato cha nne kwa upande wa somo la fasihi. Mshairi wa kazi hii amefanikiwa kwa kiasi kikubwa mno kuifunua jamii yake  kwa kuanika UOZO uliomea vilivyo ndani ya jamii aliyoiandikia. Hakika amegusa mambo kadhaa yanayomzunguka mwanajamii; yapo yenye kutia moyo na yenye kukera.

FANI YA WASAKATONGE:
Fani ni ufundi au ujuzi ambao msanii wa kazi ya kifashi anautumia katika kujenga na kuwasilisha kazi yake. Mshairi huyu amefanikiwa kuijenga vilivyo kazi yake akitumia kifundi zaidi vipengele vya kifani hata kuifanya kazi yake iwe ya kipekee mno.
A:  MUUNDO
Ni sura, mjengo au namna ambavyo kazi fulani ya kishairi ilivyojengwa. Kuna vipengele kadhaa vinavyotumika kama sehemu ya muundo navyo ni idadi ya mishororo, vipande,beti na vituo.
Kwa kipengele cha idadi ya mishororo, mshairi ameijenga kazi yake kwa idadi tofauti tofauti ya mishororo kama ifuatavyo:
Ø  Tathlitha:
Katika kazi hii yapo mashairi kadhaa yaliyojengwa kwa mishororo mitatu maarufu kama muundo wa tathlitha nayo ni kama vile; KANSA, HATUNA KAULI, TUTABAKIA WAWILI  na NILINDE.



Mfano;
                               NILINDE

           Nilinde sichukuliwe, hata kwa moja shubiri,
           Tubaki mimi na wewe, pendo letu linawiri,
            Tuwazidishe kiwewe, wasotutakia heri,

Ø  Tarbia:
Ni muundo mwingine katika kipengele cha idadi ya mishororo ambapo mashairi hujengwa kwa mishororo minne kwa kila ubeti. Mshairi pia ametumia muundo huu katika kazi yake hii ya kishairi. Muundo huu unajidhihirisha vizuri katika MAHABA, TOHARA, TONGE LA UGALI, WAFADHILIWA.
Mfano:
                  PEPO BILA KIFO

          Nataka nifikie pepo,
          Nipate raha zilizopo,
          Na kila kizuri kilichopo,
              Nifaidike.

Ø  Takhmisa:
Ni muundo ambao kazi ya kishairi inajengwa kwa mishororo mitano kwa kila ubeti. Mjengo huu unajidhihirisha wazi katika tungo kama vile; UNYAMA, KOSA, WASAKATONGE, TWENDA WAPI?
Mfano:
                    UNYAMA
           Unyama wa binadamu,
           Haukadiriki
           Haufukiriki
           Hausaidiki,
           Ni mnyama wa wanyama.



Ø  Tasdisa:
Ni muundo ambao kazi ya kishairi huundwa kwa mishororo sita kwa kila ubeti. Mashairi ya namna hiyo yanapatikana katika kazi hii nayo ni kama; TIBA ISIYOTIBU, SI WEWE,AFRIKA, ASALI ILPOTOJA.
Mfano:
                     AFRIKA
                Lini?
                Afrika utakuwa,
               Bustani ya amani,
               Ukabila kuuzika,
               Ukabila kuufyeka,
                          Ni lini?

Ø  Sabilia:
Ni muundo ambao kazi ya kishairi hujengwa kwa mishororo saba au zaidi kwa kila ubeti. Katika Diwani hii yapo mashairi kadhaa yaliyojengwa kwa:
·         Mishororo 7 -----      MVUJA JASHO, NILIKESHA, HATUKUBALI
·         Mishororo 8 ------    BUNDI, SIKULIWA SIKUZAMA, VINYONGA
·         Mishororo 10 ------ MADIKTETA, UASI
·         Mishororo  13 -----  MARUFUKU

B.   MTINDO:
Ni tabia ya kiutunzi au uandishi na huhitilafiana kati ya mtunzi na mtunzi mabayo hutegemea ufundi,  hisia na ufanisi wa mtunzi. Mtindo huifanya kazi ya kifasihi kuvutia machoni na masikioni mwa hadhira.
Malenga huyu ametumia mitindo tofauti katika kazi yake kama ifuatavyo;
        I.            Pindu:
Ni mbinu ambayo sehemu ya neno au neno zima la mwisho katika mshororo au kipande huanzisha mshororo au kipande kingine. Mbinu hii inaonekana vizuri katika mashairi ya NAHODHA na KANSA.
                                        KANSA
                         Jamii imeoza, imeoza yanuka
                         Uchafu wachomoza, wachomoza wafoka,
                         Inatoa mafunza, mafunza yamwagika.
    ii.    kikufu:
            tabia kiutunzi ambapo neno la mwisho au kipande cha mwisho katika kituo cha ubeti
            uliotangulia linakuwa neno la kwanza au linaanzisha mshororo wa kwanza wa ubeti
            unaofuatia. M. S. Khatib ameutumia mtindo huu katika shairi la USIKU WA KIZA na    
            MCHEZA HAWI KIWETE

