KISWAHILI IV-NADHARIA YA USHAIRI

NADHARIA YA USHAIRI
Ushairi ni sanaa inayojipambanua kwa mpangilio maalum wa maneno fasaha na yenye muwala, kwa lugha ya mkato, picha au sitiari au ishara katika usemi maandishi au mahadhi ili kueleza jambo,wazo au tukio au hisi fulani kuhusu maisha, mazingira ya binadamu kwa namna inayogusa moyo.
Ushairi ni utanzu / fani mojawapo ya fasihi ambao umbo lake hutofautiana na tanzu nyingine za fasihi, mathalani tamthiliya na riwaya na riwaya.
Utanzu huu una historia ndefu iliyojikita katika fasihi simulizi za jamii zilizohusika. Kutokana na historia yake ndefu ni jambo la kukubalika kuwa hapana budi kuwepo na mabadiliko ambayo yamechimbuka kutoka kipindi kimoja kwenda kingine.
Baadhi ya mabadiliko yaliyochimbuka katika ushairi ni hali ya kuwa na MASHAIRI HURU/ MASIVINA/ YA KISASA amabayo hayafuati kanuni za kimsingi ambazo washairi wa awali WANAJADI/ WANAMAPOKEO wananazizingatia.
Ushairi wa Kimapokeo na Masivina:
Kuna tofauti kubwa kati ya utenzi, shairi la kimapokeo na masivina. Nazo zaweza kuwa hivi;
Utenzi
Shairi la kimapokeo
Masivina
Utenzi hugawanyika katika beti zenye idadi sawa ya mistari.
Hugawanyika kama utenzi katika beti mbalimbali na katika idadi sawa ya mistari.
Kuna beti mbalimbali lakini idadi ya mistari inatofautiana mara nyingi kutoka kifungu hadi kifungu.
Kwa kawaida utenzi unagawanyika ama kuundwa na mistari minne katika ubeti.
Laweza kuwa na mistari miwili, mitatu na kuendelea katika ubeti kufuatana na matakwa ya msanii.
Si rahisi kutaja idadi ya mistari katika ubeti mmoja wa shairi kwani hutofautiana mara kwa mara.
Mistari hugawanyika katika mizani ambayo huwa kati ya 8 na 12.
Mistaari hugawika katika mizani na maranyingi huwa 16 lakini si chini ya mizani 11.
Mizani uwepo lakini hutofautiana kutoka mstari hadi mstari.
Utenzi una vina vya mwisho vinavyofanana.
Lina vina vya kati vinavyofanana na vya mwisho vinavyofanana. Navyo vyaweza kufanana kwa shairi zima au la.
Urari wa vina haujipambabui sana kama ilivyo katika shairi la kimapokeo.
Beti zake hazijitoshelezi, mawazo yake yanaendelezana kutoka ubeti hadi ubeti.
Ubeti mmoja hujitosheleza hivyo waweza kuwa na shairi la ubeti mmoja tu.
Maana ya shairi hupatikana baada ya kulisoma shairi lote.
Kimsingi utenzi huwa mrefu kuliko shairi la kawaida nao mara nyingi huelezea tukio moja kwa kirefu sana.
Mara nyingi haliwi refu sana na linaweza kuwa na ubeti mmoja.
Mara nyingi huwa na urefu wa wastani. Yanafanana na mashairi ya kimapokeo.
Utenzi katika usimulizi wake mara nyingi huanza na dua au kumaliza na dua
Si jambo la muhimu sana ingawa baadhi ya wasanii hufanya hivyo
Dua halijitokezi katika masivina.




Sanaaa hii ya ushairi yaweza kujipambanua katika;
·         Tenzi
·         Nyimbo
·         Mashairi
·         Ngonjera.

