NYANZA: Mwenyekiti wa Bawacha adaiwa kutekwa na kujeruhiwa

Image result for bendera ya chadema       Image result for bendera ya chadema                           Geita. Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake la Chadema (Bawacha) mkoani Geita, Husna Amri (34) ameokotwa na wafyatua matofali wa Mtaa wa Pakacha Wilaya ya Kondoa, Mkoa wa Dodoma, akiwa amepigwa na kujeruhiwa sehemu mbalimbali za mwili wake.
Amri ambaye inadaiwa kuwa alitekwa na watu wanne wasiofahamika Agosti 16, akiwa njiani akitokea wilayani Nyang’hwale Mkoa wa Geita kwenye mkutano wa uchaguzi wa madiwani wa viti maalumu akielekea mjini Kakola kupanda gari kurejea nyumbani kwake Buseresere wilayani Chato.
Baada ya kuvamiwa na watu hao, walimpeleka kusikojulikana. Hali hiyo ilizua hofu kwa wanachama wenzake, ndugu na jamaa.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, Joseph Konyo alisema taarifa za kutekwa kwa mwenyekiti huyo walizipata kutoka kwa Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Geita, Alphonce Mawazo baada ya kupigiwa simu na mwenyekiti huyo usiku wa kuamkia Jumatatu akilalamika kuwa ametekwa anahitaji msaada.
“Tuliamua kufuatilia baada ya kupokea taarifa hizo hadi jana (juzi) saa 2:00 usiku, tulipata taarifa kutoka Kituo cha Polisi Kondoa kuwa kuna mwanamke ameokotwa akiwa anakimbizwa na watu wanaodaiwa ndiyo waliomteka,” alisema Konyo.
Kamanda Konyo alisema polisi walipomuuliza Amri ili awapatie taarifa sahihi, alidai kuwa wakati anatoka Nyang’hwale alivamiwa na watu wanne wakiwa kwenye pikipiki ambao walimchukua hadi Kakola wilayani Kahama na kumpeleka mahala kusikojulikana.
“Wakati anajaribu kujiokoa watu hao walishtuka na kuanza kumkimbiza, lakini wakati wanakaribia kumkamata alikuwa tayari amefika eneo ambalo kuna watu hivyo alipiga kelele kuomba msaada, watekaji walipoona watu walikimbia na kuacha mfuko ukiwa na panga jipya na sindano mbili za kushonea nguo.”
Alisema tayari watu wawili wanashikiliwa akiwamo mwendesha pikipiki aliyembeba mwenyekiti huyo kutoka Nyang’hwale na mwanachama mwenzake, ambaye anaelezwa alipanda naye kwenye pikipiki moja na alishuka njiani.
Awali, Diwani wa Kata ya Buseresere, Chrispian Kagoma (Chadema) akielezea mkasa huo alidai kuwa kabla hajatekwa akiwa Nyang’hwale, wanachama wenzanke walimtaka alale lakini alikataa kwa madai kulikuwa na watu wanamtafuta ambao ni wafuasi wa chama kimoja cha siasa kwa sababu aliwahi kukorofishana nao kwenye mambo ya siasa, hivyo alihofia usalama wake.
Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Geita, Alphonce Mawazo alikiri kutekwa kwa Amri na kwamba, hali hiyo inawapa hofu wapinzani, kwani hilo siyo tukio la kwanza kuna mwenyekiti wa Chadema Kata ya Kalangalala alitekwa na watu wasiojulikana Aprili na hadi sasa hajapatikana.
Powered by Blogger.