                                     Usiku wa kiza, nimejiinamia
                                     Sana nakuwaza, nakufikiria
                                     Wakunipumbaza, meniondokeya,

                                     Meniondekeya, wangu mahabuba,
                                     Nilikuzoweya, kwa yako mahaba,
                                     Nnajikondeya, sili nikashiba.
          
iii.    Kidato:
         ni mbinu ambayo mshororo mmoja aghalabu wa mwisho hufupishwa kwa sababu maalum.   
         Mbinu hii imetumika vizuri katika NALITOTE, TOHARA.

                                                     NALITOTE
                                     Nalitote, mbao tugawane,
                                     Kwa vyovyote,isiwezekane,
                                     Iwe pute, mali tugawane.
                                                Nalitote.

iv.   maswali:
       ni mtindo ambao mshairi huandika shairi huandika katika namna ya kuhoji jambo. Mtindo  
       huu unaonekana vizuri kupitia mashairi ya AFRIKA, WASO DHAMBI
                                         AFRIKA
                                            Lini?
                                            Afrika utakuwa,
                                            Bustani ya amani,
                                            Ukabila kuuzika,
                                            Udini kuufyeka,
                                                  Ni lini?
v.  Kiitikio:
      Katika mbinu hii mshairi hutumia kibwagizo, Mohamed Seif Khatib ametumia kibwagizo
      katika mashairi yake kadhaa, mfano wa mashiri hayo ni; MAMA NTILIYE, SILI NIKASHIBA,
      TUTABAKIA WAWILI.
                                               BANDARINI
                         3.   utwesi ukenda kombo, zikaingia kikiri,
                               Mrama kikenda chombo, nikaliona kaburi,
                               Mawimbi kupiga kumbo, hamkani si shuwari.
                                       Kiitikio
                               Sitopanda majahazi, vingalawa na vihori,
                               Adha yake siiwezi, ya kuleweshwa chakari,
                               Sisafiri kwa nyambizi, wala kubwa manuwari.

vi.  Takriri: ( Kikwamba )
        Mbinu ya kurudia rudia neno katika nafasi maalum katika mshororo katika ubeti. Takriri hii
        inaonekana katika mashairi kama KWA HERI, HATUKUBALI, NILINDE.

                                                 KWA HERI
                                Ingawa umenuna, vishavu vyako kutuna,
                                          Kunapambazuka, jua linatoka,
                                          Bado kunakucha,
                                                    Kwa heri.

                                Ingawa mekasirika, na uso kusawijika,
                                          Zinavuma pepo, hata kama hupo,
                                          Kusi matlai,
                                                   Kwa heri

vii. Ukaraguni:
       Ni mbinu ambayo vina vya mwanzo na mwisho vinatofautiana katika beti  katika shairi zima.  
       Mtindo huu unajitokeza vilivyo katika shairi la KANSA.

                                        Jamii imeoza, imeoza yanuka,
                                        Uchafu wachomoza, wachomoza wafoka,
                                        Inatoa mafunza, mafunza yamwagika.

                                        Imetunga usaha, usaha usokwisha,
                                        Yazidisha karaha, karaha yatapisha
                                         Yahatarisha siha, siha inadhohofisha.



viii. Ukara:
        mbinu ambayo vina vya kipande kimoja vinabadilika wakati vina wakati vina vya kipande
        kingine vinakaririwa ubeti  mmoja hadi mwingine katika shairi. Mbinu hii, mshairi huyu
        ameitumia katika mashiri kadhaa kama vile; NILINDE,  JIWE SI MCHI, MAMA NTILIYE,
        SIKUJUA.
                        
                                          NILINDE
                     Nilinde sichukuliwe, hata kwa moja shubiri,
                     Tubaki mimi na wewe, pendo letu linawiri,
                     Tuwazidishe kiwewe, wasotutakia heri.