ISTILAHI ZA KISHAIRI
Istilahi ni maneno yanayotumika katika uwanja fulani maalum. Sanaa ya ushairi ina istilahi zake, nazo ni kama vile;
v  Utoshelezi:
Katika arudhi ya kimapokezi, kila ubeti unahitajika kuwa na maana kamili inayojitosheleza au inayojisimamamia bila kutegemea ubeti unaofuata au unaotangulia na vile vile kuwa na mtiririko mzuri wa habari zinazoelezwa.
v  Muwala:
Ni mtiririko wa mawazo na fani na mantiki katika shairi. Muwala unaweza kuwa wa namna mbili. Mosi, inapasa mawazo katika kila ubeti yawe yanafuatana kwa ufasaha kutoka mstari wa kwanza hadi wa mwisho.
Pili shairi liwe na mtiririko mzuri wa mawazo kutoka ubeti hadi ubeti katika shairi.


v  Ubeti:
Ni mgawo wa vifungu katika shairi, utenzi, wimbo au ngonjera unaojitosheleza kimaana. Huu ni ubeti wa shairi:
1.      Hicho ni kitu nasema, maarufu duniani,
Si kikubwa chake kima, si kidogo wastani,
Tena ni kitu cha nyama, kina ladha mdomoni,
Nyama nje ngozi ndani, ni kitu gani wajuzi?

v  Mshororo:
Ni mstari katika ubeti wa shairi, tenzi au ngonjera. Katika mashairi ya arudhi inapasa mishororo iwe na idadi ya mizani iliyo sawa.
Ubeti ulioainishwa hapo juu una mishororo minne.

v  Kipande:
Ni sehemu za mshororo wa ubeti  wa shairi ambazo hutenganishwa na alama ya mkato. Mwishoni mwa kila kipande katika mshororo huwa kuna kina. Mashairi mengi huwa na vipande viwili katika kila mshororo.

v  Mizani:
Ni silabi ambazo zimo katika kila mshororo wa kila ubeti. Mfano:
    Hi-cho  -ni- ki-tu- na-se-ma, ma-a-ru-fu du-ni-a-ni

v  Vina:
Hizi ni silabi zinazofanana ambazo hujitokeza mwishoni mwa kila kipande katika kila mshororo wa ubeti.

v  Kituo:
Huu ni mshororo wa mwisho katika ubeti wa utungo wa shairi. Maneno ya kituo yaweza kuwa yanayokaririwa kutoka ubeti hadi ubeti ambayo huitwa BAHARI, yanayobadilikabadilika kutoka ubeti hadi ubeti ambayo huitwa KIMALIZIO au yanayobadilika kwa kipande kimoja kutoka ubeti hadi ubeti ambayo hitwa NUSU BAHARI.

DHIMA YA USHAIRI
Ushairi una umuhimu mkubwa sana katika jamii. Kwanza ulikuwa unatongolewa kama fasihi simulizi katika jamii nyingi za kiafrika. Baada ya mabadiliko ya kihihstoria, kiuchumi na kisayansi ulianza kuandikwa kama fasihi andishi.
Ushiri hutegemea mapigo au mahadhi yanayotumika kuweza kuibua hisi mbalimbali ambazo humfanya msomaji/ msikilizaji aone furaha au huzuni. Kwa muhtasari tu dhima za ushairi ni:
ü  Kuibua hisia na kuburudisha au kuhuzunisha
ü  Kuadhibu
ü  Kuweka kumbukumbu/ kuhifadhi amali za jamii
ü  Kukuza na kuhifadhi lugha
ü  Kunoa fikra
ü  Kuelimisha
ü  Kuhamasisha

MAMBO YANAYOJENGA USHAIRI WA KIMAPOKEO ( KI-ARUDHI)
 FANI
A.    MUUNDO
Ni msuko, umbo au uwiano wa vipengele vyote vinavyojenga ushairi. Ushairi waweza kuainishwa kimuundo kwa kuzingatia.
·         Idadi ya mishororo:
Ø  Tathnia:
Ni ushairi wenye beti zenye mishororo miwili kwa kila ubeti. Shiri la tathnia huwa na urari wa vina na mizani.
Mfano:
           Ingawa ni nchi yangu, mie siipendi sana,
           Ina tando na ukungu, kadha mawimbi mapana,

Ø  Tathlitha:
Ni ushairi wenye mishororo mitatu kwa kila ubeti. Tathlitha pia huitwa UTATU.
Mfano:
             Nakupa waswia, moyo shika mno,
             Niloyakimbiya, henda penye sono,
             Yangalikujiya, usinene neno.

