MALENGA WAPYA WAANDISHI: TAKILUKI WACHAPISHAJI: O.U.P MWAKA : 1997

MALENGA WAPYA
WAANDISHI: TAKILUKI
WACHAPISHAJI: O.U.P
             MWAKA : 1997

UTANGULIZI
MALENGA WAPYA ni diwani yenye mkusanyiko wa mashairi yapatayo thelathini na saba (37) yaliyoandikwa na washairi wapya(malenga wapya). Washairi hawa ni wanafunzi wa Taasisi ya Kiswahili na Lugha za Kigeni huko Zanzibar.
Katika diwani hii ,washairi wamejadili masuala mbalimbali yanayotokea katika jamii. Baadhi yake ni masuala ya kisiasa, kiuchumi, kijamii n.k.Washairi hawa wamejadili masuala ya msingi katika kujenga jamii mpya na kama yatazingatiwa mabadiliko chanya yatatokea kwenye jamii.
MAUDHUI YA MALENGA WAPYA:
Maudhui ni mawazo yanayozungumzwa na msanii wa kazi ya kifasihi pamoja mtazamo wa mwandishi au msanii juu ya mawazo hayo.
A). DHAMIRA:
Ni wazo kuu lililomo katika kazi ya kisanaa.Huu ni msukumo alionao mwandishi hata akaandika kazi Fulani ya kifasihi.Mshairi anaweza kuwa na lengo la kuonesha mambo mbali mbali- mienendo mizuri na mibaya- yatokeayo katika jamii.Katika diwani hii washairi hawa wameyachora mambo kadhaa yatendwayo na jamii, nayo ni kama;
1. UONGOZI MBAYA
Washairi wa diwani hii wamezungumzia suala la uongozi mbaya kama ndicho chanzo cha kudorora kwa maendeleo ya jamii katika Nyanja mbalimbali.Mwandishi ameonesha kuwa viongozi wengi hawatekelezi wajibu wao na pia hawapati muda wa kusikiliza shida za wananchi,viongozi hupuuza kuchukua hatua hata kwa mambo yanayotaka ufumbuzi wa haraka.Kama shairi la PUUZO msanii anasema;
                   Unapokuwa na shida, wao wanakupuuza,
                   Wanajitia kidata, na kuifanya ajiza,
                             Wajifanya hawajali.
                  
                    Ofisini ukifika, wanakuweka baoni,
                   Wakati uliofika, wao hawauthamini,
                             Wanakuambia subiri.
Hali kadhalika viongozi wengi wadhulumaji kwani huwalazimisha wananchi wanunue hata huduma ambazo kimsingi ni stahiki yao.Katika shairi la BAHARI . Msanii ameonesha dhahiri namna viongozi wanavyotumia nafasi zao kuwakandamiza wananchi.Mshairi anasema
                   Mdai ni haki yao, mola amewajalia
                   Kuwadhulumu wenzao, wao wanafurahia,
                   Nao kwa unyonge wao,wadogo wateketea,
                   Bahari ni hatari,wala usichezee,
Katika shairi la MPAKA LINI? Mshairi anelezea kuwa viongozi wana kawaida ya kuwanyanyasa wananchi wanaosema ukweli na kuwakumbatia wale wanafiki na wafitini,kama ubeti huu usemavyo
                   Msema kweli, kwenu nyinyi ni chagizo,
                   Mtaka hali, havuki mbele ya vikwazo,
                   Mwongo sana, kwenu nyinyi ni kigezo,
                   Mpaka lini mtatuchezea?
Pia mwandishi amebainisha jinsi viongozi wasivyo tekeleza ahadi zao na kubaki wanapayuka (kuhutubia majukwaani) mfano katika shairi la PAYUKA (uk 50).
                   Kupayuka kwenu huko,
                   Mbona tu kokoriko,
                   Sioni linalokuwa