                     Nilinde unifutike, wala sione usiri,
                     Mikononi nisitoke, hata ikizuka shari,
                     Kwa huba unigubike, niwe katika suduri.




C.   MATUMIZI YA LUGHA
Diwani ya WASAKATONGE imetumia lugha fasaha ya Kiswhili ambapo msamiati katika mishororo umepangiliwa katika namna inayovuta udadisi, hisia na matumizi kadhaa vipengele vya hisi kama picha, sauti na uchaguzi wa maneno ili hadhira agundue mchomo ambao malenga huyu aliupata naqzo (hisia ) zaweza kuleta jazba.
§  Matumizi ya tamathali za semi
Tamathali za semi ni viwakilisho au vifananisho vya dhana nyingine tofauti au zinazofanana. Nazo zaweza kupanua, kupuuza ama kubadilisha maana za wazi ili kuleta maana maalum katika ushairi.

Diwani hii ina utajiri wa tamathali za semi kama ifuatavyo:
a.      Tashbiha:
Ni tamathali inayofananisha vitu kwa kutumia maneno ya ufananisho. Tashbiha imeonekana vizuri katika  NILINDE, NILICHELEWA KUPENDWA, KANSA, MWANAMKE.
                                    MWANAMKE
                    Namwona kitandani,
                         Yu uchi maungoni,
                         Ni mrembo,
                        Kama chombo,
                        Chenye ushawishi,
                        Mzima utashi.

b.      Sitiari:
Ni ufananisho wa moja kwa moja bila kutumia maneno ya ufananisho. Sitiari inajidhihirisha katika mashairi kama TIBA ISOTIBU, MTEMEA MATE MBINGU, MAHABA, JIWE SI MCHI, WEWE JIKO LA SHAMBA.
                              WEWE JIKO LA SHAMBA
           Wewe ni jiko la shamba, si kuka si seredani,
           Mezoea kumba kumba, kila aina ya kuni,
           Kwangu huwezi kutamba, nimekutoa thamani.

c.       Msisitizo bayani
Ni tamathali ambayo hutumika kusisitiza jambo kwa kutumia kinyume. Tamathali hii yaonekana kwa urahisi katika mashairi kama BUZI LISILOCHUNIKA, NILICHELEWA KUPENDWA, MCHEZA HAWI KIWETE, BANDARINI.
                              MCHEZA HAWI KIWETE
        Si unyago si sindimba, na wewe kadhalika,
        Hata kukiwa na rumba, machezo hayatatoka,
        Mkilema hata tamba, ngoma yake kunogeka,
           Mcheza hawi kiwete, ngoma yataka matao.

d.      Tashhisi: hali ya kuvipa vitu sifa za binadamu na kuonekana kutenda kama binadamu. Tamatahali hii imeonkana pia kwa urahisi katika mashairi kadhaa, baadhi ni kama vile AFRIKA, NILICHELEWA KUPENDWA, PENDO TAMU.
                            

                                    
                                 PENDO TAMU
               Pendo lenye tabasamu, za dhati si za uheke,
               Na nyoyo za ukarimu, uchoyo ni sumu yake,
               Haliishi yake hamu, hupendi imalizike.

e.      Mubaalagha/ udamisi/ chuku: hali yakutia chumvi sana mambo yanayoonekana kuwa ni ya kawaida. Yanatiwa chumvi kwa makusudi ya kuleta athari maalum iliyokusudidwa  na mwandishi. Nayo yaonekana katika mashairir kama KANSA, AFRIKA na PENDO TAMU.
                              KANSA
                  Jamii imeoza, imeoza yanuka,
                 Uchafu wachomoza , wachomoza wafoka,
                 Inatoa mafunza, mafunza yamwagika.

f.        Taashira:  ni tamathali hutamka sehemu ya kitu kinachohusiana na kingine kikubwa ili kuwakilisha kitu kamili. Tamathali hii yaweza kuonekana kwa uzuri katika shairi la WASO DHAMBI.

                       Wavilemba!
                             Wavilemba, na majoho safi roho, tasbihi,
                                 Wajigamba, safi roho, ni kebehi,
                                    Wanotenda
                                           Unafiki.

§  Taswira:
Ni mkusanyiko wa picha zinazoundwa na maelezo ya jumla ya msanii katika kazi yake ya kifasihi.
Katika kazi ya fasihi , taswira hujengwa kutokanan na matumizi ya tamathali za semi, hasa SITIARI na tashbiha na ishara mbali mbali zenye kuhusu mawazo, dhana, vitu na umbile na kadhalika. Ujenzi wa taswira humfanya msomaji apate aina mbali mbali za hisi kama za kunusa , kuona , kugusa na kusikia.

