Wamtaka Magufuli atimize ahadi zake

Rais mteule Dk John Magufuli
Geita. Mchungaji wa Kanisa la AIC Kalangalala la Geita Mjini mkoani hapa, limeitaka Serikali mpya inayoingia madarakani itimize ahadi zote walizozitoa kwa wananachi.
Imeelezwa kuwa, baadhi ya viongozi na Serikali katika chaguzi zilizopita, walitoa ahadi za maendeleo ambazo zingine hazijatekelezwa hadi sasa.
Akizungumza kwenye Ibada maalumu ya kumshukuru Mungu kwa kumaliza Uchaguzi Mkuu uliofanyika Oktoba 25 salama, Mchungaji Masanyiwa alisema Watanzania wana tabia ya kumshukuru Mungu kwa mambo yanayowapendeza na kuacha yale yanayowakwaza.
“Tunaambiwa tushukuru kwa kila jambo, linalotukera pia tunapaswa kupiga magoti na kumshukuru Mungu kwa hilo,” alisema Masanyiwa.
Alisema Serikali inayoingia madarakani ina kazi kubwa ya kurudisha imani ya Watanzania ambayo imetoweka, kutokana na hali ngumu ya maisha inayowakabili.
Alisema inatakiwa ionyeshe utofauti wake kwa matendo siyo kwa maneno.
Mchungaji Masanyiwa alisema maendeleo hayaletwi na Serikali pekee, bali kwa ushirikiano na wananchi wanaojituma kwa kufanya kazi.
Akizungumzia wagombea walioshindwa katika kinyang’anyiro hicho, aliwataka kumuunga mkono mgombea aliyechaguliwa ili kuijenga Tanzania mpya.
Akizungumza baada ya ibada, muumini Boniface Waika alisema kipindi cha ushindani kimemalizika viongozi wamepatikana kilichobakia ni kwa Watanzania kuendelea na mshikamano pamoja na kufanya kazi kwa bidii.
“Viongozi na Watanzania kwa ujumla, tunapaswa kutambua kuwa uchaguzi umemalizika tuendelee na maisha yetu na kwa wanasiasa nao wanatakiwa wajipange kwa uchaguzi mkuu mwingine wa 2020, kwa sasa tufanye kazi zaidi tuweke sisa kando,” alisema Waika .

Powered by Blogger.