Unachopaswa kufanya siku ya uchaguzi

Jaji Damian Lubuva, Mwenyekiti NEC
Dar es Salaam. Tanzania inaelekea kwenye Uchaguzi Mkuu, Oktoba 25, mwaka huu. Baadhi ya wananchi hasa vijana waliofikisha miaka 18 hivi karibuni hawajawahi kushiriki kwenye uchaguzi wowote na uchaguzi huu ni wa kwanza kwao.
Vijana hawa na watu wengine, wanahitaji kujifunza au kukumbushwa juu ya mambo ya kufanya siku ya uchaguzi ili kufanya zoezi la upigaji kura kuwa lenye mafanikio na kuepusha uvunjifu wa sheria unaoweza kumweka mtu matatani.
Kwa bahati mbaya, elimu kwa mpigakura haitolewi mara kwa mara kwa wananchi mpaka nyakati za uchaguzi. Hata wakati huo ukifika, baadhi ya watu hasa wale wa hali ya chini, hawafikiwi na elimu hiyo.
Elimu kwa mpiga kura bado inahitajika ili kila mwananchi afahamu haki na wajibu wake katika mchakato mzima wa uchaguzi. Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) ndiyo yenye jukumu la kutoa elimu hiyo kwa kushirikiana na wadau wengine.
Hata hivyo, zoezi hili linakabiliwa na changamoto ya uhaba wa rasilimali za kufanikisha utoaji wa elimu kwa wapigakura. Vilevile, hakuna chombo maalumu cha kuratibu na kusimamia utoaji wa elimu ya uraia.
Mwenyekiti wa Nec, Jaji Damian Lubuva anasema changamoto kubwa wanayokabiliana nayo ni pamoja na uhaba wa Asasi za kiraia zinazotoa elimu kwa wapigakura na kuwafikia wananchi wote nchi nzima.
Jaji Lubuva anasema Tume imejipanga vizuri kuhakikisha kwamba elimu inawafikia wapigakura nchi nzima. Anasema watatumia vyombo vya habari vikiwamo vinavyomilikiwa na taasisi za dini ili kuwafikia wananchi haraka zaidi.
Zingatia haya siku ya uchaguzi
Mkurugenzi wa uchaguzi – Nec, Kailima Kombwey anafafanua mambo muhimu ambayo mpigakura anatakiwa kufanya siku ya uchaguzi bila kuathiri masharti ya sheria za uchaguzi na kanuni zake.
Wahi kituoni
Anasema jambo la kwanzana la msingi ni  kuwahi asubuhi katika kituo cha kupigia kura. Kombey anasema wananchi wanatakiwa kufika vituoni kuanzia saa moja asubuhi wakiwa na vitambulisho vyao vya kupigia kura.
Anasema kila mpigakura anatakiwa kujua kituo atakachopigia kura na kuhakiki kama jina lake lipo kwenye orodha ya wapigakura kwenye kituo husika.
Panga foleni
Kombey anabainisha kuwa watu watapanga foleni kuingia chumba cha kupigia kura na vituo vitafungwa kuanzia saa 10 jioni. Anasema watakaokuwa kwenye mstari baada ya muda huo wataruhusiwa kuendelea kupiga kura mpaka watakapomaliza.
“Tunasisitiza wananchi wajitokeze kwa wingi ili wawachague viongozi wao. Kupiga kura ni jambo la muhimu kwa maendeleo ya Taifa letu. Wasipojitokeza basi wasilaumu kiongozi atakayechaguliwa na wengine,” alisema Kombwey.
Mkurugenzi huyo anasema katika uchaguzi wa mwaka 2010, waliandikisha watu milioni 20 lakini waliojitokeza kupiga kura walikuwa chini ya milioni 10. Kwa hiyo, anasisitiza zaidi kujitokeza kupiga kura siku hiyo.
Usivae sare za chama
Jambo la pili, mpigakura asivae nguo yenye nembo au alama yoyote ya chama cha siasa kwenye kituo cha kupigia kura. Kufanya hivyo ni kukiuka taratibu za uchaguzi na mtuhumiwa anaweza kushitakiwa kwa kuhujumu mchakato wa upigaji kura.