 Katika diwani hii, mshairi ametumia tswaira mbali mbali kama vile “ tonge la ugali” katika shairi  la TONGE LA UGALI kuashiria madaraka. Kwahivi katika shairi hili mshairi anaweka wazi tatizo la kugombea madaraka.
                   
                              Wanapigana,
                              Wanaumizana,
                              Wanauana,
                                      Kwa tonge la ugali!

Pia kuna matumizi ya picha ya “ nahodha “ kuashiria kiongozi wa jamii, “ jahazi “ kumaanisha nchi au jamii. Katika shairi hili mshairi anaweka wazi tatizo la kung’ang’ania madaraka. Hili ni shairi la NAHODHA.

                             Nahodha,
                             Wang’ang’ania sukani
                             Na jahazi lenda mramamrama,
                             Mrama, na kupasuka mataruma,
                             Mataruma, mkuku umeachama,
                             Meachama, tanga limo kudatama,
                             Kudatama, foromali yainama,
                             Yainama , chombo sasa kitazama,
                             Nahodha tosa nanga!

Kama vile haitoshi mshairi huyu ametumia taswira ya “jiko la shamba” katika shairi la WEWE JIKO LA SHAMBA kuashiria  mwanamke asiyejiheshimu ( Malaya ) anayeshiriki tendo la ndoa  na kila mwanaume.

                            Wewe jiko la shamba, si kuka si  seredani,
                            Mezoea kumbakumba, kila aina ya kuni,
                            Kwangu huwezi kutamba, nimekutoa thamani.

Vile vile, malenga huyu ametumia picha ya “vinyonga” katika shairi la VINYONGA kumaanisha viongozi vigeugeu au wasaliti.

                            Jukwaa
                            Meingiliwa,
                            Wanasiasa vinyonga,
                            Maisha ya ufahari,
                           Kauli zao nzuri,
                           Vitendo vyao hatari,
                           Ni kinyume na maadili,
                           Ni usaliti.

Taswira nyingine inayoonekana katika kazi hii ni ya “fahari la dunia”,katika shairi la FAHALI LA DUNIA, malenga anamaanisha mataifa ya kibeberu/ makubwa. Mataifa haya yanaonea mataifa madogo kisiasa, kiuchumi, hata kitamaduni.

                              Fahali la dunia,
                          Lisilo na huruma, linatesa,
                              Linapiga vindama,
                              Na wengine wanyama,
                              Tena bila ya huruma,
                              Laoneya.
Tena, “bundi” ni taswira nyingine iliyotumika kazi hii, nayo yapatikana katika shairi la BUNDI, picha hii imetumika kuashiria ukoloni mamboleo. Ukoloni mamboleo bado upo na  hautoki. Mataifa ya magharibi yanaendelea kutawala mataifa madogo kwa mbinu nyinginne.

                               Bundi hataki kubanduka,
                               Yu paani amejipachika,
                               Lalialia kila dakika,
                               Mambo si salama,
                               Hakuna uzima,
                               Ila ni nakama
                               Sote twayoyoma,
                                        Hakujacha.

§  Misemo:
 Hizi ni kauli zinazozuka ghafla katika jamii kufuatana na matukio maalum katika jamii nayo husadifu ukweli. Misemo kadhaa imetumika katika kazi hii; nayo hubeba maana iliyokusudiwa.
ü  Sakubimbi jendaheka:
Msemo huu unaonekana katika shairi la MAMA NTILIYE


Wameshindwa wenye nyusi, na kope kukamilika,
Hawakunipa mkosi, ndio kwanza nachanika,
Seuze ukaragosi, sakubimbi jendaheka.

ü  Kumbakumba:
Msemo huu unapatikana katika shairi la WEWE JIKO LA SHAMBA


Wewe ni jiko la shamba, si kuka si seredani
Mezoea kumbakumba, kila aina ya kuni,
Kwangu huwezi kutamba, nimekutoa thamani.

§  Methali:
hizi ni tungo zenye mpangilio maalum wa maneno yenye hekima, busara, mafunzo na maadili kwa jamii. Ubora wa hekima hiyo hutegemea muktadha au mahali ambapo methali hiyo hutumika.

Methali imetumika katika shairi la SADDAM HUSSEIN, nayo ni “ulopanda utavuna!”
               Nakuafiki, Saddam, si kwa Uislamu wako,
                    Ni wako muumba,
                    Ingawa Raisi,
              Ajua yako ila, Saddam, ulopanda utavuna!