2.     MATABAKA
Mwandishi ameonesha katika jamii kuna matabaka mawili tabaka la chini (tabaka tawaliwa) na tabaka tawala linavyogandamiza na kulinyonya tabalka la chini ( linavyotumikiswa na kulinganishwa na punda) mfano katika shairi la PUNDA msanii anasema;
                   “Toka tulipozaliwa, maishayo ni kigozo,kizogo,
                   Hatujapata kuenziwa, waishi tingivyogo,
                   Nawe hujajielewa, u kiumbe u kigogo,
                   Kama ungefadhiliwa, usingebeba mzigo,
                   Hakika ulionewa, hustahili kupigwa kipigo,
                   Haki umeitambua, idadi japo kidogo”
Vile vile suala la matabaka limejadiliwa na mwandishi mfano mshairi wa SAMAKI MTUNGONI (UK 19) shairi hili linaonyesha tabaka la juu yaani tabaka tawala (viongozi) ambao ni wavuvi na tabaka la chini yaani tabaka tawaliwa ni samaki, tabaka hili linanyonywa na kugandamizwa.
Katika Shairi la  NINI WANANGU (UK 24) msanii ameonesha maisha ya chini ya tabaka la chini. Tabaka hli lina hali mbaya ya maisha ukilinganisha na tabaka la juu.
Pia katika Shairi la MKULIMA (uk 3) wasomi wanaonesha tabaka la chini (wakulima ) lisivyothaminiwa na tabaka la juu hali hii inasababisha kunyimwa kwa huduma muhimu wanazotakiwa kupewa raia.
3.     ATHARI ZA UKOLONI MAMBOLEO
Ukoloni mamboleo ni hali ya nchi moja kutawala nchi nyingine kiuchumi.Ukoloni mamboleo unaathiri uchumi wanchi zinazoendelea. Katika Shairi NIPATIENI DAWA, mwandishi anaonesha kuwa baada ya ukoloni kuondoka nchini ukoloni huo ulirudi kwa umbo (sura) nyingine ukiendeleza taratibu za kikoloni za kunyonya uchumi wanchi masikini .
                   “Palepale penye donda, ndipo apajanibana,
                   Nikawa sasa nakonda, pumzi nikawa sina,
                   Nikabaki kama ng’onda, la kufanya sikuona,
                   Nipatieni dawa, nipate kutononoka,
                   Kila nikifurukuta, donde apata toa,
                   Najitia kwenye tata, shida kujizidishia,
                   Dawa nimeshatafuta, ili niptate kuoa,
                   Nipatieni dawa, nipate kutononoka.”
Mwandishi anaonesha jinsi ukoloni mamboleo ulivozifanya nchi masikini na kunyonya uchumi wake hivyo basi ili kuondokana nao ni lazima atafute dawa.

