TMA: Mvua za El-Nino zinakuja

Chumba cha darasa la tatu katika Shule ya Msingi Izia, kikiwa kimeezuliwa paa kufuatia mvua kubwa iliyonyesha jana ikiambatana na upepo mkali mjini Sumbawanga mkoani Rukwa. Picha Mussa Mwangoka
Dar/mikoani. Mamlaka ya Hali ya Hewa nchini (TMA), imewatahadharisha wananchi kuwa mvua kubwa za El-Nino zinatarajiwa kunyesha mwezi huu na Desemba, katika mikoa ya Kanda ya Ziwa, Kanda ya Magharibi na Nyanda za Juu Kaskazini mashariki.
TMA imesema mvua hizo zinakuja kutokana na mifumo ya hali ya hewa kuzidi kuonyesha hali hiyo.
Mamlaka hiyo imewataka wakulima, wafugaji, mamlaka za wanyamapori, mamlaka za maji na afya kufuata ushauri wa wataalamu wa sekta husika ili kutekeleza mipango isiyoweza kuathiriwa na mwelekeo wa hali ya hewa ya msimu wa mvua za vuli.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Dk Ladislaus Chang’a alisema jana katika taarifa kuwa maeneo yanayopata mvua mara moja kwa mwaka ya Dodoma, Singinda, Ruvuma, Lindi, Mtwara, Songea, Mbeya, Iringa, Njombe, Tabora, Kigoma Rukwa na Katavi zinatarajiwa kuanza kati ya wiki ya pili na ya nne ya mwezi huu.
“Mvua hizo zimeanza kujiimarisha katika mikoa ya Kigoma, Tabora na Katavi na zinatarajiwa kusambaa katika maeneo mengine mwezi huu,” alisema.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, wilaya za Kondoa, Kongwa na maeneo ya Singida vijijini pamoja na Dodoma yanatarajiwa kupata vipindi vya mvua mwanzoni mwa mwezi huu.
Alisema mvua za El-Nino zinatokana na kuendelea kuongezeka kwa joto katika maeneo ya Bahari ya Pacific na kusababisha mifumo mingine ya hali ya hewa kuvurugika.
Chang’a alisema mabadiliko hayo yamesababisha mwitikio wa mfumo wa hali ya hewa katika Bahari ya Hindi kuwa na mchango hasi, kinyume na ilivyotarajiwa katika mwenendo wa mvua za vuli nchini kwenye kipindi Oktoba na kusababisha vipindi virefu vya upungufu wa mvua katika mikoa ya Morogoro, Pwani na Dar es Salaam.
“Hata hivyo, mifumo ya hali ya hewa katika Bahari ya Hindi kwenye ukanda wa Afrika Mashariki na ukanda wa Pwani ya Angola katika Bahari ya Atlantic imeanza na inaendelea kuimarika,” alisema.
Kaimu mkurugenzi huyo alivitaka vyombo vya habari kufuatilia, kupata na kusambaza taarifa sahihi za mienendo ya hali ya hewa kutoka TMA na kutumia wataalamu wa sekta husika kuandaa na kufikisha taarifa za masuala mtambuka ya hali ya hewa kwa jamii.
Wakati TMA ikitoa taarifa hiyo, tayari mvua imeanza kunyesha kwa kasi ikiwa na upepo mkali katika mikoa ya Mwanza na Mbeya na kukwamisha baadhi ya shughuli za jamii katika sehemu hizo.
Katika mkoa wa Mbeya, mvua iliyoambatana na upepo mkali iliyonyesha jijini hapa jana, ilisababisha kuta kubomoka na mabati ya nyumba nyingi kuezuliwa.
Mvua hiyo ilinyesha kwa dakika 20, lakini ilikuwa na mawe ya theluji, huku ikiambatana na upepo mkali kutoka Kaskazini kwenda Kusini.
Nyumba zlizoezuliwa mapaa ni pamoja na mabanda ya biashara ya mitaa ya Sokoine, Jakaranda na Mwanjelwa.
Katika Mtaa wa Mwambene, wigo wa nyumba mbili tofauti ulianguka huku mabati ya nyumba nyingi yakinyofolewa.
Kutoka jijini Mwanza, mvua kubwa iliyonyesha kuanzia alfajiri ilisababisha kufungwa kwa Uwanja wa Ndege na mwanafunzi mmoja kusombwa na maji.
Kutokana na mvua hizo, usafiri wa kuingia na kutoka katikati ya jiji hilo ulikuwa wa shida na kusababisha wafanyakazi wengi kuingia ofisini kuanzia saa 4:00 asubuhi kutokana na foleni kubwa za magari zilizokuwa barabarani.
Maeneo ya Mabatini na Kirumba ambayo hukumbwa na mafuriko mara kwa mara yalijaa maji na kusababisha watu kulazimika kuyachota ndani na kumwaga nje.
Mkazi wa Mabatini, Ronaida Mtatina alisema vitu vyake vilivyokuwa kwenye kibanda cha biashara vilisombwa na maji na vingine kulowana.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Charles Mkumbo alisema mwanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Nyamanoro, Zainab Shaaban (18) alisombwa na maji eneo la Nyamanoro wakati akivuka kwenda shuleni, lakini haijathibitika kama alifariki au la.
Meneja wa Uwanja wa Ndege wa Mwanza, Ester Madale alisema kutokana na mvua hiyo ulijaa maji na ilipotimu saa 3:00 asubuhi walilazimika kusitisha huduma za kutua na kuruka kwa ndege hadi saa 8:00 mchana.
Imeandikwa na Fidelis Butahe, Lauden Mwambona na Jesse Mikofu
-
Desktop View
Powered by Blogger.