MAUDHUI YA WASAKATONGE:
Maudhui ni jumla ya mambo yanayoelezwa ama kujitokeza katika kazi ya kifasihi. Maudhui ya kazi ya kifasihi hujumuisha dhamira , ujumbe, maadili, migogogoro na falsafa.
Diwani ya Wasakatonge imesheheni maudhui yanayogusa mmbo kadhaa yanayoizunguka jamii inayoandikiwa. Malenga huyu anatanabaisha matatizo yanayoikumba jamii kinagaubaga ambayo hasa ndiyo chanzo cha ugumu na uduni wa maisha ya jamii inayoandikiwa.
Katika diwani hii dhamira mbali mbali zimejadiliwa.
A.      Dhamira:
Ni lengo , kusudio au msukumo alionao msanii katika kuumba kazi yake ya kifasihi. Msanii anawezakuwa na lengo la kuonesha mambo mbali mbali yatukiayo ndani ya jamii yake anayoiandikia.
Kazi ya malenga huyu yaweza kugawanywa katika maeneo matatu kidhamira, nayo ni kama ifuatavyo;
1.      Kisiasa:
Malenga huyu anaonekana kusumbuliwa mno na mienendo yetu kisiasa ambayo hakika  ndiyo inayochangia jamii kusonga mbele au kurudi nyuma kimaendeleo. Kisiasa anaichora jamii hivi.


a.      Ung’ang’aniaji wa madaraka:
Mshairi anasikika akilia kwa uchungu juu ya jambo hili lililokuwa kero kubwa ndani ya jamii. Walio madarakani wamekuwa wagumu mno kuachia madaraka wakati unapotimu. Mshairi anasikika vizuri katika mashairi ya TONGE LA UGALI na NAHODHA.
                                   NAHODHA
                      Nahodha,
                      Wang’ang’ania sukani,
                      Mechafuka, bahari si shwari,
                      Si shwari, pepo zinatuathiri,
                      Zatuathiri, na mawimbi ni hatari,
                      Ni hatari, tufani meshamiri,
                      Meshamiri, na mvua zitiriri,
                      Zitiriri,radi nazo si kadiri,
                      Nahodha tosa nanga.

b.      Unyanyasaji na ukandamizaji wa raia:
Malenga huyu ametoa kilio chake pia katika suala hili la dola kuinyanyasa jamii yake. Dola imekuwa ikitumia mamlaka yake vibaya kuwaonea raia wanyonge. Kilio hiki kinasikika vizuri katika mashairi ya UNYAMA, MIAMBA  na MARUFUKU. Sikia kilio cha msanii katika shairi la MARUFUKU.

                  Sitaki uone,
                       Ingawa una macho,
                  Sitaki useme,
                       Ingawa una mdomo,
                  Sitaki usikie,
                       Ingawa una masikio,
                   Sitaki ufikiri,
                       Ingawa una akili,
                  Sababu utazinduka,

                      Utakomboka,
               Uwe mtu,
                      Hilo sitaki
               Marufuku.



c.       Kukosekana kwa uelekeo au itikadi:
Jambo lingine lililomfanya Malenga huyu kutoa machozi ni hilo. Jamii yoyote ile inapokosa itikadi inakuwa sawa na ndege isiyo na rubani. Mshairi wetu anatoa kilio cha kite kuhusu jambo hilo katika mashairi ya NALITOTE na TWENDA WAPI?
Katika shairi la TWENDA WAPI? Mshairi anasema uchungu.

                        Twenda wapi?
                           Mashariki “siko”!
                           Magharibi “siko”!
                           Wapi tuendako?
                                 Tunatapatapa!

d.      Ukoloni mamboleo:
Mshairi anasema kuwa pamoja na jamii yake kujipatia uhuru mapema miaka ya 1960 bado jamii hii imezongwa na inaishi chini ya ukoloni mamboleo. Jamii imechorwa ikishindwa kufanya maamuzi bila kuingiliwa na mataifa makubwa ya Ulaya. Malenga huyu analisema hili kupitia HATUNA KAULI, KLABU, HATUKUBALI, TIBA ISOTIBU, WAFADHILIWA.

                                 WAFADHILIWA
                          Wafadhiliwa kufurahishwa,
                          Ni sera zao kupitishwa,
                          Rais anaamrishwa,
                                  Tekeleza!