4.    NAFASI YA MWANAMKE KATIKA JAMII
Mshairi wa diwani hii amemjadili au amemchora mwanamke katika sura au nafasi tofautitofauti kama ifuatavyo:-
Ø Mwanamke ni msaliti
Katika shairi la UTANIKUMBUKA mwanamke anaonekana ni mtu asiye mwaminifu katika mapenzi na ndoa yake kwa sababu anashiriki ngono na wanaume wenye pesa na mali nyingi huku akimuacha mume wake ambayeni msikini. Mshairi anasema
          “Umeona bora kitu, ukasahau ya nyuma,
          Umetupa mbali utu, na zote zangu huruma,
          Kwako kutokaa katu, iko siku utakwama,
          Utaumeza uwatu, iwe ni yako hatima”.
Ø Mwanamke ni mtu mwenye tamaa mbaya
Katika shairi la UTANIKUMBUKA,mwanamke anaonekana ni mtu mwenye tamaa ya kutaka vitu kutoka kwa wanaume sio kuangalia penzi la mtu. Mwanamke anaonekana kuwa ni mlafi wa mali na mwenye kutamani mali.
Ø Mwanaume kama chombo cha starehe(muhuni/Malaya)
Katiaka shairi la “KITENDAWILI” mwanamke anaonekana ni chombo cha starehe (mtu Malaya) yaani mtu asiyetulia kwa mwanamme wake (ndoa yake) huku akishiriki mapenzi na wanaume wengine kiasi cha kuogopwa na wengi kwa matendo yake. Mshairi anasema
          “Jogoo lina mafamba, linatamba kiamboni,
          Kwa kiburi lajigamba, hadi kiambo jirani,
          Hili jogoo la shamba, sasa lawika mjini,
          Kitendawili natega, mteguzi ategue”.
Aidha katika shairi la KUUNGE, mwanamke amechorwa kama chombo cha starehe (mtu Malaya) yaani anashiriki tendo la ngono na wanaume wengi ili kukidhi haja ya matamananio ya wanaume. Umalaya husababisha mwanamke kupata magonjwa mbalimbali ikiwemo UKIMWI na hivyo kuwaambukiza wanaume wengi. Mshairi anasema
          “Nawambia silipandi, hii pingu naiweka,
          Naogopa sina kundi, nikifa la kunizika,
          Nawapenda kina bundi, na kila anayeruka,
                   Silipandi kataani”.
Ø Mwanamke ni mtu mwenye mapenzi ya kweli
Katika shairila “NIPATE WAPI MWINGINE” mwanamke anaonekana ni mtu mwaminifu katika mapenzi, mtiifu, na mtu mwenye tabia njema. Ndio maana baada ya kufa,mume wake (mshairi) alimlilia sana. Mshairi anasema:
          “Njiwa ali maridadi, kwa tabia hana shaka,
          Na hakuwa mkaidi, umwitapo kakufika,
          Mafanowe Kama radi, chini inapoanguka,
          Njiwa ameshanitoka, nipate wapi mwingine”.
Ø Mwanamke ni kiumbe dhaifu/duni
Katika shairi la “KIFUNGO”, mwanamke anaonekana ni kiumbe dhaifu kisichoweza kufanya chochote cha maendeleo kwani humtegemea mumewe kwa kila kitu na kunyimwa haki yake ya msingi ya kutafuta riziki.Mwanamke hufungiwa ndani ya nyumba pasipo kutoka nje akifanya kazi ya kupika na kulea watoto tu. Mshairi anasema
          “Kwa kuwa ni mwanamke, ndani munanifutika,
          Lazima nje nitoke, kupata ninayotaka,
          Nimechoshwa na upweke, sitaki kudhalilika,
          Kifungo kimenichosha, minyororo nafungua”.
5.    UMUHIMU WA KUINUA UCHUMI
Ili Kujenga taifa linalojitegemea ni lazima kujenga uchumi unaoweza kuleta maendeleo.Mwandishi anaonyesha umuhimu wa kilimo ili kuepukana na adui njaa. Katika Shairi la ADUI msanii anasema;
                   “Tulime jama tulime, tushinde adui njaa,
                   Hapa kwetu ituhame, kwengine kutokomea,
                   Wala sisi tusikome, chakula kujilimia,
                   Tutie jembe mpini, tuteremke shambani,
                   Chakula kujilimia, ziada kujipatia,
                   Tuache kutegemea, vya nje kuagizia,
                   Siku watajigomea, nani tutamlilia?
                   Tutie jembe mpini, tuteremke shambani”.
Kwa upande wa kilimo mwandishi ameonesha kuwa kilimo ni uti wa mgongo wa taifa letu,katika shairi la MKULIMA mwandishi ameonesha kuwa  mkulima ni mtu wa kumthamini kwani yeye ndiyo kila kitu kama beti hizi mbili zinazothibitisha;
“Wakaazi wa mjini, na wafanya kazi pia,
Na viongozi nchini, huduma awapatia,
Sijui kakosa nini?, thamani kutomtia,
Mkulima naye mtu, yafaa kuthaminiwa”

“Upungufu wa chakula, utokeapo nchini,
Hukumbana na suala, shambani wafanya nini?,
Kazi yako unalala, watia njaa nchini,
Mkulima naye mtu, yafaa kuthaminiwa”.
Mwandishi anaonesha kuwa jamii inapaswa kumdhamini mkulima kwani anamchango mkubwa katika maendeleo ya taifa.