Ø  Tarbia:
Ni ushiri ulio na mishororo minne kwa kila ubeti. Tarbia pia hufahamika kama UNNE. Kidesturi shairi la tarbia huwa na mishororo iliyogawanyika katika vipande viwili.
Wakati mwingine mshororo wa mwisho wa tarbia huwa na utaratibu wa kuteua vina vinavyotofautiana na vina vya mishororo mitatu inayotangulia.
Ushairi huu ndiyo kwasi na maarufu kuliko aina/ miundo yote katika utanzu wa ushairi kiasi kwamba unahatarisha uhai wa miundo mingine ya kishairi.



Ø  Takhmisa:
Ni ushairi wenye mishororo mitano katika kila ubeti. Ushairi huu pia huitwa UTANO au TAKHMISI.
Zipo takhmisa ambazo zilitungwa zikiwa hazina mgawo wa vipande viwili kama ilivyozoeleka sasa na zikiwa na mizani kufikia 15.
Mfano:
           Moyo siwe pite kama jua mwendawazimu
           Kwanda tafakari umbo lako ulifahamu
           Ni tone la mayi lalokaa likawa damu
           Tei Tabaraka lahu kaliumba Mola Karimu
           Katia mifupa na mishipa ngozi na nyama.

Ø  Tasdisa:
Ni utungo wenye mishororo sita katika kila ubeti. Huitwa pia USITA, TARDISA, TASHLITA.
Utungo huu si maarufu sana katika ushairi wa Kiswahili. Tungo hizi kama vile tungo za mistarisaba, nane,tisa, kumi au kumi na mbili hazina mifano mingi.
Mfano:
            Ikinipasa kungoja, mpaka nijue vema,
            Pasivumbuke mmoja, kwa makosa kunisema,
            Daima hautakuja, tukawa hivi daima,
            Sitatenda neno moja, kwa kuchelea lawama,
            Na jambo hili lafuja, hata kidogo si jema,
            Mtenzi hahofu hoja, wala lawama ya nyuma.
Kigezo kingine cha kuainisha muundo wa kazi ya kishairi ni;
·         Idadi ya vipande:
Ø  Mashairi ya  vipande viwili ( manthawi ):
Mara nyingi mashairi huwa na vipande viwili; kipande cha kwanza na cha pili.
Mfano;
           Ewe la azizi, uloniepuka,
           Kama mkimbizi, anavyotoroka,
           Rejea mpenzi, bado nakutaka.

Ø  Mashairi ya vipande vitatu ( ukawafi )
Yapo mashairi mengine yamejengwa kwa vipande vitatu.
Mfano:
            Mja hana haya, haya hazimo, mwake usoni
            Mja ni mbaya, hutimba shimo, ungiye ndani
            Na ukishangiya, azome zomo, furaha gani
            Mmoja kwa miya, ndiye hayumo, baya kundini.

Ø  Ushairi wa kipande kimoja ( utenzi )
Mizani ya mishororo huwa michache toka 4 hadi 12. Kwa kawaida utungo huu una vina vya mwisho bila vya kati. Utenzi husimulia habari ndefu tena nzito. Pengine huwa juu ya tukio Fulani, maelezo ya mtu mashuhuri, historia au visa.
Mfano:
            Mali ukishika,
            Ukitoa sadaka,
            Budi takukuka,
            Kwa Mola jalia.
Mbali ya idadi ya mistari, vipande pia KITUO ni kigezo kingine cha kuainisha muundo wa kazi za kishairi.
·         Kituo:
Hutumiwa kumaanisha mshororo wa mwisho katika ubeti wa utungo wa ushairi. Aina za kituo hutegemea maneno yanavyotumika katika mshororo huo.
Kama maneno ya kituo yanakuwa yaleyale yanayokaririwa kutoka ubeti hadi ubeti huitwa BAHARI au kibwagizo.
Tena kama yanabadilikabadilika kutoka ubeti mmoja hadi mwingine huitwa KIMALIZIO.
Wakati mwingine maneno ya kipande kimoja hubadilika na kipande cha pili hubaki vivyo hivyo kutoka ubeti mmoja hadi mwingine. Kiyuo hiki huitwa NUSU BAHARI.