2.      Kiuchumi:
Mshairi pia amejadili matatizo ya kiuchumi yanayoizonga jamii yake. Baadhi ya aliyoyaweka qazi ni pamoja na;
a.      Uwepo wa matabaka kati ya wanajamii.
Mshairi analia juu ya msuguano wa kitabaka uliomo ndani ya jamii yake. Mshairi analia mno na hali hiyo inayowatenganisha wanajamii katika makundi mawili ya walionacho na wasionacho. Mashairi ya ASALI LIPOTOJA, MUMIANI, WASAKATONGE, na MVUJAJASHO.




                        ASALI LIPOTOJA
                        Asali lipotoja,
                        Wengine walikuja,
                        Na mirefu mirija,
                        Kwao kawa tafrija,
                        Wakapata faraja,
                        Sisi tukatengwa.

                        Kairamba asali,
                        Kafakamia kweli,
                        Nao hawatujali,
                        Wakatutenga mbali,
                        Kwa fujo na kejeli,
                        Wakatoneya.

b.      Kutokuwajibika kwa wanajamii:
Mshairi anaiona jamii yake kama jamii isiyotaka au isiyopenda kufanya kazi na hivi kutegemea misaada na huruma za nchi tajiri. Jambo hili linamkera mno na kumuumiza hata kulisemea. Mshairi ananung’unikia hali hiyo katika KLABU na WANAWAKE WA AFRIKA. Angalia kilio cha mshairi katika KLABU.

                Tusiwe tegemezi,
                Ila tuchape kazi,
                Tutumiye ujuzi,

                Tuvijenge viwanda,
                Na kilimo kutanda,
                Ufugaji kushinda.

c.       Njaa na ukame:
Mshairi anaguswa pia na hali ya ukame na njaa inayoikumba jamii yake.
Jamii imejadiliwa ikizongwa na ukame usiokwisha unaosababisha njaa. Mshairi anailalamikia hali hiyo katika shairi la AFRIKA.


                 Lini?
                 Afrika utakuwa,
                 Kitalu chenye shibe,
                 Na njaa isikabe,
                 Pia watu washibe,
                         Ni lini?

                 Lini?
                 Afrika utakuwa,
                 Adui wa ukame,
                 Kwa vyovyote uhame,
                 Na usikuandame,
                        Ni lini?

d.      Ugumu wa maisha:
Mshairi tena anaumizwa na ugumu wa maisha unaowazonga wanajamii wake ingawa wanajitahidi kupambana kwa kila hali. Mshairi analiweka hilo bayana kupitia mashairi ya AFRIKA, MVUJA JASHO, TWENDA WAPI? Angalia kilio chake katika MVUJA JASHO

                 Kila mvuja jasho,
                 Maishaye ya kesho,
                 Si ya utajirisho,
                 Achumacho ni posho,
                 Mbaya wake mwisho,
                 Lazima suluhisho,
                        Lakini kwa vitisho.

3.      Kijamii:
Kijamii pia mshairi amesumbuliwa na masuala kadhaa katika jamii yake kama alivyosumbuliwa na masuala ya kisiasa na kiuchumi. Masuala hayo ya kijamii ni kama;
a.      Usaliti na unafiki wa viongozi wa dini:
Ndani ya jamii anayoiandikia, mshairi analalamikia viongozi wa dini kwa kutokuwa wakweli na wawazi kwa wale wanaowaongoza. Mshairi anaumia dhidi ya mitindo yao ya maisha ambayo imeshindwa kuwa mfano mzuri kwa jamii. Mshairi anayaonesha hayo katika mashairi ya UASI na WASO DHAMBI. Sikiliza sauti yake katika UASI

                     Uasi,
                            Katika dini,
                     Masheikh na masharifu,
                     Mapadri na maaskofu,
                     Kauli zao nadhifu,
                     Hujigamba waongofu,
                     Wengi wao ni wachafu,
                     Wenye vitendo dhaifu,
                     Dini wanazikashifu,
                              Wanafiki.

b.      Ukabila na udini:
Mshairi analia tena juu ya tabia hii iliyoota mizizi miongoni mwa jamii nyingi za kiafrika ya kuendekeza undugu, ukabila na udini ambayo ni chanzo cha uvunjifu wa amani ndani ya jamii yake. Mshairi anayasema hayo katika AFRIKA na SADDAM HUSSEIN.