6.    UMUHIMU WA KUTENDA MEMA
Ili jamii iishi kwa utulivu na amani,watu wote hawana budi kutenda mema.Katika shairi la USIHARAKIE MAISHA,waandishi wanataka wanafunzi wanaosoma wasiharakie maisha kwa kutamani vitu vya kesho wakati wao wanaishi leo. Pia katika Shairi la MAISHA NI KAMA NJIA mwandishi anataka jamii itende mema bila kuwatendea wengine uovu hivyo kiburi na ubabe haufai katika jamii (maisha).
    Pia katika Shairi la ULIMI mwandishi amezitaka ndimi ziseme mambo mazuri tu kama ubeti ufuatao unavyosema;
“Usiropoke kwa wenzio, kwanza sema,
Usipachike pachike, maneno yasiyo mema,
Useme wanufaike kwa kauli yako njema,
Ewe ulimi sikia”
Mwandishi anaitaka jamii itende mema nyakati zote ili jamii nzima iishi vyema.

7.    UMUHIMU WA KUTUMIA PESA VIZURI
Mali bila daftari hupotea bila habari. Hivyo amini inaaswa uwe na matumizi mazuri ya pesa, mfano shairi la ISRAFU,msanii anasema;
“Mali uliyojichumia,
Ni yako nakubalia,
Lakini kiangalia,
Vipi unaitumia’
Mwenzangu nakuusia,
Israfu haifai”.
Hivyo matumizi mabaya ya pesa husababisha umasikini ambao husababisha mhusika kukimbiwa na watu hata rafiki zake.

8.    MAPENZI NA NDOA
Mapenzi na ndoa ni kitu cha muhimu katika jamii.Mfano shairi la UA mwandishi anasema mtu afikapo umri wa kuoa au kuolewa basi na afanye hivyo shairi la NIPATE WAPI MWINGINE,wasani wanauliza walimwengu wapate wapi wenzi wao baada ya yule wa kwanza kuwatoka.Vilevile wanasema mapenzi ya siku hizi hayafai kwani hutegemea zaidi fedha.Ni mapenzi yenye kusababisha umalaya, yamejaa udanganyifu kati ya mwanamke ana mwanaume mfano shairi la KWA NINI?. Wasanii wanakemea tabia ya baadhi ya wanaume wanaowaacha wake zao na kufanya uzinzi na wanawake wengine wa na kupoteza pesa zao.
“Mke wake, atamwacha, singizini,
Atoroke, parakacha, migombani,
Kumbe kake, anakocha, mwa jirani,
Kwa nini?”.
Mwandishi anaitaka jamii kuwa na mapenzi ya dhati ili kuepusha maumivu kwa anayeachwa na jamii kwa ujumla.

B). UJUMBE
Waandishi wa diwani hii ya MALENGA WAPYA wanatoa ujumbe ufuatao;
Ø Kuinua uchumi ni jambo la muhimu sana kwani kutapunguza utegemezi wa misaada kutoka nchi zilizoendelea.Ujmbe huu unapatikana katika shairi la “MKULIMA”, “PUUZO”, “ADUI” na ‘TUYAZINGATIE HAYA”.
Ø Ukombozi wa mwanamke ni muhimu kwaajili yake na jamii nzima. Ujumbe huu unapatikana katika shairi la “KIFUNGO”,“HINA INAPAPATUKA”, na “PUNDA”.
Ø Hamadi kibindoni silaha iliyo mkononi.Hii ina maana kwamba ni vema kujiwekea akiba kwa kuzingatia matumizi mazuri ya mali, ikiwemo pesa, kwaajili ya maisha mazuri ya kesho. Ujumbe huu unapatikana katika shairi la “ISRAFU”.
Ø Ili kuinua uchumi wa nchi ni lazima kusisitiza kilimo na kumthamini mkulima. Ujumbe huu unapatikana katika shairi la “MKULIMA”.
Ø Jamii izingatie maadili mema ili kuleta haki, usawa na amani. Ujumbe uu unapatikana katika shairi la “HAKI” na “SIHARAKIE MAISHA”.
Ø Matabaka ni kikwazo kikubwa cha maendeleo ya jamii.Ujumbe huu unapatikana katika shairi la “SAMAKI MTUNGONI’, “MKULIMA”.
Ø Maisha ni kama njia.Hapa duniani si makazi ya kudumu,isipokuwa mbinguni.Hivyo tutende mema na tumwombe Mungu ili tuje kuishi maisha ya raha baada ya kifo.Ujumbe huu unapatikana katika shairi la “MAISHA NI KAMA NJIA”.
Ø Uongozi mbaya hurudisha nyuma maendeleo ya jamii.Ujumbe huu unapaikana katika shairi la “PUUZO” na “BAHARI”.
Ø Subira yavuta heri hivyo kila avumiliaye ipo siku atapata.Ujumbe huu unapatikana katika shairi la “SIHARAKIE MAISHA”.