B.      MTINDO:
Ni tabia ya utunzi au uandishi na huhitilafiana kati ya mtunzi na mtunzi ambayo hutegemea ufundi, hisia na ufanisi wa mtunzi.
Katika mtindo mhakiki huangalia yafuatayo;



v  Pindu:
Ni mbinu amabayo sehemu ya neno la mwisho au neno la mwisho katika mshororo au kipande huanzisha mshoro au kipande kingine.
Mfano:
            Nyayo, kanyagio umekanyaga mwiba,
            Mwiba, ni mwiba hasa si kijiba,
            Si kijiba, na wala siyo mbigili,
            Siyo mbigili, bali mchongoma,
            Kuutoa ndio ngoma!

v  Kikufu:
Ni tabia ya kiutunzi ambapo neno la mwisho au kipande cha mwisho katika kituo cha ubeti uliotangulia linakuwaneno la kwanza au linaanzisha mshororo wa ubeti unaofuatia.
Mfano:
            Mcheza hawi kiwete, kilema kilomshika,
            Lau mchezo wa kete, angezila pasi shaka,
            Au kama kibafute, ushindi angeushika,
            Mcheza hawi kiwete, ngoma yataka matao.

           Ngoma yataka matao, huchezwa kwa kudemka,
            Kwa maringo na pumbao, mwili wote kunyumbuka,
            Haichezwi kama bao, komwe zako kupangika,
            Ngoma yataka matao, mcheza hawi kiwete.

v  Kidato:
Ni mbinu ambayo mshororo mmoja aghalabu wa mwisho hufupishwa kwa sababu maalum.
Mfano:
           Dhuluma isipoondoka, kwa amani,
           Na haki zetu kukoseka, kuwa shani,
           Lazima twalazimika, tuamuweni,
           Turudi mwituni, tuwe vitani, tuwasakeni,
                     Damu tumwaeni.







v  Malumbano:
Ni mbinu ya kiutunzi amabyo mshairi anatoa maoni au anashiriki katika mjadala fulani wa kishairi. Mbinu hii huonekana zaidi katika magazeti.
Mfano:
            Wa ubani Bawaziri, na Kandoro kadhalika,
            Lumbano la kishairi, gazetini kuliweka,
            Nami nimejikusuri, maoni kuyatamka,
               Ua si ruwaza njema,tunzo ya mtu kupewa.

v  Maswali:
Ni mtindo ambao mshairi huandika shairikatika namna ya kuhoji jambo.

v  Majibizano:
Ni mtindo unaojitokeza zaidi kwenye kipera cha ngonjera ambapo wahusika wawili au zaidi hujibizana.
Mfano:

            KAKA
            Kusoma nilikosoma, nambiwa sipati kazi,
            Yapata mwaka mzima, nategemea shangazi,
            Wasioujua husema, sababu sina ujuzi,
            Huo uhaba wa kazi, mesababishwa ni wake.

            DADA
            Mbona watuingilia, kaka acha ubaguzi,
            Likukeralo twambia, tulijuwe waziwazi,
            Au unalochukia, ni wake kufanya kazi?
            Mambo ya kisiku hizi, watu ni bega kwa bega.

v  Taabili:
Ni mtindo ambao shairi huandikwa katika namna ya kumlilia mtu au kuomboleza aliyefariki.