Kombey anafananisha jambo hilo na akufanya kampeni siku ya kupiga kura, jambo ni kinyume na kanuni. Kwa hiyo, fulana, kofia, bendera au kanga au nguo yoyote inayovaliwa na chama chochote haitakiwi kwenye eneo la kupigia kura.
“Tunatoa muda wa kampeni ili wanasiasa na vyama vyao wajinadi kadri wanavyotaka lakini siku ya uchaguzi siyo siku ya kufanya kampeni, ni kinyume cha kanuni za uchaguzi,” anasema mkurugenzi huyo.
Anaendelea kubainisha kuwa Tume kupitia kifungu cha 124 (a) cha sheria ya taifa ya uchaguzi ya mwaka 1985 ilianda maadili ya uchaguzi ambayo yamefanyiwa mabadiliko madogo mwaka huu na kukubaliwa na vyama vyote.
Wahusika wakuu katika maadili haya ni Tume ya Uchaguzi, Serikali, wagombea na wanachama wote wa vyama vya siasa. Kombwey anasema wadau hawa kwa pamoja wana wajibu wa kufanya uchaguzi huru na wa haki.
Usilete ushabiki
Jambo la tatu, wapigakura wasilete ushabiki kwenye vituo vya kupigia kura. Mambo ya ushabiki ni pamoja na kuongelea matokeo ya uchaguzi kabla hayajatangazwa na mamlaka husika zilizokasimiwa jukumu hilo.
Mkurugenzi huyo anafafanua kwamba jambo hilo linajenga hisia tofauti miongoni mwa wapiga kura na linaweza kusababisha vurugu endapo matokeo yatakuwa kinyume chake. Anabainisha kuwa kura ni siri ya mpigakura mwenyewe.
“Sitarajii kuona watu wakitengeneza makundi ya kujadili mwenendo wa uchaguzi kwenye vituo. Hiyo ni sawa na kampeni siku ya uchaguzi, hatutaacha ufanyike kwa sababu utaharibu mchakato wa uchaguzi,” anasema.
Ukipiga kura nenda nyumbani
Jambo la nne, mwananchi akimaliza kupiga kura aende nyumbani kusubiri matokeo kutangazwa. Kuendelea kukaa kwenye vituo vya kupigia kura kunasababisha msongamano usio wa lazima.
Kombwey anasema hakuna haja ya kukaa kwenye vituo vya kupigia kura kwa ajili ya kulinda kura kwa sababu tayari mawakala wa vyama vya siasa wapo kwa ajili ya kuangalia mwenendo mzima wa uchaguzi.
“Ile dhana ya kutaka kulinda kura zisiibiwe ndiyo inayosababisha vurugu kwenye vituo. Hizo ni hisia tu, hakuna wa kuiba kura kwa sababu kuna mawakala wanaowakilisha vyama vyao,” anasema.
Tume ina jukumu la kutangaza matokeo
Anasema jukumu la kutangaza matokeo ya urais ni la Tume ya uchaguzi. Tume pia imekasimisha jukumu la kutangaza matokeo ngazi ya kata kwa msimamizi msaidizi wa kata na ngazi ya jimbo kwa msimamizi wa halmashauri.
Kombwey anasema kuna baadhi ya watu wanatishia kutangaza matokeo endapo Tume itachelewa kufanya hivyo. Anasisitiza kuwa kufanya hivyo ni kinyume cha utaratibu kwa sababu hakuna mtu mwenye jukumu hilo zaidi ya Nec.
Anasema Nec imejipanga kutangaza  matokeo ya urais ndani ya siku tatu kwa sababu watatumia Mfumo wa Kusimamia Matokeo (RMS) ambao utawawezesha kupokea, kujumlisha na kutangaza matokeo.
Licha ya kutakiwa kisheria kutangaza matokeo hayo ndani ya siku saba, Nec imebainisha kwamba mfumo huo utasaidia kuongeza kasi ya ukusanyaji wa matokeo kutoka sehemu mbalimbli nchini.
Mabadiliko ya sheria
Jaji Lubuva anasema mabadiliko makubwa ya sheria ya uchaguzi yalifanyika mwaka 2010, mwaka huu sheria hiyo haijafanyiwa marekebisho isipokuwa kanuni za uchaguzi zimerekebishwa ili kuleta ufanisi katika uchaguzi ujao.
Powered by Blogger.