B: MAADILI
Haya ni mafunzo, nasaha au ushauri unaopatikana mara baada yakuiptia kazi ya kifasihi.Ni maelekezo ambayo huelekezwa kwa hadhira ili iweze kutoka katika hali iliyomo na kuelekea kwenye jamii mpya yenye Maendeleo na utengemano. Katika hili washairi hawa wameitaka;
·       Jamii kuachana na tabia ya uvivu na utegezi  na kuwa wachapakazi ili kuunua uchumi wa nchi na maisha ya jamii kwa ujumla. Hili limesisitizwa vizuri kupitia mashairi ya TUYAZINGATIE HAYA, CHARUKA na ADUI. Hebu chunguza ubeti huu wa shairi la ADUI.
               Haya shime tuitane,sote tushirikiane,
Wala tusitegeane,kwa pamoja tushikane,
Aliye mwoga anene, kabisa tusigombane,
Tutie jembe mpini, tuteremke shambani.
·       Pia wanaume walio katika ndoa kuachana na tabia ya uasaliti wa ndoa zao kwani kwaweza kusababisha maafa makubwa kwa wanafamilia. Washairi wanashauri hili kupitia shairi la KWA NINI? Wanapohoji sababu hasa wanaume kuchepuka.
Utamwona, mwanaume, kashaini,
Anong’ona, na Selume, chochoroni,
Ndio laana, ajipime, japatani?
            Kwa nini?
·       Hali kadhalika malenga hawa wameielekeza jamii yao hasa viongozi kuacha kukandamiza na kuonea raia. Washairi wanashauri hili kupitia mashairi ya HAKI, MPAKA LINI?na SAMAKI MTUNGONI. Angalia ubeti huu katika MPAKA LINI?
        Mpaka lini, dhiki hii itafishwa?
Hadi lini, mnyonge atadunishwa?
Jambo hili, halina budi kukomeshwa,
     Mpaka lini tutasemewa?
·       Vile vile washairi hawa wameelekeza wanajamii waache majungu, umbeya na kusengenyana kwani hakuna faida yoyote kwa kufanyiana hayo ispokuwa kujenga uadui na chuki miongoni mwa wanajamii. Wanashauri hilo kupitia shairi la ULIMI
Usiropokeropoke, kwa wenzio kwanza sema,
Usipachikepachike, maneno yasio mema,
Useme wanufaike, kwa kauli yako njema,
                 Ewe ulimi sikia!
·       Isitoshe washairi hawa wamewashauri wanajamii wawe na misimamo hivyo waachane na tabia ya kuiga matendo ya watu wengine na  ambayo hayana maana yoyote wala msaada kwao kwani yaweza kusabababisha maafa makubwa kwao.Ushauri huu unasomeka vizuri katika mashairi ya SIHARAKIE MAISHA na USIWE BENDERA. Angalia ubeti huu katika shairi la USIWE BENDERA.
Usione haya, baya kukataa,
Ingawaje baya, ukajibobea,
Ukaambiwa haya, ukajifanyia,
Usiwe bendera, kufata upepo.
Kama vile haitoshi, malenga hawa wamewaelekeza viongozi kuto lewa madaraka na kusababisha kushindwa kutimiza majukumu yao na kusababisha jamii kuendelea kuwa duni. Maelekezo hayo yanaonekana vizuri katika shairi la SUKARI.
Utaumbuka ujue, sukari kiizoea,
Hukufunga utambue, utamu ukikukaa,
Lazima usijijue, ukishailafukia,
Haifai kubugia, sukari uiogope.
·       Wanajamii pia wanapaswa kuwa makini na matumizi ya mali na pesa wanazojichumia ili ziweze kuwafaa siku za mbeleni badala ya kuzitumia ovyo bila sababu maalum. Maelekezo haya yanapatikana vizuri katika shairi la ISRAFU.
Israfu ikimea,
Mali inayoyomea,
Watu watakuzomea,
Ukikosa egemea,
Mwenzangu nakuusia, israfu haifai.
·       Pia wanajamii wanaelekezwa kuwathamini wakulima wakikumbuka mchango wao mkubwa wanaotoa kwa jamii wa kuhakikisha jamii inapata chakula na pesa nyingi tu za kigeni na hivyo kusukuma maendeleo ya jamii, badala ya kuwatenga na kuwaona kama watu duni wasiostahili lolote. Haya yanaonekana kati ka shairi la MKULIMA.
Dharau wakielewa, kuna hatari mbeleni,
Mkulima ang’amuwa, naye akae mjini,
Hapo ndipo tutajua, mkulima naye nani,
Mkulima naye mtu, yafaa kuthaminiwa.