                       AFRIKA
                       Lini?
                       Afrika utakuwa,
                       Bustani ya amani,
                       Ukabila kuuzika,
                       Udini kuufyeka,
                              Ni lini?

c.       Ushoga, usagaji na umalaya:
Mshairi anaisuta pia jamii yake juu ya tabia ya kujenga uhusiano kinyume na maumbile iliyojengeka ndani ya jamii yakepia tabia ya ufuska ambazo ni kero kubwa kwa jamii. Mshairi analisema hilo kupitia mashairi ya WEWE JIKO LA SHAMBA na  JIWE SI MCHI. Angalia shairi la JIWE SI MCHI.
                                                  Vinu wenzake ni michi, wala sibadilishiwe,
                                                  Ufundi haujifichi, utwanzi na mizunguwe,
                        Jiwe la manga si fichi, haiakidhi hajawe.

d.      Unafiki, majungu na umbeya miongoni mwa akina mama:
Hili ni jambo lingine ambalo linamuumiza kichwa mshairi huyu. M.S. Khatib analia juu ya tabia ya akina mama ya kuendekeza fitina, vitimbi na kufanyiana majungu  bila sababu ya msingi. Anaitaka jamii hii iachane kabisa na jambo hilo. Anayaesema hayo kupitia  WANAWAKE WA AFRIKA na MAMA NTILIYE.
Msikie mshairi huyu katika WANAWAKE WA AFRIKA.

                          Achaneni kusengenyana,
                          Waama kununiana,
                          Kugombana,
                          Kusutana,
                          Nguvu zenu zapungua,
                                 Mtashindwa!

Msikie tena katika MAMA NTILIYE

                     Majungu na makaango, jinsi unavyoyapika,
                     Wakazanisha na shingo, moto uzidi kuwaka,
                     Kwa uzushi na uwongo, kumbe kwako umefika.

e.      Mwanamke kuwa chombo cha starehe:
Vilevile mshairi anainyooshea kidole jamii yake kutokana na mtazamo ilionao kwa mwanamke kuwa kama chombo cha kuburudisha macho na miili ya wanaume. Hili linaonekana katika shairi la MWANAMKE.
                                                 Namwona kitandani,
                                                       Yu uchi maungoni,
                                                        Ni mrembo,
                             Kama chombo,
                             Chenye ushawishi,
                             Mzima utashi.

f.        Mwanamke kufanywa mlezi pekee wa familia:
Hili nalo linamliza mshairi, mbali ya kufanywa kuwa ndiye msimamizi pekee wa familia bado mama huyu hathaminiwi na jamii yake. Hili laonekana katika shairi la MWANAMKE.

                       Namwona yu nyumbani,
                           Mpishi wa jikoni,
                           Yaya yeye,
                           Dobi yeye,
                           Hakuna malipo,
                           Likizo haipo.

g.      Mapenzi ( uhusiano wa kijinsiakati ya watu wawili )
Mshairi anautazama uhusiano huu katika namna mbili. Wapo wanajamii ambao wamekuwa wakijenga uhusiano wa kilaghai na wenzao labda kwa lengo la kujinufaisha kiuchumi au kukidhi haja za miili yao. Jambo hili linamuumuza sana mshairi kwani mapenzi ya namna hii yanazingirwa na:

 usaliti kama inavyojitokeza katika USIKU WA KIZA

               usiku wa kiza, nimejiinamia,
               sana nakuwaza, nakufikiria,
               wakunipumbaza, meniondokeya.
                           Kukosekana kwa amani kama ilivyojitokeza ITOE KAULI YAKOna USIKU WA KIZA.
                             ITOE KAULI YAKO
                Kitoe chako kiapo, kama kweli wanipenda,
                Niweze kujizatiti, moyo uondoke funda,
                Nizidi kukudhibiti, sikuache hata nyanda.

Kukosekana kwa furaha ndani ya nyumba kama inavyojitokeza katika SI WEWE na USIKU WA KIZA.
                     USIKU WA KIZA
                Meniondokeya, wangu mahabuba,
                Nilikuzoweya,kwa yako mahaba,
                Nnajikondeya, sili nikashiba.

Pia yapo mapenzi yaliyosheheni udhati na ukweli, mapenzi ya namna  hii yamezingirwa na mambo haya;
Udhati, faraja na raha kati ya wapendanao. Hili linaoneshwa katika mashairi ya MAHABA na NILINDE.
                               NILINDE
                    Nilinde wasinipate, wabaki kutahayari,
                   Tubaki chanda na pete, kama udi na ambari,
                   Wabaki kumeza mate, waambulie sifuri.