Mfano:
            Amina umejitenga, kufa umetangulia,
            Kama ua umefunga, baada ya kuchanua,
            Nakuombea mwanga, peponi kukubaliwa,
            Mapenzi tuliyofunga, hapana wa kufungua.

v  Kiitikio:
Ni mbinu nyingine ambayo kazi ya kishairi huwa na kibwagizo. Mbinu hii hujidhihirisha zaidi katika kipera cha nyimbo.
Mfano:
            Rabi utubarikie, la wawili pendo letu,
            Rehemu tuzidishie, zisafike nyoyo zetu,
            Roho zetu zitulie, tusitamani vya watu.
      Kibwagizo:
             Nia yangu sigeuzi, kupenda anipendaye,
             Ajue nitamuenzi, milele taishi naye.

v  Takriri( kikwamba ):
Ni tabia ya kurudiarudia neno/ maneno katika nafasi maalum katika mshororo katika beti.
Mfano:
            Duniani, vyakula hawavioni, mafakiri,
            Lakini, vyakula, kwao pomoni, mabepari,
            Abadani, hawa si waja wa Mungu.


            Duniani, wanalala majiani, mafakiri,
            Lakini, wanalala ghorofani, mabepari,
            Abadani, hawa si waja wa Mungu.

            Duniani, nguo mbovu matakoni, mafakiri,
            Lakini, nguo tele kabatini, mabepari,
            Abadani, hawa si waja wa Mungu.

v  Masimulizi:
Ni mbinu ambayo shairi huandikwa au kuimbwa katika mtindo wa usimulizi.
Mfano:

            Hadithi inayokuja, ni ya sungura sikia,
            Hadithi uliyongoja, leo ninakuletea,
            Alitoka siku moja, njaa aliposikia,
            Njaa aliposikia, sungura nakuambia.

v  Ukara:
Ni mtindo ambao vina vya kipande kimoja vinabadilika wakti vya kipande kingine vinakaririwa ubeti mmoja hadi mwingine katika shairi.
Mfano;
            Nyuki ni mtanashati, umbo na zake tabia,
            Yeye yu kila wakati, vichafu kuvikimbia,
            Mchana na lailati, hatui kwa kukosea,
            Kuntu Sauti ya Kiza, nyuki hapendi vichafu.

            Nyuki hatui topeni, na zizini kuingia,
            Sijamwoni karoni, mikojo kufakamia,
            Haingii na chooni, hata kwenye mazulia,
            Kuntu Sauti ya Kiza, nyuki hapendi vichafu.
v  Mtiririko:
Ni mtindo ambao vina vya mwanzo na vya mwisho vinakaririwa kutoka ubeti mmoja mpaka mwisho wa shairi, vinakaririwa katika shairi lote.
Mfano:
            Nijapotendwa ubaya, na wabaya kiwajua,
            Mwenzio huona haya, ubaya kuwatendea,
            Japo moyo una waya, hufanya kuuzuia,
              Nacheka hali najua, Hila zina maulaya,

          Hila zina maulaya, na wakinishambulia,
          Nyama ilooza mbaya, mbesi huifurahia,
          Samba huona vibaya, kula kilojiozea,
            Japo zogo la ngamia, Hila zina maulaya.


v  Ukaraguni:
Ni mtindo ambao vina vya mwanzo na mwisho vinatofautiana katika beti katika shairi zima.
Mfano:
            Kitedo kimetendeka, onyesho limetimiya,
            Baruti imelipuka, baki ni moshi na maya,
            Taa sasa zinawaka, mwenye macho angaliya,
                Limeanguka paziya, sasa mwaka ni dakika.
             Kariuki kifo chako, ni jogoo amewika,
             Amesikika tuliko, saa ya kupambazuka,
             Kwa kipofu sikitiko, wenye macho wanacheka,
                 Pazia limeanguka, tujitafute tuliko.