Ø FALSAFA
Mwandishi wa diwani hii anaamini kuwa umoja ,amani,na utulivu vitakuwepo endapo haki na usawa miongoni mwa wanajamii vitazingatiwa.Vile vile  anaamini kuwa jamii ikitilia mkazo suala la kilimo uchumi wan chi utaimarika sana.
Ø MSIMAMO/ MTAZAMO
Waandishi wanamtazamo wa kimapinduzi kwani wamejadili kwa kina matatizo yanayozikabili jamii kama vile matabaka,uongozi mbaya,unyonyaji,ukoloni mamboleo n.k na amependekeza suluhisho la matatizo hayo.
Ø FANI
Fani ni umbo la nje ya kazi za fasihi.Katika ushairi vipengele vya fani vinavyochunguzwa ni:-
A.  MUUNDO:
Hii ni sura, msuko,umbo au uwiano wa vipengele vyote vinavyojenga ushairi. Kuna vipengele kadhaa vinavyotumika kama sehemu ya muundo navyo ni;
v Idadi ya mishororo:
·       Tathlitha
Huu ni ushairi wenye mishororo mitatu kwa kila ubeti.Ushairi huu pia huitwa UTATU.Katika kazi hii ya MALENGA WAPYA yapo mashairi kadhaa yaliyosukwa namna hii, nayo ni kama vile PAYUKA, TUNZO, KUUNGE, UA na HALI HALISI.
           PAYUKA
1.     Nasikia makelele,
Ya ngoma ile ya lele,
Kuimba na kupayuka.
·       Tarbia
Ni ushairi uliosukwa kwa mishororo minne kwa kila ubeti.Tarbia pia hufahamika kama UNNE.Kidesturi shairi la huwa  na mishororo iliyogawanyika katika vipande viwili. Malenga wapya nao wameweza kuisuka kazi yao kwa kutumia muundo huu, mashairi yanayodhihirisha hilo ni pamoja na MAISHA NI KAMA NJIA, ULIMI,SISUMBUKIE KICHAA, NIPATIENI DAWA, NIPATE WAPI MWINGINE na SAMAKI MTONGONI.
                ULIMI
1.     Ulimi ninakuasa, nisemayo usikie,
       Mwenzio sijenitosa, nafasi sijutie,
       Ninachokuomba hasa, unifanye nivutie,
               Ewe ulimi sikia!
      