Amani na utulivu miongoni mwa wapendanao, hili laonekana katika mashairi ya TUTABAKI WAWILI na WEWE WAJUA.
                             TUTABAKIA WAWILI
                  Wenyewe tunajienzi, hakuna cha kuhofia,
                 Tunaishi kwa mapenzi, raha kuziogelea,
                  Wala hatuna simanzi, roho zetu maridhia.

Furaha kati yao wapendanao kama ilivyo katika YEYE NA MIMI na PENDO TAMU.
Angalia PENDO TAMU.
                 Pendo lisilo maudhi, na wala upekepeke,
                 Wawili limeturidhi, ni kubwa haiba yake,
                 Kupendana ni faradhi, yeye wangu mimi wake.

B.      Ujumbe:
Ni taarifa anazotoa msanii kwa hadhira,; ujumbe mara nyingi hutokana na dhamira na unaweza kujitokeza wazi au kwa kujificha.
Katika diwani ya Wasakatonge mshairi anatoa ujumbe ufuatao;
ü  Mwannamke ana haki sawa na mwanaume yeyote kayika jamii kupitia mashairi ya MWANAMKE.
ü  Matabaka ni chanzo cha migogoro katika jamii; hili linaonekana kupitia mashairi kama WASAKATONGE, MVUJASHO na WALALAHOI.
ü  Mapenzi ya dhati hujenga mshikamano na uaminifu ndani ya jamii kupitia mashairi kama TUTABAKIA WAWILI, PENDO TAMU na YEYE NA MIMI.
ü  Kufanya kazi kwa bidii ni suluhisho la umaskini; ujumbe huu unaonekana kupitia shairi la WANAWAKE WA WAAFRIKA na KLABU.
ü  Uongozi mbaya ni chanzo cha umaskini na minyukano ndani ya jamii; taarifa hii yapatikana kupitia SADDAM HUSSEIN, UNYAMA na MIAMBA.
ü  Tohara kwa wanawake huweza kuleta matatizo makubwa kama vifo na magonjwa, anasema hili katika shairi la TOHARA
ü  Kung’ang’ania madaraka kunaweza kukaleta kukosekana kwa raha na amani  na kutokushirikiana miongoni mwa wanajamii. Hili linasemwa kupitia  shairi la NAHODHA na TONGE LA UGALI.

C.      Maadili:
Haya ni mafunzo, nasaha au ushauri unaopatikana mara baada ya kusoma kazi ya kifasihi. Malenga huyu anatoa ushauri kwa jamii yake kulingana na mazingira  waliyomo.
ü  Malenga huyu anaitaka jamii yake iachane na utamaduni wa kumkkeketa mwanamke kwani hakusaidii lolote. Anasema hilo kupitia shairi la TOHARA
ü  Mshairi anaishauri jamii yake kuachana na tabia ya kung’ang’ania madaraka kwani haina faida yyoyote. Hili linajidhihirisha kupitiaTONGE LA UGALI na NAHODHA.
ü  Vile vile mshairi anaitaka jamii yake ipige vita tabia kushiriki tendo la ndoa kinyume na maumbile na ufuska kupitia JIWE SI MCHI na WEWE JIKO LA SHAMBA.
ü  Mshairi anaitaka jamii yake ifanye kazi kwa bidii na kuachana na tabia ya utegemezi kupitia KLABU.
ü  Mshairi tena anaitaka jamii yake kujifunza kuwa na upendo wa kweli hasa kwa wanandoa ili kuimarisha ndoa zao kupitia mashairi ya YEYE NA MIMI, PENDO TAMU na WEWE WAJUA.
KUFANIKIWA AU KUTOFANIKIWA KWA MWANDISHI
KIMAUDHUI
Mwandishi amefaulu kimaudhui kwa kuonesha udhaifu mkubwa unaomea ndani ya jamii yake anayoiandikia kuanzia kwa viongozi mpaka kwa mtu mmoja mmoja.
Mshairi huyu amefanikiwa kuwachora viongozi kama ndio chanzo kikuu cha matatizo yaikumbayo jamii kwa kushindwa kuwajibika vilivyo katika dhamana walizokabidhiwa na hivyo kuzua mitafaruku mingi ndani ya jamii hii; wao ndio vyanzo vya kukithiri kwa rushwa ndani ya jamii yetu hasa wanaposhindwa kukemea au wao wenyewe kuwa washiriki wa tendo hilo kama alivyoliweka wazi hili katika shairi la KANSA au MVUJA JASHO.


Powered by Blogger.