C.      MATUMIZI YA LUGHA:
           Lugha ndiyo malighafi ya ushairi. Utamu na ubora wa shairi hutegemea mtunzi anavyomudu kuchagua na kupanga maneno yake ili yalete athari au matokeo aliyokusudia. Hivyo mshairi ni lazima awe na hazina kubwa ya msamiati.

1.      Uteuzi wa msamiati/ maneno:
Uteuzi wa msamiati huzingatia
a.      Kile kinachosemwa.
b.      Muktadha wa kisarufi
c.       Umbo la shairi.
               Kama shairi lina mpangilio wa vina, maneno yanayoteuliwa kuwa ya mwishoni mwa
              mshororo sharti yaishie kwenye silabi zinazooana na vina vya shairi. Kadhalika maneno
              yanyoteuliwa inabidi yaingie katika mfumo wa urari. Ni vigumu kupunguza, kuongeza au
              kubadilisha neno katika shairi zuri bila kuvuruga muwala wa shairi.

2.      Mpangilio wa maneno:
Maneno ya ushairi hupangwa ili kuleta maana fulani, sauti za aina fulani au urari fulani wa mizani.
Kwa kawaida katika Kiswahili kivumishi hufuatia nomino lakini kwenye ushairi pengine kivumishi hutangulia nomino. Mwandishi wa ushairi huweza kubadilisha mpangilio huo kwa sababu maalum, pengine hufanyika ili kulinganisha vina.


Mfano:
                                       Suu ulimwengu bahari tesi,
             Una masaibu na mengi maasi

Mpangilio huu usio wa kawaida huvuta udadisi kuliko lugha ya kawaida na hutumika kusisistiza vipengele fulani vya hisi au wazo fulani la msanii ingawa si lazima shairi liwe na m[angilio usio wa kawaida ili lipendeze kwani vipengele kama taswira vyaweza kuleta athari ya mguso.


3.      Matumizi ya lugha ya picha/ taswira:
Ni matumizi ya lugha yanyopambanuliwa na uteuzi mzuri wa maneno, ulinganifu na udhahiri wa maelezo wenye kuhusisha na kujumuisha dhana mbali mbali tofauti ndani ya dhana moja ili kuleta taswira na athari maalumkatika mawazo ya msikilizaji. Ni mkusanyiko wa picha zinzoundwa kutokana na maelezo ya msanii katika kazi yake ya kifasihi.
Katika fasihi , taswira kwa kawaida hujengwa kutokana na matumizi ya tamathali za semi, hasa sitiari na tashbiha na ishara mbalimbali zenye kuhusu mawazo , dhana, vitu na maumbile.
Mshairi anapotumia taswira huwa na nia ya kuchochea hisia za msomaji za uoga , furaha, kilio, hasira au kukarahishwa.

4.      Tamathali za semi:
Ni umathilishaji wa jambo kwa kulinganisha au kufnanisha na lingine. Ni viwakilisho au viwakilisho kwa dhana nyingine au zinavyofanana. Mara nyingi tamathali zinaweza kupanua, kupuuza amakubadilisha maana za wazi ili kuleta maana maalum katika ushairi.
Tamathali za usemi pia zaweza kutumika kuipamba kazi ya sanaa ya kifasihi kwa kuongeza utamu wa lugha iliyotumika. Baadhi ya tamathali hizo ni:

a.      Tashbiha:
Ni tamathali ya ufananisho au mlinganisho wa vitu viwili  au zaidi. Hulinganishwa kwa sura, sifa au tabia kwa kutumia maneno ya ulinganisho.
Mfano.
            Kweli ni sawa na radi, inapotoa kaul…
            Kweli kinywani ikawa sawa na mto Nile…
            Kwali kama msumeno, hukereza sawa kweli.

b.      Tashhisi:
Kitu kisichokuwa nauhai hupewa  sifa za kitu chenye uhai hasa za kibinadamu. Kifasihi maelezo ya kitashihisi huwa na upekee unaomwingia mtu akilini haraka.
Mfano:
             Kimya hakineni jambo, si kimya chawatazama
             Kimya chajazua jambo, pasiwe mwenye kusema..
             Kimya kipimeni sana, msione kutosema,
             Kimya hakiishi kunena, kitakapo husimama,
             Kimya chaja katakana, kizue yaliyozama.
c.       Mubaalagha au Udamisi:
Aina hii tamathali hutia chumvi sana mambo yanayoonekana kuwa ya kawaida. Yanatiwa chumvi kwa makusudi ya kuleta athari maalumu iliyokusudiwa na mwandishi. Angalia sentensi hii.