·       Takhmisa:
Ni ushairi wenye mishororo mitano katika kila ubeti.Ushairi huu huitwa pia UTANO au takhmisa. Kuna baadhi ya takhimisa hazina mgawo wa vipande viwili kama ilivyozoeleweka.Katika kazi hii malenga hawa wametumia muundo huu pia kama inavyojidhihirisha katika shairi la ISRAFU, SIHARAKIE MAISHA.
   
   ISRAFU
1.    Ali ulojichumia,
Ni yako nakubalia,
Lakini kiangalia,
Vipi unaitumia,
Mwenzangu nakuusia, israfu haifai.

·       Tasdisa:
Ni utungo wenye mishororo sita katika kila ubeti. Pia huitwa USITA, TARDISA au TASHLITA. Ingawa tungo hizi si maarufu sana lakini inaonekana katika diwani hii kama inavyojidhihirisha katika shairi la PUNDA msanii anasema;
      Toka ulipozaliwa, maishayo ni kizogo,
      Hujapata kuenziwa, waishi tirigivyogo,
      Nawe hujajielewa, u kiumbe hu kigogo,
      Kama ungefadhiliwa, usingebeba mizigo,
      Hakika ulionewa, hustahili kipigo,
      Haki umeitambua, idadi japo japo kidogo.

·       Sabilia:
Ni muundo ambao kazi ya kishairi hujengwa kwa mishororo saba au zaidi kwa ubeti. Kama ilivyo kwa tasdisa mashairi ya namna hii ni machache sana.Katika kazi ya MALENGA WAPYA kuna mfano wa shairi la muundo huu ambalo ni PASUA UWAPE UKWELI.Katika shairi hili msanii anasema;
    Ambaye tumekuridhi, asili yetu ni moja,
    Sukani tumekukabidhi, toka zama za mababu,
    Cheleza lete jahazi, uwapashe wapashike,
    Pasi kuwa na woga, viduhushi wachochezi,
    Uyakabili mawimbi, midomo yao wafyate,
    Na hizo zake tufani, virago vyao wafunge,
    Zipoze bila muhali, wawafate bwana zao,
    Kwa kupasua ukweli, visiwa vishuwarike,
    Kutugawa kwa mafungu, neema iengezeke,
    Hilo kwetu ni muhali, tufurahie maisha,
    Si dini wala si rangi, au la hata kabila.

v Idadi ya vipande:
Hiki ni kigezo kingine cha kuainisha muundo wa kazi za kishairi,kwa kigezo hiki shairi laweza kuwa na
·       Vipande viwili ( manthawi )
Katika muundo huu mshororo wa ubeti hugawika katika sehemu mbili; sehemu ya kwanza na ya pili.Mashairi kadhaa katika diwani hii yamesukwa katika muundo huu, nayo ni pamoja na ADUI,  KIFUNGO, KITENDAWILI, CHARUKA, NIPATE WAPI MWINGINE.
                       CHARUKA
Charuka chacharukaka, mambo kuyakimbilia,
Charuka kirukaruka,mipango kufikiria,
Charuka kikurupuka,mbali uweze fikia,
Kabla hujapotea,charuka chacharukaka.
·       Vipande vitatu ( ukawafi )
Kwa muundo huu mshororo wa ubeti wa shairi hugawika katika sehemu tatu; yaani sehemu ya kwanza, ya pili na ya tatu. Diwani ya MALENGA WAPYA imetumia pia muundo huu kupitia mashairi kadhaa kama vile KWA NINI?, TUNZO na HAKI.
                             HAKI
Haki watutisha, tusikuandame, kwa matendo yetu,
Watukorofisha, tusikuandame, kila penye kitu,
Mbona watutwisha, miba ituchome, kwenye huu mwitu,
                            Tutokwe na utu!
·       Kipande kimoja ( utenzi )
Katika muundo huu mizani ya mishororo huwa michache kati ya 4 hadi 12 nao husimulia habari fulani au tukio fulani. Katika diwani hii msuko huu unajidhihirisha kupitia shairi la PAYUKA.
       Nasikia makelele,
         Ya ngoma ile ya lele,
         Kuimba na kupayuka.
  
