Ushindi wa Bashe kupingwa mahakamani

Hussein Bashe
Nzega. Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Wilaya ya Nzega mkoani Tabora, kimetangaza kwenda mahakamani kupinga matokeo yaliyompa ushindi mgombea ubunge wa CCM, Hussein Bashe.
Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo la Nzega Mjini, Hawa Mniga alimtangaza Bashe kuwa mshindi baada ya kupata kura 18,774 dhidi ya 9,658 za Charles Mabula wa Chadema.
Akihutubia mkutano wa hadhara ulioandaliwa kuwashukuru wananchi kwa kukipigia kura chama hicho juzi, Mwenyekiti wa Chadema Jimbo la Nzega Mjini ambaye pia alikuwa mgombea, Mabula alisema uchaguzi huo haukuwa huru na haki kutokana na kasoro nyingi zilizojitokeza, ikiwamo baadhi ya vituo kuwa na zaidi ya karatasi tatu za matokeo.
Mabula alisema rushwa ilitawala siku ya kupiga kura pamoja na vurugu, mambo ambayo waliyaripoti kwa mamlaka zinazohusika lakini hazikuchukua hatua zozote.
Alisema hivi sasa wanasheria wao wanaendelea na mikakati ya kuandaa kesi na muda wowote itafunguliwa katika Mahakama Kuu Kanda ya Tabora, lengo likiwa haki itendeke na kila mgombea apate kura halali alizopigiwa na wananchi.
Mwenyekiti wa Chadema Wilaya ya Nzega, Omary Omary ambaye pia ni Diwani wa Kata ya Bukene aliwataka wananchi kuwa watulivu wakati chama hicho kinaendelea na mchakato wa kupinga matokeo hayo mahakamani.
Omary alisema uchaguzi huo ulighubikwa na kasoro nyingi ambazo zitaweza kutatuliwa na mahakama na kuongeza kuwa, wananchi wanapaswa kuendelea na shughuli zao, ikiwamo kudumisha amani na utulivu.
Msimamizi wa uchaguzi huo alisema ulikuwa huru na haki kwa kuwa kila chama kiliwakilishwa na mawakala na kwamba, kama kuna mgombea hakutendewa haki afuate utaratibu wa kuipata.
-
Powered by Blogger.