            Nitakuandikia barua za mapenzi zitakazojaza posta yote ya Jiji.
d.       Kejeli:
Ni usemi ambao maana yake ya ndani ni kinyume na inabeua maana yake halisi. Ni usemi wa kebehi ambao kisemwacho sicho kikusudiwacho na msemaji.
Mfano:
            Huifanya fedha kuwa Mungu wao,
            Itazame adha na imani yao!
            Na mwenye akili kama hana fedha,
            Hatajwi mahali ila kwa rakadha.
            Na kuadhieriwa kuwa mtu duni,
            Tazama dunia ilivyo na dini!

e.      Sitiari:
Ni tamathali ya semi ambayo athari zake hutegemea uhamishaji wa maana na hisi kutoka katika kitu au dhana moja hadi kitu  au dhana nyingine tofauti. Vitu hivyo viwili vyenye kuhusishwa kwa kawaida huwa havina uhusiano wa moja kwa moja. Sitiari ni picha ingawa  picha si lazima iwe sitiari ila sitiari ni kipengele cha muhimu kabisa katika ushairi na matumizi yake bora hudhihirisha ubingwa na uwezo wa mshairi.

f.        Takriri:
Ni marudiomarudio ya sauti, silabi, neno, sentensi au wazo ili kuleta athari na maana maaalum kwa msikilizaji au msomaji wa shairi hilo. Njia ya kishairi ya kuonesha uzito wa hisia, kusisitiza wazo au dhamira fulani.
Marudiomarudio haya huvuta hisia na udadisi na umakini wa msomaji wa shairi ingawa pia kwaweza kumchosha msomaji kama ufundi hautotumika.
Mfano:
             Siku ya panga kufuta,
                        Mashujaa kwenda kombo,
             Siku ya kuja matata,
                        Na fadhaa na mshindo,
             Siku ya watu kuteta,
                        Kufua moyo mfundo,
             Siku ya nchi kutota,
                        Kwa damu kwenda mkondo…
g.      Mjalizo:
Ni mbinu ya kuunda maneno yanayofuatana bila kuwa na viungo vilivyozoewa kama vile na, kwa, mfano, kama…
Mfano:
            Nilikaa, nikashangaa, nikachoka.
            Niliimba, nikanuna, nikacheka.

MAUDHUI
Maudhui  ni mawazo  yanayozungumzwa na msanii wa kazi ya kifasihi pamoja mtazamo wa mwandishi au msanii juu ya mawazo hayo.

A.       DHAMIRA:
Ni wazo kuu lililomo katika kazi ya kisanaa. Huu ni msukumo alionao mwandishi hata akaandika kazi fulani ya kifasihi. Msanii anaweza kuwa na lengo la kuonesha madhara ya ufisadi, matatizo ya ndoa, umaskini, uongozi mbaya au upofu wa kisiasa.

B.      UJUMBE:
Ni taarifa aipatayo msomaji asomapo shairi au kazi ya kifasihi. Ujumbe unawezwa kutazamwa kwa njia kuu mbili unaweza kuwa mbaya au wenye mafunzo mabaya au ukawa mzuri.

C.      MAADILI:
Haya ni mafunzo, nasaha au ushauri unaopatikana mara baada ya kupitia kazi Fulani ya kifasihi.

D.     MTAZAMO:
Utetezi au hali ya kubeza aliyonayo msanii.



Powered by Blogger.