   Kupayuka kwenu huko,
         Mbona tu kokoriko,
         Sioni linalokuwa.

v Mbali ya idadi ya mishororo na vipande pia kituo hutumika kuainisha muundo wa kazi husika. Katika diwani hii ya MALENGA WAPYA msanii imetumia vituo tofauti kama vile;
·       Bahari:
Kituo cha namna hii maneno ya mshororo wa mwisho yanakaririwa kutoka ubeti mmoja hadi mwingine.Msuko huu unajidhihirisha katika HINA INAPAPATUKA, BAHARI na HALI HALISI.
·       Nusu Bahari:
Kituo cha namna hii maneno ya kipande kimoja hukariririwa ubeti mmoja hadi mwingine wakati ya kipande cha pili hubadilikabadilika. Muundo huu umejitokeza katika shairi la CHARUKA.
·       Kimalizio:
Katika kituo cha namna hii mshororo wa mwisho hubadilikabadilika kutoka ubeti mmoja hadi mwingine.Muundo huu umetumika vilivyo katika diwani hii hasa katika mashairi ya NINI WANANGU?, UTANIKUMBUKA, SOKOMOKO BAHARINI
MATUMIZI YA LUGHA
Katika ushairi kipengele cha lugha huhisisha taswira, tamathali za semi, methali, nahau,misemo na mkato wa maneno.
Taswira (picha/jazanda) hiki ni kipengele cha lugha ambacho huchora au huwasilisha wazo kwa kutumia picha au taswira mbalimbali,mfano katika shairi la SAMAKI MTUNGONI kuna taswira ya samaki ikiwakilisha watu wa tabaka la chini (watawaliwa), taswira ya mvuvi ni watu wa tabaka la juu (viongozi) na taswira ya mtungo ni sheria,kanuni au taratibu zinazotumiwa kuwabana watu wa tabaka la chini.
Ø Njiwa  mpenzi shairi la NIPATE WAPI MWINGINE?
Ø Punda- tabaka linalokandamizwa (shairi la PUNDA)
Ø Ua – mwanamke/ msichana (shairi la UA)
METHALI
Kuna methali mbalimbali zimetumiwa katika diwani hii; mfano
Ø Subira yavuta heri (shairi la SIHARAKIE MAISHA)
Ø Aisifie mvua kaloa mwilini mwake (shairi la SISUMBUKIE KICHAA)
Ø Fahari – wapiganapo nyasi ndizo huonewa (SOKOMOKO BAHARINI)
MISEMO
Ø Siharakie maisha (SIHARIKIE MAISHA)
Ø Sisumbukie kichaa (SISUMBUKIE KICHAA)
Ø Sokomoko baharini (SOKOMOKO BAHARINI)
TAMATHALI ZA SEMI
TASHIBIHA
Ø Ubaguzi umezama kama nguzo (shairi la TUNZO)
Ø Maisha ni kama njia (shairi la MAISHA NI KAMA NJIA)
Ø Yametolewa na kombe mithili ya gome la mti (shairi la BAHARI)
TASHIHISI
Ø Samaki wakasirika (shairi la SAMAKI MTUNGONI)
Ø Njaa imetuvamia (shairi la ADUI)
Ø Ua limejituliza (shairi la UA)
Ø Ulimi ninakuasa (shairi la ULIMI)
TASHITITI
Ø Katika shairi la MWABAJA MWASEMA NINI?
Ø Nasikia mwatunga,mwatungani washairi
TANAKALI SAUTI
Ø Parakacha mlio wa majani makvu (shairi la KWA NINI?)
Ø Kokoriko – shairi la MKULIMA
TAKRIRI
Ø Kuna takriri kituo cha mfano shairi la KWA NINI?
MKATO WA MANENO

Ø Kuna maneno yamekatwa ili kuepuka urari wa vina na mizani mfano “anong’ona (shairi la KWA NINI?).
Powered by Blogger.